Mbinu 2 Za Kukusaidia Kutunza Muda Wako.

Mbinu 2 Za Kukusaidia Kutunza Muda Wako.

Katika maisha ili uweze kufanikiwa, unahitaji rasilimali. Kati ya rasilimali zote ambazo Mungu ametubariki, Muda ndiyo rasilimali ya muhimu sana kuliko rasilimali zote na inapaswa kutunzwa kwa umakini wa hali ya juu. Hii ni kwa sababu, muda ukipotea hauwezi kuurudishwa (non- renewable resource). Muda ni wa thamani kuliko pesa kwani ukipoteza pesa, unaweza kutafuta nyingine ukapata na maisha yakaendelea. Lakini ukipoteza muda hauwezi kuurudisha. Hivyo, ili uweze kufanikiwa ni lazima uweze kufahamu jinsi ya kutunza muda wako. Katika Makala ya leo, nitakushirikisha mbinu mbili ambazo zitakusaidia kutunza muda wako ili uweze kufanikiwa.
Mbinu 2 za kukusaidia kutunza muda wako uweze kufanikiwa.
1. Panga vitu vyako katika mpangilio maalumu (systematic arrangement).
Jambo la kwanza kabisa ambalo litakusaidia kutunza muda wako ni kupanga vitu vyako katika mpangilio maalumu. Kama ni nyumbani weka mpangilio maalumu unaoonesha vitu vyako vitakaaje. Kwa mfano, nguo za kazini mahali zinapokaa, funguo za nyumba, ufunguo wa gari, vitabu na kadhalika. Mpangilio huu utakusaidia kufahamu kila kitu mahali kinapokuwa na hivyo kukusaidia kuokoa muda ambao ungeweza kuupoteza kwa kutafuta vitu. Kama ni ofisini, fanya mpangilio mzuri wa aina za faili. Mfano weka sections mbalimbali zinazotofautisha aina ya faili zilizopo ofisini kwako. Mfano unaweza kutofautisha aina za faili kama vile: Faili za barua, faili za nyaraka, faili za mikataba, faili za mambo ya fedha na kadhalika. Hii itakusaidia kutumia muda mfupi sana kutafuta faili zako. Pia unaweza kuweka mpangilio wa vitu vingine vilivyopo ofisini kwako kama vile vitabu, daftari, peni, mihuri na kadhalika. Kwa kufanya hivyo, utaonkoa muda mwingi sana ambao utautumia kufanya shughuli zingine.
2. Panga vitu vyako siku moja kabla.
Jambo la pili ambalo unaweza kulitumia kutunza muda wako ni kupanga vitu vyako siku moja kabla. Hapa kama unaenda kazini, unaweza kupanga nguo ambazo utavaa na unazitenga kabisa. Pia unatenga vitu vingine ambavyo utakwenda navyo kazini, kama vile vitabu, notebook, laptop na kadhalika. Hii itakusaidia unapoamka kesho, usipoteze muda muda kuanza kutafuta vitu ambavyo unapaswa kuenda navyo kazini. Kwa kufanya hivyo, utaokoa muda mwingi sana ambao utautumia kwa kuwahi kwenye eneo lako la kazi na hivyo kuongeza ubora wa kazi yako.
Kwa leo niishie hapo, nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakusaidia kutunza muda wako vizuri ili uweze kufanikiwa kwenye maisha yako. Kumbuka kuwa muda ndio rasilimali ambayo ikipotea hauwezi kuirudisha. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuandika hapo chini. Pia kama una swali lolote kuhusiana na mada ya leo, usisite kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante sana na karibu kwenye Makala zinazokuja.

Rasilimali 3 Unazohitaji Kutimiza Malengo Yako

Rasilimali 3 Muhimu Unazohitaji Uweze Kutimiza Malengo Yako

Watu wengi huwa wanaweka malengo makubwa katika maisha yao lakini wanaofanikiwa kutimiza malengo yao ni wachache sana. Hata wewe unaweza kujiuliza, mwaka uliopita ulikuwa umeweka malengo, je umeweza kutimiza malengo yako kwa kiwango gani? Jibu unalo. Lakini pia mwaka huu inawezekana una malengo ambayo tayari umeyaweka. Ili uweze kutimiza malengo yako, kuna rasilimali ambazo lazima uwekeze. Kila lengo unalopanga litahitaji rasilimali hizi. Katika Makala ya leo nitakushirikisha rasilimali tatu muhimu unazohitajika kuwa nazo ili uweze kutimiza malengo yako.
Rasilimali 3 muhimu unazohitaji uweze kutimiza malengo yako
1. Muda

Muda ndio rasilimali ya kwanza na muhimu sana katika maisha ambayo unahitaji kuweza kufikia malengo yako. Ni rasilimali ambayo inapaswa kulindwa na kutumika kwa uangalifu mkubwa sana. Hii ni kwa sababu muda ukipotea hauwezi kurudishwa (non-renewable resource). Hivyo ili uweze kutimiza malengo yako unapaswa kutumia vizuri muda wako kwenye kile tu ulichojiwekea malengo. Usiruhusu muda wako kupote ovyo. Kumbuka kuwa unaweza kupotesa pesa na ukatafuta nyingine ukaipata. Lakini hauwezi kuurudisha muda uliopotea. Mara nyingi huwa ninaona watu wapo kijiweni, na ukiwasalimia wanasema tupo hapa tunapoteza muda! Wanapoteza rasilimali ya thamani ambayo hawawezi kuirudisha. Hivyo, muda ni rasilimali ya thamani sana kwenye mafanikio yako.
2. Watu
Rasilimali nyingine ambayo utahitaji kuweza kufanikisha malengo yako ni watu. Utahitaji watu wa kukushika mkono, utahitaji watu wa kukusaidia kwenye kazi yako na utahitaji watu kwenye kila unachokifanya.
3. Fedha
Fedha pia ni rasilimali nyingine ambayo ni ya muhimu ili uweze kutimiza malengo yako. Fedha inahitajika katika kuendesha mradi au biashara uliyoianzisha.
Swali la msingi ni hili, kwa nini watu wengi huwa wanashindwa kutimiza malengo yao?
Jibu ni kuwa, watu wengi wanashindwa kutimiza malengo yao kwa sababu huwa wanatapanya rasilimali zao kwenye malengo mengi. Unakuta mtu ameanza biashara ya duka, mara akasikia kilimo cha matikiti kinalipa akaamua kulima matikiti, baadaye akasikia kuwa biashara ya mtandao inalipa akaamua pia kufanya biashara hiyo. Kumbuka kuwa kila lengo linahitaji rasilimali hizi muhimu tatu kama nilivyozielezea hapo juu yaani muda, watu na fedha. Hivyo ukiwa na malengo mengi utashindwa kufanikiwa kwa sababu utakuwa unarashia kwenye kila lengo. Hivyo, ili uweze kufanikiwa kutimiza malengo yako, ni lazima uwekeze nguvu kwenye lengo moja. Nguvu zako zote na rasilimali zako zote ni sharti uziwekeze kwenye lengo moja, hapo mafanikio utayaona. Kumbuka kuwa mafanikio hayaji kwa kufanya vitu vingi, bali yanakuja kwa kufanya kitu kimoja kwa weredi wa hali ya juu. Weredi huu unapatikana pale tu ambapo utakuwa umewekeza rasilimali zako zote kwenye lengo lako yaani pesa zako zote, muda wako wote na watu wa kukusaidia kufikia lengo lako.
Kuna neno la kingereza linalosema FOCUS. Maana ya neno focus ni kuzingatia na kufanya kile ulichokipanga na kukataa kila vishawishi ambavyo vitakuhamisha kwenye kile unachokifanya. Hivyo ili uweze kutimiza malengo yako ni lazima uwe na Focus, fanya kitu kimoja na usiruhusu upepo wowote ambao unaweza kuja kutaka kukuhamisha kwenye kile unachokifanya.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakusaidia kuweza kufanikisha malengo yako. Kama una maoni au swali, usisite kuandika hapo chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu kwenye Makala zinazofuata.

Jinsi Ya Kutambua Kusudi La Maisha Yako

Jinsi kugundua Kusudi la Maisha Yako

Katika maisha, Mungu amemuumba kila mwanadamu na kumleta duniani kwa kusudi maalumu. Hivyo Mungu amempatia kila mwanadamu uwezo mkubwa ndani yake, kila mtu kwa aina yake ili aweze kutimiza kusudi lake la kuwa duniani. Hata wewe, Mungu ameruhusu uwepo duniani kwa kusudi maalumu. Ukigundua kusudi la maisha yako, utaweza kufanya mambo makubwa sana. Kwa bahati mbaya sana, watu wengi wanazaliwa mpaka wanakufa bila kutambua kusudi la maisha yao na hivyo kushindwa kutumia uwezo mkubwa ambao Mungu ameuweka ndani yao ambao kama wangeutumia wangeweza kufanya mambo makubwa sana Duniani na wangekuwa mbaraka mkubwa kwa watu wengine. Katika Makala ya leo nitakushirikisha jinsi ya kutambua kusudi la maisha yako ili uweze kufanikiwa kufanya mambo makubwa.
Jinsi ya kutambua kusudi la maisha yako uweze kufanikiwa.
1. Chunguza nguvu (umahili) wako.
Ili uweze kugundua kusudi la maisha yako, njia ya kwanza ni kuchunguza kwenye uwezo wako wa ndani. Hebu jichunguze, ni vitu gani ambavyo ukivifanya, unavifanya kwa ubora wa hali ya juu. Kwa mfano inawezekana ukawa una uwezo wa kuongea vizuri mbele za watu, kuimba, kucheza mpira, kuandika na kadhalika. Kutambua uwezo ulio nao ni hatua kubwa sana ya kutambua kusudi ambalo Mungu amekuleta Duniani. Hii itakusaidia kuwekeza nguvu kubwa kwenye eneo ambalo una umahili wa kutosha na kukufanya uweze kufanya mambo makubwa na ya kushangaza. Kumbuka kuwa kila uwezo au umahili ulionao una uwezo kabisa wa kuubadilisha na ukawa ni chanzo cha kuuingizia kipato.
2. Ongea na watu wa karibu wakuambie uwezo wako upo kwenye maeneo gani.
Njia nyingine ya kutambua kusudi la maisha yako ni kuongea na watu wako wa karibu. Hawa wanaweza kuwa ni wale watu unaowaamini kuwa watakuambia ukweli wa jinsi ulivyo. Mfano: marafiki wako wa karibu, mke au mme wako, wazazi na kadhalika. Waulize maswali wakuambie ni kitu gani unapokuwa unakifanya, unaonekana umekifanya vizuri sana na watu huwa wanakifurahia. Kusanya majibu ambayo watakuwa wamekupatia. Majibu uliyoyapata, yatakusaidia kugundua uwezo wako na hivyo kuweza kufahamu kusudi la maisha yako.
3. Fikiria ni vitu gani ulivyowahi kuvifanya na watu wakavifurahia (Past experience).
Njia nyingine ambayo unaweza kugundua kusudi la maisha yako ni kwa kuangalia uzoefu wako wa nyuma (past experience). Hapa unaangalia mambo yote ambayo uliwahi kuyafanya na ukayafurahia na pia watu wakakupongeza kuwa umefanya vizuri. Mfano, inawezekana kuna siku uliwahi kusimama mbele ya watu na ukaongea vizuri, baada ya kumaliza kuongea watu wakakupongeza sana kuwa umeongea vizuri sana. Hii ni dalili nzuri kuwa una uwezo mkubwa wa kuongea mbele ya watu kwa sababu si kila mtu anaweza kusimama na akaongea mbele za watu vizuri. Huo ulikuwa ni mfano tu, sasa unaweza kufikiria mambo yote uliyowahi kuyafanya na watu wakakupongeza.
Baada ya kutumia njia nilizokuelezea hapo juu, sasa unaweza kujua ni mambo gani una uwezo kubwa wa kuyafanya. Kwa kuangalia mambo hayo, sasa unaweza kufikiria ni kazi au shughuli gani unaweza kuifanya ambayo inahusiana na uwezo ulio nao. Kazi utakayoifanya ndilo litakuwa ni kusudi lako la maisha kwa sababu itakuwa ni kazi ambayo utakuwa unaifurahia na ni kazi ambayo inakuwezesha kutumia uwezo wote ambao Mungu ameuweka ndani yako. Hivyo, utafanya kazi kwa viwango vya juu na Kufanikiwa sana.
Kwa leo niishie hapo. Kama una maoni yoyote kuhusiana na mada ya leo, usisite kuweka maoni au swali lolote, usisite kuweka hapo chini. Pia kama unahitaji ushauri wowote, usisite kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazokuja.

Jinsi Ya Kutengeneza Kipato Kinachokua Kila Siku

Kutengeneza Kipato endelevu Kinachokua Kila Siku

Mfumo wetu wa elimu huwa unatufundisha aina mbili za elimu: Aina ya kwanza ni elimu ya kujua kusoma, kuandika na kuhesabu (scholastic education). Hii ni elimu ambayo inakuwezesha kujua jinsi ya kusoma, kuandika na kuhesabu. Aina ya pili ya elimu ni elimu ya ujuzi (professional education). Aina hii ya elimu ndiyo inayozalisha wataalamu mbalimbali kama vile madaktari, walimu, wahandishi na kadhalika. Kuna aina ya tatu ya elimu ambayo haifundishwi darasani, nayo ni elimu ya msingi kuhusu fedha (financial education). Hii ni elimu inayokuwezesha kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato, jinsi ya kutumia pesa yako na jinsi ya kuwekeza pesa yako. Katika Makala ya leo nitakushirikisha aina hii ya tatu ya elimu na nitazungumzia jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku (Passive income).
Jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku.
Kwanza kabisa, ili uweze kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato ambacho kitakuwa kinakuwa kila siku na endelevu, ni lazima nianze kwanza kuelezea aina ya vipato. Watu wote wanaofanya kazi duniani na kupata kipato, vipato vyao vimegawanyika sehemu kuu tatu: aina hizi za vipato ni active income, portfolio income na passive income. Nitaelezea kila aina ya vipato.
Aina za vipato:
1. Active income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inakutaka wewe uwe mahali pa kazi, ufanye kazi ndio ulipwe. Hii inajumuisha watu walioajiriwa ambao wanalipwa baada ya kuwa wamefanya kazi. Maana yake ni kuwa, kama hakufanya kazi hawawezi kulipwa. Pia inajumuisha watu waliojiajiri ambao ni lazima waende kwenye maeneo yao ya kazi, wafanye kazi ndio waweze kupata kipato. Kwa lugha rahisi ni kuwa, active income ni aina ya kipato ambayo unalipwa tu pale unapokuwa umefanya kazi. Kama hukufanya kazi huwezi kulipwa.
2. Portfolio income
Hii ni aina ya kipato inayopatikana mtu anapoamua kuwekeza pesa yake kwenye maeneo ambayo itaongezeka thamani kama vile kuwekeza kwenye kununua hisa, kuwekeza kwenye mifuko ya pamoja na kuwekeza kwenye hatifungani. Kwa ligha rahisi ni kuwa, unawekeza pesa yako kwenye maeneo ambayo baadaye utapata faida.
3. Passive income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inapatikana bila ya ulazima wa wewe kuwepo mahali pa kazi. Biashara yako inakuwa inajiendesha yenyewe bila ya wewe kufanya kazi. Kwa mfano: unapokuwa umeamua kuandika kitabu na ukamaliza, basi kitabu hicho utakiuza maisha yako yote. Kazi kubwa utaifanya mwanzoni tu wakati wa kuandika. Lakini baada tu ya kumaliza kuandika kazi yako itakuwa ni kuuza tu. Hivyo kitabu chako kinakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato kikubwa na endelevu (passive income). Mfano mwingine ni unapokuwa umeandaa kozi yako na ukaiweka mtandaoni. Kazi yako kubwa itakuwa tu mwanzoni wakati wa kuandaa kozi yako lakini ukishamaliza, basi inakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato endelevu bila ya ulazima wa wewe kufanya kazi nyingine ya ziada. Lakini pia unaweza kuandaa video zako za mafunzo na ukaziweka YouTube. Baada ya kuwa umepata wafuasi wa kutosha na video zako zikawa na watazamaji wengi, basi unaweza kutengeneza kipato endelevu (passive income) kwani YouTube itakuwa inakulipa kupitia matangazo yake ambayo itayaweka kwenye video zako.
Kama njia yako ya kutengeneza kipato ni ile ya kwanza (active income) basi unaweza kuifanya lakini uwe na malengo ya kuandaa njia nyingine ambayo itakusaidia kupata kipato endelevu ambacho hakitakulazimu kufanya kazi (passive income). Hii ni kwa sababu, kadiri unavyoendelea kufanya kazi, nguvu zako zinaendelea kupungua hivyo ni muhimu kuwa na njia ya kutengeneza kipato ambayo hakitakulazimu kufanya kazi.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ya jinsi ya kutengeneza kipato kinachokua kila siku. Kama una maoni au swali, usisite kuweka maoni yako hapo chini. Pia kwa ushauri wowote usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu katika Makala zinazokuja.

Mambo 4 Ya Kufanya Unapoamka Asubuhi

Mambo 4 ya kufanya unapoamka asubuhi

Jinsi unavyoianza siku yako kila unapoamka asubuhi ina mchango mkubwa sana katika mafanikio yako. Watu wengi huwa wanakosea jinsi wanavyoanza siku asubuhi na hivyo kushindwa kupata mafanikio. Kisaikolojia, ukishindwa kuanza siku yako vizuri, utakuwa umeharibu siku nzima kwani utashindwa kupata matokeo makubwa uliyokuwa unayakusudia. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo manne muhimu unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi ili uweze kupata mafanikio makubwa katika maisha yako.
Mambo 4 muhimu ya kufanya kila unapoamka asubuhi.
1. Anza na Mungu.
Mungu ndiye muweza wa kila kitu. Ndiye anayetupa uhai, uwezo na nguvu za kufanya kazi zetu. Hivyo jambo la kwanza kabisa, uanpoamka asubuhi, anza na maombi. Muombe Mungu akusaidie katika kazi zako zote unazoenda kuzifanya. Hii itakusaidia kujenga mahusiano mazuri na Mungu na hivyo kukuwezesha kufanikiwa kwenye kazi zako. Pia unapoanza na Mungu, unapata utulivu wa akili kwa kuwa utakuwa umekabidhi mipango, na kazi zako zote kwake.
2. Angalia malengo yako ya muda mrefu.
Jambo la pili la kufanya kila unapoamka asubuhi ni kupitia malengo yako ya muda mrefu. Hapa utaangalia kama kazi unazoenda kuzifanya ndani ya siku ya leo zinatimiza malengo yako ya muda mrefu au la. Hii itakusaidia kutokuhama kwenye malengo yako uliyojiwekea ya muda mrefu. Kumbuka kuwa, ili uweze kufanikiwa ni lazima uwe na malengo makubwa uliyojiwekea. Kwa mfano , kwa mwaka huu umeweka malengo ya kuandika kitabu. Hivyo, unapoanza siku yako angalia kazi unazoenda kuzifanya zisikuhamishe kwenye lengo lako la muda mrefu.
3. Soma, angalia au sikiliza kitu kinachokutia nguvu na kukupa hamasa.
Kila unapoamka asubuhi, jambo la tatu unalopaswa kulifanya ni kusoma kitabu ambacho kitakupa hamasa (inspirational book). Lakini pia kama huna kitabu unaweza kuangalia video ambayo ina mada zinazohamasisha. Hii itakupa nguvu na hamasa kufanya kazi kwa bidi kutimiza malengo yako. Usianze siku yako kwa kuangalia udaku au kuangalia taarifa. Kumbuka kuwa unapoangalia taarifa, utapata taarifa nyingi ambazo nyingine ni za kusikitisha. Ukifanya hivyo utakuwa umeharibu hamasa ya kufanya kazi kwa siku nzima. Kumbuka kuwa jinsi unavyoianza siku yako asubuhi, ndio itaashiria jinsi siku nzima itakavyokuwa. Kama utaichosha akili yako kwa kusoma udaku asubuhi, utakuwa umeharibu utendaji wako wa siku nzima.
4.Hakikisha unaorodhesha vitu ambavyo utavifanya kwa siku nzima.
Baada ya kuwa umefanya mambo matatu kama nilivyoelezea hapo juu, jambo linalofuata ni kuorodhesha mambo yote ambayo utayafanya kwa siku nzima. Kuna faida kubwa sana kuorodhesha mambo unayoenda kuyafanya. Faida ya kwanza ni kutokupoteza muda kwani utakuwa unafahamu mambo unayopaswa kuyafanya, lipi linaanza na lipi linafuata. Faida ya pili ni kuhakikisha kuwa unafanya mambo yale tu ambayo umeyapanga yafanyike kwa siku hiyo hivyo kukusaidika kutimiza malengo yako ya muda mrefu uliyojiwekea.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi. Jambo la msingi ni kuchukua hatua. Kumbuka kuwa, mafanikio makubwa yanajengwa na vitu vidogo vidogo tunavyovifanya kila siku. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazokuja.

Mambo 3 Wanayofanya Watu Waliofanikiwa.

Mambo 3 muhimu wanayofanya watu Waliofanikiwa Duniani.

Katika kufanya utafiti na kusoma kwangu vitabu nilitamani kujifunza jinsi watu waliofanikiwa na matajiri duniani wanavyoishi. Lengo la kusoma kwangu vitabu lilikuwa ni kujua siri ya maisha yao na kufahamu vitu vya tofauti wanavyofanya na hivyo kuweza kujitofautisha na watu wa kawaida. Miongoni mwa watu ambao niliowahi kusoma vitabu vyao ni aliyekuwa Rais wa Marekani, Donard Trump pamoja na matajiri wengine wengi. Katika kusoma kwangu, niligundua kuna mambo matatu muhimu ambayo watu waliofanikiwa huwa wanafanya. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo matatu muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa Duniani ambayo hata wewe unaweza kuyafanya ili uweze kufanikiwa.
Mambo 3 muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa duniani.
1. Ni wasomaji wazuri sana wa vitabu.
Jambo la kwanza kabisa ambalo watu waliofanikiwa hufanya ni wasomaji wazuri sana wa vitabu. Ukifuatilia matajiri wote wakubwa wa dunia kama vile Donard Trump, hutumia muda wao mwingi katika kuongeza maarifa kupitia usomaji wa vitabu. Lengo kubwa la usomaji wao wa vitabu ni kuongeza ujuzi na maarifa kuhusiana na biashara pamoja na shughuli zao zingine wanazozifanya. Hivyo, hata wewe kama unataka kufanikiwa kwenye malengo yako, wekeza muda wako katika kujenga ujuzi wako kwenye shughuli unayofanya ili uweze kupata matokeo makubwa. Akili ya mwanadamu ni kama panga la kukatia ambalo linatakiwa kunolewa ili liweze kukata kwa urahisi. Tunanoa akili zetu kwa kujifunza maarifa mapya kila siku kupitia usomaji wa vitabu. Hivyo, kama unataka kufanikiwa, panga ratiba ya kusoma vitabu kila siku.
2. Hawaishi maisha ya kujionyesha ili kuridhisha watu.
Changamoto kubwa iliyopo kwa watu wengi ni kuishi maisha yasiyokuwa na uhalisia. Unakuta mtu anatamani kuishi maisha ya juu kuliko kipato chake. Anatamani awe na gari, awe na nguo za gharama kubwa, apange kwenye nyumba ya bei ya juu wakati kipato chake hakiwezi kuhimili gharama hizo. Wanaishi maisha yao ili kuwaridhisha watu. Matokeo yake ni kuingia kwenye madeni na kupata stress za maisha. Watu waliofankiwa hawafanyi hivyo. Wanaishi maisha yao kulingana na kipato chao. Hawaishi kuwaridhisha watu. Hivyo, ili uweze kufanikiwa, unapaswa kuwa na bajeti na matumizi yako yasizidi kipato chako. Ishi maisha yako na siyo kuishi ukishindana na watu.
3. Matumizi yao makubwa ya pesa yanaenda kwenye uwekezaji.
Watu waliofanikiwa wanapopata kipato chao hawaelekezi kipato chao chote kwenye matumizi ya kawaida. Asilimia kubwa ya kipato chao huwa wanakielekeza kwenye uwekezaji. Kila wanapopata kipato, asilimia Fulani wanawekeza kwenye biashara, kwenye kununua hisa, kwenye kununua hatifungani na kadhalika. Kabla ya kuanza kufanya matumizi ya kawaida, jambo la kwanza kabisa huwa wanatenga pesa kwa ajili ya uwekezaji. Hebu jiulize swali hili, kila unapopata pesa, ni asilimia ngapi unawekeza? Kama hauwekezi, na pesa yote unatumia kwa matumizi ya kawaida, basi hautaweza kufanikiwa. Haijalishi unapata kiasi gani cha pesa. Hata kama ni kidogo kiasi gani, kumbuka kutenga kwanza kiasi cha pesa ambacho utawekeza.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo wanayofanya watu waliofanikiwa ambayo hata wewe pia ukifanya utapata mafanikio makubwa. Kama una maoni au swali lolote usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana name kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazofuata.

Vikwazo 3 Vya Kushinda Ili Utimize Malengo Yako

Jinsi ya kutimiza MALENGO yako

Katika maisha kila mtu ana malengo au ndoto Fulani anayotamanai kuikamilisha ili aweze kufikia mafanikio. Hata wewe inawezekana una ndoto katika maisha yako unayotamani kuifikia. Inawezekana unatamani kufanya mambo makubwa kabla hujaondoka duniani. Lakini si wote wanaokuwa na malengo na ndoto katika maisha yao ambao wameweza kutimiza ndoto zao. Kuna sababu ambazo zinawafanya watu wengi washindwe kutimiza ndoto walizo nazo. Katika Makala ya leo nitakushirikisha vikwazo vitatu (3) ambavyo ni lazima uvishinde ili uweze kutimiza malengo yako.
Vikwazo 3 ambavyo ni lazima uvishinde kutimiza malengo yako.
1. Kutokuamini katika uwezo ulio nao.
Watu wengi sana wameshindwa kufikia kilele cha ndoto zao kwa sababu ya kutokuaminni katika uwezo walio nao. Hii inatokana na jinsi walivyoaminishwa toka wakiwa watoto, maneno ya walimu wao, maneno ya marafiki zao, mazingira waliyokulia na kadhalika. Wamekuwa wakisikia kwenye masikio yao maneno ya kukatisha tamaa kuwa hawawezi. Inawezekana hata wewe umekatishwa tamaa na wazazi, walimu, marafiki kuwa hauwezi. Ninataka nikuhakikishie kuwa una uwezo ndani yako wa kufanya makubwa na kutimiza malengo yako. Amini katika uwezo ulio nao na uchukue hatua. Amini kuwa una uwezo wa kuwa mtu mkubwa, amini kuwa unaweza kuwa bilionea na kadhalika. Usijidharau, una uwezo mkubwa sana uliojificha ndani yako ambao unachohitajika tu kufanya ni kuchukua hatua.
2. Kuamini kuwa kuna mtu yupo mahali fulani atakusaidia.
Katika maisha, hatma ya maisha yako unaipanga wewe mwenyewe. Hakuna mtu ambaye yupo kwa ajili ya kukusaidia katika maisha yako. Hata kama yupo, tambua kuwa sio wajibu wake kufanya hivyo. Hivyo ni lazima uchukue hatua wewe mwenyewe kwa asilimia mia moja kutimiza malengo yako. Kumbuka kuwa unapokuwa umeanza kuchukua hatua watu watakuja kukushika mkono wakiona tayari umekwisha anza. Kama malengo yako ni kuwa mwandishi, anza kuandika, kama ni kufanya biashara anza kwa kiasi chochote ulicho nacho. Hata kama hauna mtaji kabisa, tumia nguvu zako kuweza kupata mtaji wa kuweza kuanzisha biashara yako. Jambo la kuzingatia hapa ni wewe kuanza, haijalishi una hali gani. Unapokuwa umeanza, fursa zingine za kukufanya usonge mbele zitafunguka.
3. Kukata tamaa.
Kikwazo kingine ambacho kinaweza kukufanya ushindwe kutimiza malengo yako ni kukata tamaa. Watu wengi wameshindwa kutimiza malengo yao kwa sababu baada ya kuanza walipopata changamoto walikata tamaa na wakaamua kuacha malengo yao. Hata wewe inawezekana tayari umeamua kuchukua hatua, jambo la msingi ni kuendelea haijalishi utapitia changamoto kubwa kiasi gani, usikate tamaa. Endelea kupambana kwani mafanikio hayaji kwa urahisi, yanahitaji kujitoa kwa nguvu zako zote na akili yako yote. Hapa unatakiwa kupuuza maneno yote uliyoambiwa na ambayo unaweza kukutana nayo kuwa hauwezi. Maneno yoyote yale ambayo yatakuvunja moyo na kukukatisha tamaa yapuuze na upige hatua na mafanikio utayaona. Kama bado haujachukua hatua ni lazima utambue kuwa unapoanza kuchukua hatua kutimiza malengo yako kuna wakati utapitia nyakati ambazo zitakufanya ukate tamaa. Usikubali endelea kuchukua hatua mpaka pale utakapokuwa umetimiza kusudi la maisha yako.
Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yatakusaidia kuchukua hatua muhimu sana kwa ajili ya kutimiza malengo yako. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni au swali lako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazokuja.

Kila Aliyefanikiwa Alifanya Uamuzi Huu Mkubwa.

Kila Aliyefanikiwa Alifanya uamuzi huu Mkubwa

Katika maisha kila mmoja wetu anahitaji kufanikiwa. Lakini katika mafanikio kuna kanuni ambazo kila ambaye anahitaji kufanikiwa anapaswa kuzifahamu na kuzifanyia kazi. Na ndio maana katika maisha kuna watu waliofanikiwa na ambao hawajafanikiwa japokuwa wote wanawekeza juhudi kubwa kutafuta maisha. Hivyo kuna moja ambalo watu waliofanikiwa huwa wanalifanya na hivyo kuwatofautisha na watu wengine ambao hawafanikiwi. Katika Makala hii, tutaangalia jambo kubwa au uamuzi mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Tunapozungumzia mafanikio ni pana sana. Kwa mujibu wa Makala hii, mafanikio ni ile hali ya kufikia viwango ulivyojiwekea kwenye maisha yako. Viwango hivyo vinaweza kuwa: Kuwa na elimu kubwa, kuwa na biashara kubwa, Kuwa na kazi nzuri, Kukuza kipaji chako na kadharika. Hivyo katika Makala hii nitajikita kuelezea ni uamuzi gani mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Sasa, nianze na tabia ambayo watu wengi ambao hawajafanikiwa wanayo. Tabia mojawapo ambayo watu ambao wameshindwa kufanikiwa wanayo ni tabia ya kurukaruka. Maana yake ni kuwa watu wengi wanafanya vitu ambavyo kwa asilimia 100 hawajaamua kufanya. Au kwa lugha nyingine ni kuwa, wanafanya vitu kwa kujaribu.

Kwenye maisha, kama hautaweka nguvu zako, akili zako na mawazo yako kwenye jambo unalotaka kufanya kwa asilimia mia moja, kamwe hautaweza kufanikiwa. Ndio maana watu wengi walioingia kwenye biashara walifeli, kwa sababu hawakuingia wazima wazima bali waliingia mguu mmoja ndani mwingine nje. Hivyo wakaweka nguvu kidogo hapo na pale kidogo. Hivyo wakashindwa kupata matokeo makubwa. Watu wa namna hiyo unakuta leo anafanya biashara hii, kesho anaona mwingine anafanya biashara nyingine na wao wanafuata. Hawawekezi nguvu zao sehemu moja.

Sasa ngoja nikusimulie habari hii itakupatia jambo la kujifunza.

Miaka mingi iliyopita kulikuwa na Kamanda mmoja wa kikosi cha Hispania cha Kijeshi aliyekuwa anaitwa Hernan Cortes. Mwaka 1519 alipewa kazi ya kwenda kuvamia kisiwa kimoja nchini Mexico kilichoitwa Berecluse na akapewa wanajeshi 500 na meli 11. Walipofika pale Kisiwani akaagiza wanajeshi wote washuke pamoja na wale mabaharia. Waliposhuka akaagiza meli zote zichomwe moto. Walipochoma moto na moshi ulipoanza kupanda juu, akawaita wale wanajeshi na wale mabaharia akawauliza, mnaona nini? Wakasema tunaona meli zetu zinaungua. Akasema, safi sana. Akawaambia, tuna chaguzi mbili tu zilizobaki hapa, tushinde vita au tushindwe vita tuangamie wote hapa. Hakuna njia mbadala tofauti na hizo.

Matokeo yake yalikuwaje?

Walikuwa wanajeshi wachache sana lakini vita walishinda. Kwa nini? Ni kwa sababu waliamua kwa asilimia mia moja kufanya kile kitu walichokuwa wanakifanya.

Jambo la kujifunza ni hili, ili uweze kufanikiwa kwenye jambo lolote, usiseme ninajaribu. Sema ninafanya. Chochote unachoamua kufanya, jitoe kwa nguvu zako zote na utaona matokeo makubwa. Kuanzia leo, usiseme najaribu jaribu, bali sema nafanya. Na ukiamua kufanya, CHOMA MELI ZAKO ZOTE na utashinda.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Mojawapo ya majuto ambayo watu wengi hupitia hasa umri wao unapokuwa umekwenda ni kuwa, hawakuishi maisha waliyokuwa wanayataka na kufanya kile kitu walichokuwa wanakipenda. Na pia hawakufikia malengo yao ya maisha kama walivyokuwa wanatamani kufikia. Katika Makala hii tutaangalia jambo kubwa ambalo limewachelewesha wengi kufanikiwa kufikia malengo yao ambalo pia linaweza kukufanya ushindwe kufanikiwa kwenye malengo yako na jinsi ya kukabiliana nalo.

Tafiti nyingi sana zinaonesha watu wengi sana hasa wanapokaribia kufa hujilaumu maisha waliyoishi. Mwanasaikolojia mmoja anayeitwa Daniel Amend aligundua kanuni nzuri sana inayoitwa 18, 40, 60. Kanuni hii ilikuwa inasema hivi:

Mtu anapokuwa na umri wa miaka 18-39 huwa anajiuliza nikifanya jambo hili, kazi hii au biashara hii watu watanionaje? Watu wa kundi hili maisha yote yanaendeshwa na maoni ya watu na sio utashi wao.

Mtu huyu akifikisha umri wa miaka 40-59 huwa anaanza kusema, kwa sasa umri wangu umekwenda hivyo sitojali. Mimi nitafanya, mwenye kunisema na aniseme lakini mimi nitafanya ili kufanikiwa.

Mtu huyu anapofikisha umri wa miaka 60 na kuendelea anakuja kugundua kuwa, watu aliokuwa anawafikiria kuwa wanamuwazia yeye hawakuwa wanamfikiria kabisa na wala hawakuwa na mpango naye. Wao pia walikuwa wanahangaikia maisha yao.

Baada ya kuona kanuni hiyo utagundua kuwa ndivyo maisha yalivyo. Watu wengi wanaishi wakiogopa kufanya kitu ambacho kingebadilisha maisha yao wakifofia kuwa watu watawaonanje au kuwafikiriaje. Kumbe wale ambao wanawahofia na wao wana mambo yao na wala hawana muda wa kuwafirikia.

Jambo kuwa ambalo unapaswa kulizingatia ili uweze kufanikiwa ni kuwa, usiwe mtu wa kuishi ili kuwaridhisha watu. Ishi maisha yako. Kama una malengo ya maisha uliyojiwekea na unahisi kuwa ukiyafanya yatabadilisha maisha yako, fanya kwa nguvu zako na akili zako zote. Usihofu kuwa watakuonaje. Kumbuka kuwa hakuna aliye na muda wa kujali au kuangalia maisha yako. Ukiwaangalia na kuwahofia watu, unajichelewesha mwenyewe.

Mfano, watu wengi wanaishi kwenye nyumba zenye gharama kubwa kupita uwezo au kipato chao, wamechukua mikopo wakanunua magari ili kuwaridhisha watu, wananunua nguo za gharama kubwa kuliko uwezo wao. Hii ni kwa sababu walitaka kuwaridhisha watu na hivyo wakajikuta wapo kwenye msongo mkubwa wa madeni katika maisha yao.

Kitu cha msingi katika maisha yako ni kuishi maisha yako na kufanya kitu unachokipenda ambacho unaona kitaleta mapinduzi kwenye maisha yako bila kuangalia watu watasemaje. Nimatumaini yangu umepata maarifa ya msingi sana ambayo yatakusaidia kufanikiwa kufikia malengo yako. Kama una maoni yoyote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kama utahitaji ushauri zaidi kwa simu na. 0752 081669. Asante na karibu katika Malala ijayo.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Karibu mpendwa msomaji katika Makala hii ya leo. Katika Makala hii nitaelezea jambo moja kubwa unalopaswa kulizingatia na kulifanyia kazi ili uweze kufanikiwa katika maisha. Inawezekana umekuwa ukitumia juhudi kubwa katika kazi zako ili uweze kujikwamua kimaisha lakini matokeo yanakuwa hayaonekani. Nikuhakikishie kuwa ukifuatilia Makala hii mwanzo hadi mwisho utakuwa umepata kitu cha msingi sana ambacho kitakusaidia uweze kufanikiwa katika maisha yako. Karibu tuendelee.

Je ulishawahi kujiuliza ni kitu gani kinawatofautisha watu waliofanikiwa sana na wale ambao hawajafanikiwa? Katika Makala hii ya leo ningependa nikushirikishe kitu kimojawapo ambacho kinaweza kukusaidia sana kwenye maisha yako. Kitu hicho ni uwezo wa kupanga malengo na kuyafuatilia.

Watu  wengi wanaamka kwenda kazini lakini ukiwauliza baada ya miaka kumi watakuwa akina nani hawawezi kukujibu. Sasa hebu nikushirikishe utafiti uliowahi kufanywa na Chuo Kikuu cha Havard cha nchini Marekani.

Chuo kikuu cha Havard mwaka 1979 kwenye kitengo cha biashara walifanya utafiti. Walikusanya wanafunzi 100 ili waweze kuwafanyia utafiti. Utafiti huo ulikuwa ni wa kuwauliza maswali. Waliwauliza kuwa,  wakimaliza shule baada ya miaka kumi watakuwa ni wapi ki-maisha au watakuwa na mafanikio gani? Wanafunzi hao walitoa majibu kama ifuatavyo:

Asilimia 84 ya wanafunzi walikuwa hawajui watakuwa wapi, hivyo hawakuwa na mpango wowote katika maisha yao. Walikuwa wakisoma lakini walikuwa hawajui maisha yao yatakuwaje.

Asilimia 13 ya wanafunzi  walikuwa wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote wa jinsi ya kupata kile kitu walichokuwa wanahitaji kwenye maisha yao.

Asilimia 3 ya wanafunzi walisema wanajua wanachokitaka na walikuwa wametengeneza mpango kamili wa jinsi ya kufanikiwa kupata kile walichokuwa wamekusudia kukipata.

Utafiti huo uliendelea baada ya miaka kumi .Baada ya miaka 10 Chuo cha Havard kiliwafuatilia wanafunzi hao ili kiweze kupata matokeo ya utafiti wao. Matokeo yaliyopatikana yalikuwa ni ya kushangaza.

Katika matokeo hayo:

Wale wanafunzi asilimia 13 ambao walisema wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote walikuwa wamefanikiwa  mara mbili zaidi ya wale asilimia 84 waliosema hawajui wanataka nini katika maisha yao.

Wale wanafunzi asilimia 3 ambao walisema wanajua wanachokitaka na wametengeneza mpago kamili wa jinsi ya kufanikiwa walikuwa wamefanikiwa mara 10 zaidi ya wale wanafunzi wengine wote.

Utafiti huu ukahitimisha kuwa, unapokuwa na malengo yako na ukayaishi, una uwezo wa kufanikiwa mara 10 zaidi ya wale ambao hawana malengo.

Kuanzia leo usiwe mtu asiyekuwa na malengo. Tumia muda kutafakari na kujiuliza miaka 10 ijayo utakuwa wapi?

Utakuwa na kiwango gani cha elimu.

Utakuwa na cheo gani.

Utakuza biashara yako kwa kiwango gani na kadhalika.

Hivyo, uwezo wa kupanga malengo na kuyaishi ni muhimu sana katika maisha yako. Usiishi kama mtu asiyekuwa na mwelekeo. Weka malengo na upange namna ya kuyafikia. Unapoamka asubuhi hakikisha unapitia malengo yako uliyojiwekea ili usiweze kupoteza muda wako kwa mambo ambayo yako nje ya malengo yako.

Chukua muda kutafakari na kupanga malengo yako unataka kuwa nani na wapi katika maisha. Unaweza kunishirikisha kwa kukomenti hapo chini. Asante sana na karibu katika Makala ijayo.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp