Vitabu 3 Bora vya Maendeleo Binafsi (Self Development Books).

Katika maisha, ili uweze kufanikiwa, unapaswa kuwa msomaji mzuri wa vitabu. Vitabu vinabadilisha mtizamo wa maisha na kutufanya tuwaze kwa namna tofauti. Hivyo, kama nia yako ni kuwa mtu mwenye mafanikio, unapaswa kusoma vitabu vya maendeleo binafsi (self development). Katika makala hii nitakushirikisha vitabu vitatu bora vya maendeleo binafsi ambavyo vimekuwa na athari kubwa sana kwangu. Vitabu hivi vinaweza kubadili maisha yako na kukupeleka kwenye mafanikio makubwa.

1.Fikiri na Utajirike (Think and Grow Rich) – Napoleon Hill

Kitabu cha kwanza ni “Think and Grow Rich” kilichoandikwa na Napoleon Hill. Napoleon Hill alikuwa mwandishi na mwanahabari, na alipata fursa ya kukutana na Andrew Carnegie, mmoja wa matajiri wakubwa na wenye mafanikio makubwa wa wakati huo. Carnegie alimwomba Hill amsaidie kuunda falsafa ya mafanikio. Aliahidi kumfungulia milango ya kukutana na matajiri 500 wakubwa zaidi Marekani ili aweze kuwahoji na kukusanya taarifa muhimu kwa ajili ya kuandika vitabu vya kusaidia vijana wengine kufanikiwa kwa haraka zaidi.

Carnegie alimwambia Hill kuwa hatamlipa hata senti moja, lakini atamfungulia milango yote ili apate taarifa hizo. Hill, aliyedhani kuwa angeajiriwa na kulipwa fedha nyingi, alishangaa sana lakini alikubali changamoto hiyo ndani ya sekunde 46. Carnegie alimwambia kuwa alikuwa na sekunde 60 kutoa jibu, na Hill alitoa jibu lake ndani ya sekunde 46, jambo ambalo lilimvutia sana Carnegie.

Kwa miaka mingi, Hill aliwahoji watu matajiri na kugundua kanuni 17 ambazo walizifuata na ambazo zinaweza kujifunzwa na mtu yeyote. Alianza kwa kuandika seti ya vitabu 22 juu ya mafanikio ambavyo havikununuliwa, kisha akaandika kitabu cha kurasa 1000 ambacho pia hakikunuliwa. Hata hivyo, mwaka 1936, baada ya mdororo wa uchumi, alitoa kitabu kidogo cha kurasa 250 kinachoitwa “Think and Grow Rich” ambacho kilipata mafanikio makubwa na kikawa kitabu bora zaidi cha mafanikio duniani. Nimesoma kitabu hiki mara kadhaa na kimekuwa na athari chanya kubwa sana kwangu.

2.Mafanikio ya Juu Kabisa (Maximum Achievement) – Brian Tracy

Kitabu cha pili ni “Maximum Achievement” kilichoandikwa na Brian Tracy. Kitabu hiki kimeandikwa kwa ajili ya karne ya 21 na kinakuonyesha jinsi ya kubadili kabisa jinsi unavyofikiri, jinsi ya kuweka malengo katika kila eneo la maisha yako, na jinsi ya kuchukua udhibiti wa maisha yako na hivyo kuondoa hisia hasi zinazokuzuia kufanikiwa.

Kitabu hiki kinakuonyesha jinsi ya kujenga mahusiano mazuri na watu muhimu katika maisha yako, jinsi ya kukuza viwango vya juu vya kujiheshimu na kujiamini, na mambo mengine mengi. Mwandishi ameandika kitabu hicho kutokana na uzoefu wake wa kusoma vitabu na makala nyingi, kuweka pamoja maarifa hayo katika semina na kuwafundisha zaidi ya watu milioni moja katika nchi 58 kuhusu kanuni hizi, na kisha kuandika kitabu hiki.

“Maximum Achievement” na “Think and Grow Rich” ni kama mkono wa kulia na wa kushoto wa mafanikio.

3.Nguvu ya Kufikiria Chanya (The Power of Positive Thinking) – Norman Vincent Peale

Kitabu kingine ninachopendekeza ni “The Power of Positive Thinking” kilichoandikwa na Norman Vincent Peale. Peale alikuwa mhubiri na alitoa mawazo ya kuvutia sana kuhusu jinsi kufikiria kwa njia chanya kunavyoongeza nishati na shukrani maishani, na jinsi kunavyovutia watu na hali ambazo ziko sambamba na mawazo yako makuu.

Mawazo ya Peale yamebadilisha kizazi kizima. Ni kwa sababu vitabu hivi na vingine kama hivyo vimebadilisha mawazo ya watu wengi, na wale waliovisoma miaka ya 50, 60, na 70 wamekuwa viongozi na matajiri wakubwa.
Kama unataka kufanikiwa kama wao, namba moja, soma “Think and Grow Rich.” Namba mbili, soma “Maximum Achievement.” Namba tatu, soma “The Power of Positive Thinking.” Vitabu hivi vitabadilisha maisha yako. Kama ukisoma vitabu vyote vitatu, utashuhudia tofauti kubwa katika maisha yako.

Asante sana kwa kufuatilia makala hii. Kama una swali au maoni yoyote, usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu katika makala zinazofuata.

Kanuni 9 Za Kutengeneza Utajiri : Kitabu The Millionaire Next Door.

Kanuni 9 Za Kutengeneza Utajiri : Kitabu The Millionaire Next Door.

Kuna dhana iliyojengeka miongoni mwa watu wengi kuwa mamilionea wanaishi maisha ya anasa. Wanasafiri kwa ndege binafsi, wanaendesha magari ya kifahari, wanavaa nguo za mitindo mipya kila wakati na pia wanaishi katika nyumba za gharama kubwa. Ukweli ni tofauti kabisa. Thomas J. Stanley na William D. Danko wanadai kugundua siri kubwa zaidi ya mamilionea halisi wa Marekani. Katika kitabu chao cha ‘The Millionaire Next Door’, wanafichua ugunduzi wao kuhusu mtindo rahisi wa maisha ya mamilionea wa Marekani. Mtindo ambao hata wewe ukiweza kuishi utaweza kutengeneza utajiri.

Kitabu cha ‘The Millionaire Next Door’ kina msingi mmoja mkuu: hata wewe pia unaweza kuwa na mafanikio ya kifedha ikiwa utaepuka kutumia zaidi ya unavyopata, kujitoa kikamilifu katika kuwekeza, na kupanga mipango ya fedha zako vizuri.

Kuhusu Thomas J. Stanley na William D. Danko.

Thomas J. Stanley (1944-2015) alikuwa ni Mmarekani mwandishi na mfanyabiashara. Aliandika na kushiriki kuandika vitabu kadhaa kuhusu tabaka tajiri la Marekani. Orodha hiyo inajumuisha kitabu kilichouza sana cha The Millionaire Next Door, ambacho alikiandika kwa kushirikiana na William D. Danko.

Stanley alipata shahada ya uzamivu katika utawala wa biashara kutoka Chuo Kikuu cha Georgia. Baada ya kuhitimu, alihudumu katika nafasi mbalimbali za uongozi katika makampuni mbalimbali. Pia alikuwa mshauri mkuu katika Kampuni ya Datapoint iliyoanzishwa mwaka 1968. Datapoint ilikuwa kampuni ya teknolojia iliyokuwa ikitengeneza terminali za kompyuta. Baadaye katika kazi yake, alitoa mihadhara ya masoko katika vyuo vikuu vya Tennessee na Georgia.

Dkt. William D. Danko ni mwanachama wa kitivo katika Chuo Kikuu cha Jimbo la New York (State University of New York). Katika miongo mitatu iliyopita, amesoma tabia ya watumiaji na jinsi ya kutengeneza utajiri kwa kina (consumer behavior and wealth formation). Mbali na The Millionaire Next Door, pia ameshiriki kuandika kitabu cha Richer Than a Millionaire: A Pway to True Prosperity. Dkt. Danko ni mtafiti aliyechapishwa nchini Marekani, Australia, Canada, Ujerumani, Poland, na Uswisi. Alimaliza Ph.D. yake katika chuo cha Rensselaer Polytechnic Institute’s (RPI) Lally School of Management.

Stanley na Danko walitumia miaka 20 kusoma jinsi Wamarekani waliofanikiwa walivyopata utajiri na jinsi wanavyotumia pesa zao. Walishirikisha takriban watu 1,000, ambao walijibu maswali 200 kila mmoja. Waandishi wengi hutumia muda mwingi kusoma na kuandika jinsi ya kupata utajiri. Lakini Stanley na Danko walilenga kuelewa jinsi matajiri wanavyoishi maisha yao tofauti na Wamarekani wa kawaida. Stanley alifariki katika ajali ya gari mwaka 2015.

Karibu sasa tuangalie kanuni za kutengeneza utajiri kutoka kwenye kitabu hiki cha The Millionaire Next Door.

Kanuni 9 Za Kutengeneza Utajiri : Kitabu Cha The Millionaire Next Door.

1: Mamilionea Hawatumii Kiasi Kikubwa cha Pesa Wanachopata.
Kama milionea, unaweza kuwa umewaza kuendesha gari la kisasa na kunywa mvinyo wa bei kubwa. Lakini kwa uhalisia, mamilionea wengi ni waangalifu katika matumizi.

“Watu wengi wanaoishi katika nyumba za gharama kubwa na kuendesha magari ya anasa, kiuhalisia hawana utajiri mkubwa. Tuligundua kitu cha ajabu zaidi kwenye utafiti wetu: Watu wengi wenye utajiri mkubwa hawaishi hata katika maeneo ya kifahari.” – Thomas J. Stanley

Hii sio dhana ambayo utaisikia kwenye vyombo vya habari kuhusu mamilionea. Badala yake, vyombo vya habari vinaonyesha maudhui yanayosifu matumizi makubwa ya pesa na maisha ya kifahari.

“Sekta ya matangazo na Hollywood wamefanya kazi nzuri ya kutufanya tuamini kwamba utajiri na matumizi makubwa ya pesa vinakwenda sambamba.” – Thomas J. Stanley

Lakini, ikiiwa unataka kufikia mafanikio ya kifedha na kutengeneza utajiri, usifuatilie maisha yasiyokuwa na uhalisia kutoka kwenye vyombo vya habari. Lazima upange matumizi yako na ujifunze jinsi ya kuokoa pesa unapoanza kupata pesa zaidi ya zile unazozihitaji.

“Kwa kipato chochote ulichonacho, ishi chini ya kipato chako. Mamilionea mara nyingi hutengeneza utajiri kwa kutotumia mali nyingi kwenye makazi yao ya kwanza, hivyo kuwafanya wawe na uwezekano mdogo wa kuishi katika maeneo tajiri” – Thomas J. Stanley

Ili uweze kuwa millions siyo lazima uwe msomi au mtaalamu wa teknolojia. Mara nyingi mamilionea ni watu wanaoishi maisha ya kawaida kabisa jirani yako. Wanatumia kila dola kununua bidhaa zinazoongeza thamani katika maisha yao. Mamilionea pia sio lazima wamiliki magari ghali zaidi. Badala yake, wanaweza hata kumiliki magari ya kawaida ya mkono wa pili (second hand).

Jinsi Mamilionea Wanavyoishi Maisha Yao Kwa Uangalifu.
Bajeti madhubuti na kuishi maisha ya uangalifu ni muhimu sana katika kujenga utajiri wako. Kupata mshahara mkubwa haimaanishi kuwa wakati wewe ni tajiri. Hata kama wewe ni miongoni mwa wafanyakazi wanaolipwa vizuri zaidi, kodi itachukua sehemu kubwa ya kipato chako. Baada ya kupunguza gharama za maisha, utakuwa umebakiwa na pesa kidogo za kujikimu hadi mshahara ujao.

Lakini huna haja ya kupata mamilioni ili kuokoa pesa na kuweka akiba kwa ajili ya siku zijazo. Kanuni rahisi ya utajiri ni kuokoa kiasi kikubwa cha pesa iwezekanavyo unapokuwa umepata pesa zaidi kuliko unazohitaji kuishi.

“Jambo la msingi kabisa la Kutengeneza utajiri ni kuweka ulinzi, na ulinzi huu unapaswa kuwa umejikita kwenye bajeti na mipango.” – Thomas J. Stanley

Mkakati muhimu ambao mamilionea hutumia kwa uangalifu ni kuendeleza mazingira ya kuishi maisha ya kawaida. Ingawa wanaweza kumudu chakula cha dola 200, wanachagua mlo wa dola 50. Badala ya kutumia gari la gharama kubwa, huchagua usafiri wa gharama ndogo ili kuokoa pesa.

2: Mamilionea Wanatenga Muda na Nguvu Katika Kutengeneza Utajiri
Subira, shauku, na uvumilivu ni thamani muhimu miongoni mwa watu waliojilimbikizia utajiri. Stanley na Danko waligundua kwamba mamilionea huwa wanawekeza muda na nguvu katika kupanga mustakabali wao wa kifedha. Wanazingatia kujenga uchumi wao wa kifedha kuliko vitu vingine maishani. Mara nyingi kutengeneza utajiri huchukua miaka, ikiwa sio miongo.

“Kipato ni kile unachobeba kupeleka nyumbani leo. Utajiri ni kile unachokuwa nacho kesho, kesho kutwa na siku inayofuata” – Thomas J. Stanley

Kinyume na imani inayoenezwa na vyombo vya habari, kujenga utajiri sio tukio la haraka au la mara moja. Badala yake, ni la polepole, la mfumo na linalochukua muda kukomaa.

Kuwa na kipato cha juu sio sababu ya moja kwa moja ya kutengeneza utajiri kwa haraka. Wapokeaji wa kipato cha juu mara nyingi wanagawanywa katika makundi mawili ambayo ni Walimbikizaji wa utajiri (Prodigious Accumulators of Wealth (PAW)) na walimbikizaji duni wa utajiri (Under Accumulators of Wealth (UAW))

Walimbikizaji wa Utajiri (PAWs) ni mabingwa wa kuokoa pesa na kukuza utajiri. Wana thamani ya utajiri mara nne zaidi ya watu wengi wenye kipato kama chao. Wanazingatia katika kufikia uhuru wa kifedha.
Walimbikizaji Duni wa Utajiri (UAWs) wanafanya chini ya wastani katika kuokoa pesa. Hivyo, wako nyuma sana ya PAWs licha ya kuwa na kipato kama chao.

Bahati mbaya, UAWs wengi ni wataalamu wenye elimu ya juu wanaopata kipato cha juu. Hata hivyo, wanatumia pesa zao kudumisha maisha ya anasa. Pia wanajaribu kudumisha viwango vya maisha ya juu ili kujionyesha kwa jamii inayowazunguka.

“Ni vipi watu wenye elimu nzuri, wenye kipato cha juu wanaweza kuwa wajinga kiasi hicho kuhusu pesa? Kwa sababu kuwa na elimu nzuri, kupata kipato cha juu haimaanishi moja kwa moja kuwa na uhuru wa kifedha. Kutengeneza utajiri na kuwa na uhuru wa kifedha Inahitaji kupanga na kujinyima.” – Thomas J. Stanley

3: Mamilionea Wanapima Uhuru wa Kifedha Kuliko Hali ya Kijamii ya Anasa.
Tunaishi katika ulimwengu wa mitandao ya kijamii ambapo watu mara nyingi wana hamu ya kuonyesha maisha ya kifahari kwa ajili ya umaarufu. Ikiwa jambo hili ni udhaifu ulio nao, hauko peke yako. Kwa bahati mbaya, kuzuia hamu hii inaweza kuwa ngumu. Ili kuonekana tajiri katika ulimwengu wa nje, vijana wengi hujitahidi kutumia pesa nyingi kuliko uwezo wao ili kujionyesha mitandaoni.

Ni mikopo ndiyo inayoendesha maisha ya anasa ya wafu wengi leo, sio mapato halisi. Watu wanataka kuwa na nguo za wabunifu maarufu na kukodisha magari ya starehe. Hata hivyo, nguvu zao za kifedha haziruhusu hilo. Kwa kufuata maisha haya ya anasa, huwezi kuwa na amani inayotokana na uhuru wa kifedha. Badala yake, kwa ndani kabisa, mbali na macho ya umma, utakuwa unajua kuwa haujafanikiwa kifedha.

“Kuna uhusiano wa kinyume kati ya muda uliotumika kununua vitu vya anasa kama magari na nguo na muda uliotumika kupanga mustakabali wa kifedha wa mtu.” – Thomas J. Stanley

Mamilionea bora wa Marekani hawahisi kuwa na shinikizo la kuthibitisha kwamba wanaishi maisha ya anasa kwa ulimwengu. Badala yake, wanapendelea kupata uhuru wa kifedha kuliko kuonekana matajiri. Wanaona uendelevu wa kifedha kama tuzo kuu ya kukua na kutengeneza utajiri.

“Ili kujenga na kudumisha utajiri, itakuwa muhimu kwako kushughulikia usimamizi wote wa kifedha – matumizi, kuweka akiba, kuzalisha mapato, kuwekeza – kwa njia tofauti, kwa nidhamu zaidi kuliko mtu yeyote mwingine anayekuzunguka” – Thomas J. Stanley

Kitabu cha The Millionaire Next Door kinaonyesha kwamba uhuru wa kifedha unachangia ustawi. Mamilionea wana furaha na kujiamini zaidi katika uendelevu wao wa kifedha wa sasa na wa baadaye. Wana malengo na madhumuni wazi ya muda mfupi na mrefu, yakiwaruhusu kupanga na kubajeti mahitaji yao kulingana na vipaumbele.

Kila mtu anathamini ustawi wa familia zao kuliko vitu vingine. Zingatia uhuru wa kifedha na epuka dhana ya mitandao ya kijamii ya “tajiri.” Kwa njia hii, unaweza kufurahia uhuru wa kifedha na familia yako kama milionea bora.

4: Mamilionea Hawaendekezi Maisha Ya Kujionyesha.
Vijana wa kiume na wa kike wenye wazazi matajiri mara nyingi hufanya sherehe za anasa na kuonyesha maisha yao ya gharama kubwa. Hata hivyo, hilo sio zuri kwa mustakabali wa kifedha wa vijana wenyewe. Kwa kweli, hilo linaweza kuwa janga la kifedha linaloandaliwa.

Wazazi wengi matajiri hutumia pesa nyingi kwa watoto wao kupitia zawadi za pesa taslimu na kufadhili safari zisizo za biashara.

Kuishi maisha ya uangalifu katika maisha yako kunafundisha watoto wako kufuata mtindo huo wa maisha. Kuwa na matumizi makubwa kunahimiza watoto wako kukumbatia maisha ya anasa badala ya kutengeneza utajiri.
Kufundisha watoto wako umuhimu wa uangalifu katika matumizi ya fedha ni ufunguo wa utajiri. Inawasaidia kuendeleza mipango ya kufikia uhuru wa kifedha.

5: Mamilionea Wanalea Watoto Wenye Majukumu ya Kiuchumi.
Hakuna mtu anayetaka kuacha urithi mbaya anapofariki. Kila mtu anataka urithi wake udumishwe kwa miongo na vizazi vyake viongeze utajiri. Lakini je, hili linatokea kila wakati?

Watoto wanaotegemea wazazi watarithi utajiri zaidi kutoka kwa wazazi wao. Lakini mara nyingi wanakosa maarifa ya kuwekeza na kujilimbikizia utajiri. Hii inawapelekea kutumia vibaya utajiri kupitia maisha ya kifahari. Hata hivyo, mahojiano ya Stanley yanaonyesha jinsi mamilionea bora wanavyochukulia malezi ya watoto wanaojitegemea. Hapa kuna baadhi ya masomo ya kujifunza kutoka kwao:

  1. Usiwaambie wako kwamba wewe ni tajiri.
    Watoto wenye wazazi wa UAW huiga tabia za matumizi ya wazazi wao. Pia wana hamu ya maisha ya anasa. Lakini watoto wa wazazi wa PAW hukua bila kujua thamani ya utajiri wa wazazi wao. Hii inawasaidia kujifunza kuwa kujitegemea na kuwajibika kwa tabia zao za matumizi ya fedha.
  2. Wafundishe watoto wako kuwa waangalifu kwenye matumizi ya pesa.
    Bila kujali umekusanya utajiri kiasi gani, fanya uangalifu. Wafundishe watoto wako vivyo hivyo ili waweze kuishi maisha rahisi.
    Watoto wako hawapaswi kutambua kuwa wewe ni tajiri hadi watakapokuwa watu wazima wenye majukumu na nidhamu. Wakati wanatambua utajiri wako, wanapaswa kuwa wamekomaa vya kutosha kuchukua majukumu na kufanya maamuzi chanya ya kuongeza utajiri.
  3. Elekeza watoto wako kuelekea mafanikio.
    Mamilionea wengi wanasisitiza haja ya kuwafundisha watoto wao jinsi ya kutengeneza utajiri. Kuwafundisha watoto kwamba kupata kipato kunawezesha matumizi zaidi kutaangamiza maisha yao ya kiuchumi. Bahati mbaya, hivyo ndivyo wazazi wengi wa UAW wanavyofanya. Matokeo yake, watoto wao wanapopata ongezeko la mshahara, wanazingatia kuongeza matumizi. Badala yake, wanapaswa kujifunza kuokoa au kuwekeza pesa wasizozihitaji.

6: Mamilionea Wanatumia Fursa za Soko.
Mamilionea wanafanyaje maamuzi ya nini cha kutumia? Wapangaji wa kimkakati wanafahamu siri za pesa. Wanawekeza katika huduma za afya za familia zao na biashara zinazoongeza uzalishaji.

Mamilionea wanafanya uangalifu kwa kuepuka bidhaa na huduma zisizo za lazima. Hata hivyo, hawana uoga wa kuchukua hatari zilizohesabiwa kwa fursa za biashara zenye thamani.

“Moja ya sababu ambazo mamilionea wanafanikiwa kiuchumi ni kwamba wanafikiri tofauti.” – Thomas J. Stanley

Ili kufuata nyayo za mamilionea, jifunze kupanga uwekezaji wako kwa uangalifu. Fursa zenye hatari kubwa zinaweza kuwa na malipo makubwa ikiwa zitachunguzwa na kutekelezwa kwa uangalifu.

7: Mamilionea Huchagua Kazi kwa Hekima.
Una mpango gani wa kutengeneza utajiri? Je, unataka kufikia kilele cha kazi yako au kuanzisha biashara yako mwenyewe kutoka mwanzo?

Kitu cha kushangaza ni kuwa, mamilionea wengi nchini Marekani ni wamiliki wa biashara binafsi. Unaweza kupata mshahara mkubwa kutoka kwenye ajira yako. Hata hivyo, utajikuta unatumia sehemu kubwa ya mshahara wako kulipia bili zako na kudumisha maisha yako ya gharama kubwa.

Kinyume chake, wamiliki wa biashara hupokea kipato kutoka vyanzo tofautitofauti. Njia hizi zinawawezesha kuzidisha uwekezaji wao huku wakiendeleza maisha rahisi.

“Utajiri ni kile unachojilimbikizia, sio kile unachotumia” – Thomas J. Stanley

Kuanzisha biashara sio dhamana ya kuwa milionea. Biashara nyingi hazitimizi malengo ya wamiliki. Kushindwa kwa biashara nyingi kunaweza kuwa ni kutokana na ushindani au mipango mibovu.

Mamilionea wanazingatia kuchagua kazi za kuwekeza. Wawekezaji wengi wa kawaida hudhani kazi maarufu ndizo zenye mafanikio zaidi. Hata hivyo, mamilionea wana maoni tofauti. Hapa kuna baadhi ya mawazo kuhusu kuchagua kazi sahihi:

  1. Sekta Isiyovutia. Si ajabu kwamba mamilionea wengi wanawekeza katika biashara hizi zinazoonekana ‘zisizovutia’. Sekta zisizovutia ni thabiti zaidi lakini hazivutii watu wengi.
  2. Uangalifu katika Biashara. Unahitaji kufanya uangalifu katika maisha yako binafsi na katika biashara. Punguza matumizi katika idara zisizo na tija. Hii itakusaidia kuzidisha rasilimali katika maeneo yanayotoa faida zaidi.
  3. Maarifa Mapana ya Biashara. Usiwekeze katika biashara tu kwa sababu inaahidi kuwa na faida. Mamilionea wengi wana ujuzi katika maeneo ya biashara wanayowekeza. Ikiwa haujazoea sekta ya ukarimu, fikiria upya kabla ya kufungua mgahawa.

8: Mamilionea Wana Malengo na Madhumuni Wazi.
Kama vile binadamu walivyo na sifa za kipekee, vivyo hivyo katika kujenga utajiri. Umepanga kukusanya utajiri kiasi gani katika mwaka mmoja? Ni mikakati gani umeweka ili kuhakikisha unafikia lengo lako?

Mamilionea wengi ni wapangaji wakuu na wenye ufanisi katika kufafanua malengo yao. Wanatoa kipaumbele katika usimamizi wa fedha zao. Wengi wana ratiba za kila siku, kila wiki, na kila mwezi kufuatilia maendeleo yao.

Malengo yanatoa taarifa kuhusu mikakati na njia wanazochukua. Wanachanganua malengo ya muda mrefu katika majukumu madogo yanayoweza kusimamiwa. Hii inatoa njia wazi kuelekea lengo la mwisho.

Katika kitabu chake, No Excuses! Brian Tracy anadai kwamba asilimia tatu tu ya Wamarekani wazima wana malengo na madhumuni. Kundi hili linajilimbikizia utajiri mkubwa zaidi kuliko sehemu nyingine ya idadi ya watu.

Ikiwa uko tayari kufanya kile kinachohitajika kuwa milionea, anza kwa kuweka malengo na madhumuni. Changanua malengo yako kwa kuyagawa katika malengo madogomadogo na kuanzisha mipango kwa kila hatua itakayokupa mtazamo wazi wa malengo yako.

9: Mamilionea Wamepitia Nyakati Ngumu.
Wengi wetu tunazingatia tu hadithi za mafanikio ya mamilionea. Lakini hatuelewi historia ya mafanikio yao. Mamilionea wengi walivuka mipaka yao kufikia walichonacho. Je, umewahi kufikiria kufanya kazi mbili bila likizo? Haya ni baadhi ya mambo ambayo mamilionea wamevumilia katika safari yao.

Safari za kujenga utajiri mara chache huwa rahisi na zinahitaji maadili makali ya kazi. Mamilionea wengi waliojijenga wenyewe wamelazimika kukabiliana na vikwazo na vizuizi ili kufikia kiwango chao cha mafanikio. Pia wamelazimika kujinyima katika sasa yao ili wawe katika nafasi nzuri kwa siku zijazo.

Fikiria gari la michezo unalotaka kununua leo ambalo linagharimu $50,000. Hata kama una pesa taslimu za kununua, hiyo $50,000 je, huwezi kuwekeza katika masoko ili kupata faida kubwa zaidi? Mamilionea wangeona hiyo ni fursa inayostahili kuchangamkiwa ili kupata faida kubwa zaidi baadaye.

Kila hadithi inaleta mtazamo kwamba hakuna njia rahisi ya kujilimbikizia utajiri. Inahitaji kujitoa, uvumilivu, na nidhamu.

Muhtasari wa Mwisho na Mapitio ya Kitabu cha The Millionaire Next Door.
Kitabu cha Stanley na Danko, The Millionaire Next Door, kinawasilisha njia ya kweli ya kuwa milionea bora. Huna haja ya kuthibitisha wewe mwenyewe au utajiri wako kwa watu. Kutumia pesa zako kwa vito vya thamani, nguo za wabunifu, na magari hupunguza utajiri wako.

The Millionaire Next Door inaonyesha kwamba, kuwa milionea inamaanisha kuokoa mapato yako ya ziada. Zaidi ya hayo, kupata utajiri sio otomatiki unapokuwa na pesa zaidi kuliko unazohitaji. Badala yake, ni mchakato wa polepole ambao unaweza kuchukua miaka. Safari pia inaweza kujumuisha changamoto nyingi. Uvumilivu wako na utayari wa kufanya makosa na kuyarekebisha ni muhimu.

Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kukusaidia kutengeneza utajiri kutoka kwenye kitabu hiki cha The Millionaire Next Door. Kama una maoni basi usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami kwa simu namba 0752 081669. Asante sana na karibu katika makala zinazokuja.

Hatua 10 Za Kuwa Na Mafanikio Na Kuwa Tajiri

Hatua 10 Za Kuwa Na Mafanikio Na Kuwa Tajiri

Napoleon Hill alikuwa ni mwandishi wa vitabu vya mafanikio, raia wa Marekani. Vitabu vyake vililenga zaidi kwenye kanuni za mafanikio na kuwa tajiri katika maisha na kifedha. Alianza kazi yake kama mwandishi wa habari kabla ya kuwa mshauri wa rais wa Marekani wa kipindi kile aliyejulikana kwa jina la Franklin D. Roosevelt.
Ni wakati alipofanya mahojiano na Andrew Carnegie ndipo alipopata hamasa ya kuanza kazi yake ya kuhamasisha watu juu ya mafanikio. Alitumia maarifa aliyoyapata kwenye mahojiano hayo kuandika vitabu vya mafanikio katika biashara na kutengeneza kipato. Vitabu vyake vingi vimeendelea kuwa maarufu mpaka sasa kama vile vilivyokuwa kabla ya kifo chake mwaka 1970.

Hatua 10 Za Kuwa Na Mafanikio Na KuwaTajiri.
Kitabu Cha Think and Grow Rich kinaelezea nguvu iliyopo kwenye kuwa na fikra chanya kwenye maisha. Kitabu hiki kinaelezea umuhimu wa kuwa na fikra chanya za mafanikio. Watu waliofanikiwa toka zamani walikuwa na mawazo chanya kuwa watafanikiwa wakiwa na uvumilivu pamoja na elimu ya kile walichokuwa wanafanya. Pia walikuwa wamezingukwa na watu waliokuwa wana mawazo yanayoendana ya mafanikio kwenye kile walichokuwa wanafanya.
Kila mmoja anaweza kushindwa katika malengo aliyojiwekea ya maisha, lakini, kwa wale ambao wataendelea kujaribu bila kukata tamaa watafanikiwa.
Mambo ya msingi ya kujifunza kutoka kwenye kitabu cha Think and grow rich.

1: Mafanikio yanahitaji kuwa na malengo pamoja na mipango iliyoainishwa vizuri.
“Set your mind on a definite goal and observe how quickly the world stands aside to let you pass.” — Napoleon Hill.

Maana yake ni kuwa, jiwekee malengo, hapo ndipo utaona jinsi utakavyowapita wengine kimafanikio kwa haraka.

Jambo la muhimu kabisa katika mafanikio ni kujua nini hasa unachohitaji kufanikiwa. Bila kuwa na malengo yaliyo bayana, hatuwezi kuanza safari ya mafanikio. Hivyo, andika malengo yako kwa lugha rahisi iwezekanavyo. Kama unataka kuwa tajiri, unatakiwa ubainishe ni kiasi gani cha pesa unataka kumiliki utakapokuwa umefikisha umri fulani. Malengo yatakusaidia kufahamu ni kwa kiwango gani unapaswa kuwekeza ili uweze kufikia lengo kuu uliloliweka.

Baada ya kuwa umefahamu hitaji lako kuu na umejiwekea muda wa kuwa umelitimiza, jambo linalofuata ni kuweka mikakati ya hatua kwa hatua jinsi ya kutimiza lengo lako kuu. Baada ya kuwa umeweka hizo hatua, anza kufanyia kazi mara moja bila kukawia.
Kuweka malengo kutakupatia hamasa ya kufanya bidii kwenye kazi zako na hivyo kuweza kufanikiwa.

2: Kuwa na shauku ya kutimiza malengo yako. (Desire is the Starting Point of All Achievement)
Unaweza kupata chochote unachokitafuta katika maisha kama utakuwa na shauku (desire) ya kukipata.
Hii haimaanishi kuwa na shauku tu ya kupata kile unachokitamani. Kwa mfano unatamani kuwa na pesa na hivyo kwa kuwa na shauku tu pesa itashuka kwa muujiza, hapana. Badala yake ni kuwa, unapokuwa na shauku ya kufikia lengo kubwa katika maisha, utahamasika kuweka mipango madhubuti ya kufikia mafanikio.

Hatua zifuatazo zitakusaidia kuweka malengo yako ya kufanikiwa na kuwa tajiri (becoming wealthy):

i. Amua ni kiasi gani cha pesa unahitaji kukipata.

ii. Amua ni kitu gani utatoa au utawekeza ili uweze kupata kiasi cha pesa unachokihitaji.

iii. Weka tarehe ambayo umeamua kuwa utakuwa umepata kiasi hicho cha pesa.

iii. Weka mipango ya hatua kwa hatua ya jinsi utakavyofikia lengo lako. Pia angalia ni kitu gani utaanza kukifanyia kazi sasa bila kuchelewa.
Mambo yote hapo juu yaandike kwa sentensi fupi.
Jambo la mwisho, hakikisha kuwa unasoma sentensi hiyo mara mbili kwa siku.

3: Watu waliofanikiwa huwa wana imani na uwezo wao (successful People Have Faith in Their Abilities)
Imani isiyoyumba ndiyo rasilimali ya muhimu sana na ya ajabu sana kwenye mafanikio yako. Watu walio na imani watafanya kila kitu kwa nguvu, na kwa akili zao zote ili waweze kutimiza malengo yao. Hii ni kwa sababu, hautaweza kutimiza malengo yako kama haujiamini.

Mahatma Gandhi ni mfano mzuri sana wa nguvu ya imani na kujiamini. Gandhi hakuwa na nguvu yoyote ya kifedha au kijeshi. Badala yake alikuwa na imani isiyoyumba kuwa angeweza kuongoza taifa lake la India kupata uhuru. Imani Hii ilimuwezesha kuwashawishi wananchi wenzake kuanza kupigania uhuru wao.

Hata sisi, hatuna tofauti na Gandhi. Ikiwa tutakuwa na imani, ikiwa tutajiamini sisi wenyewe na uwezo tulionao, tutaweza kupata chochote tunachokihitaji.

4: Hauwezi kuwa na imani wakati huohuo ukiwa na hofu na mashaka.
Imani haiwezi kuwepo mahali palipo na hofu. Hivyo, wakati tutakapokuwa tumeshinda hofu zinazotukatisha tamaa, tutakuwa na imani isiyoyumba kutimiza malengo yetu na kupata utajiri.

Kuna aina sita za hofu:
i. Hofu ya umasikini ambayo husababisha kujiona kuwa haufai na kuwa na mashaka.

ii. Hofu ya kukosolewa. Hii ni hofu ambayo humfanya mtu asichukue hatua kwa kuogopa kuwa watu watamdharau na kumkosoa.

iii. Hofu inayosababishwa na hali ya kiafya. Kama mtu afya yake haiko sawa, anaweza kuogopa kuchukua hatua kutimiza malengo yake.

iv. Hofu ya kupoteza marafiki. Wakati mwingine unaweza kuogopa kuchukua hatua kwa kuogopa kupoteza marafiki.

v. Hofu inayotokana na uzee. Umri unavyozidi kwenda kuelekea kwenye uzee uwezo wa kufanya mambo huwa unapungua na kumfanya mtu awe na uoga wa kufanya mambo makubwa ambayo yatabadilisha maisha yake.

vi. Hofu ya kifo. Hofu ya kifo huwa inatufanya tuwaze zaidi kufa badala ya kuwaza ni kwa namna tunaweza kuishi tukiwa na maisha bora.
Mawazo yote ya hofu, hayawezi kukupatia mafanikio ya kifedha. Hivyo, tunapaswa kuepuka hofu ili tuweze kutimiza malengo yetu.

5: Pata elimu ya kitu unachotaka kufanya.
Elimu ni miongoni mwa vitu vya msingi sana katika kufikia malengo yako ya maisha. Kuwa na elimu haimaanishi kuwa na Diploma au Shahada.

Henry Ford ni mfano mzuri wa mtu ambaye hakubahatika kusoma lakini alikuwa na maarifa ya msingi ya kumsaidia kuweza kutimiza malengo yake.

Kuwa na mafanikio haihitaji kuwa na vitu vingi unavyovifahamu, badala yake, unahitajika kuwa kuwa na elimu na na uzoefu sahihi wa kile unachotaka kufanikiwa.

Ni rahisi kuridhika kuwa unafahamu vya kutosha kile unachokifanya katika maisha yako. Lakini, wale ambao wanaendelea kujifunza zaidi na kubobea kwenye ujuzi wa kazi wanazozifanya huwa wanafanikiwa sana. Hivyo, unaweza kujiendeleza zaidi kwa kusoma chuoni au kusoma kozi mtandaoni zinazoendana na kile unachokifanya ili uweze kukifanya kwa ufanisi na hivyo kufanikiwa kwenye maisha yako.

Pia, ili uweze kupata maarifa ya kutosha, mara zote unapaswa kujenga mahusiano na kuwa karibu na watu wenye uzoefu na elimu ya kile unachokifanya.

6: Kuwa na ndoto kubwa na uwe na hisia ya kuwa lazima utafanikiwa.
Kila mtu aliyefanikiwa, alianza kuwa na ndoto. Baada ya kuwa na ndoto, akajenga hisia kuwa lazima atafanikiwa. Hisia hizi zikanasa kwenye ubongo. Hivyo ili uweze kupata mafanikio, ni lazima uwe na ndoto pamoja na na hisia kali za kufanikiwa kwenye ndoto yako. Unapokuwa na hisia za mafanikio, hapo ndipo utapata njia na mipango ya kuwekeza kutimiza ndoto zako.

7: Tambua uwezo wako pamoja na mapungufu yako.
Kama unatambua udhaifu wako, utajipa changamoto ya kuzuia udhaifu wako usiweze kuzuia kutimiza malengo yako. Miongoni mwa mapungufu ambayo watu wengi wanayo ni pamoja na kukosa hamasa ya kufanya mambo (lack of ambition), kughairisha mambo (procrastination) na kuwa na malengo yasiyopimika (vague goals).

Ingawa unaweza kufahamu uwezo wako na udhaifu wako, unaweza kufahamu kwa ufasaha uwezo na mapungufu yako kwa kuandaa maswali ya kukuongoza kama ifuatavyo:

Je, nimetimiza malengo yangu ya mwaka?
Je, huwa ninakuwa na ushirikiano na wenzangu? Na kadhalika.

8: Kuwa na mtizamo chanya.
Unapokuwa ukifanya kazi kutimiza malengo yako, kuwa na mtizamo chanya kuwa utafanikiwa haijalishi utapitia changamoto kubwa kiasi gani. Jenga urafiki na mahusiano na watu walio na mtizamo chanya wa maendeleo kwani ukiwa umezungukwa na watu wenye mtizamo hasi, watakukatisha tamaa.

9: Watu waliofanikiwa ni wavumilivu kwenye changamoto.
Jizatiti kwenye malengo yako.

Watu huwa wanaferi katika malengo yao kutokana na kukosa uvumilivu. Katika malengo yako utapitia kushindwa lakini kumbuka kuwa mvumilivu. Kila unapopata changamoto, ichukulie kuwa ni sehemu ya kujifunza na kukufanya uwe bora zaidi. Watu waliofanikiwa huwa hawatoki nje ya malengo yao haijalishi wanapitia changamoto kubwa kiasi gani.

Jinsi ya kujenga uvumilivu na ustahimilivu kwenye malengo.
Ili uweze kuwa na uvumilivu pamoja na ustahimilivu kwenye kutimiza malengo yako, kanuni hizi zifuatazo zitakusaidia:

i. Andaa lengo katika maisha yako kutokana na kitu unachokipenda (Passion)

ii. Gawa lengo lako kwenye sehemu ndogondogo za utekelezaji na uweke mpango wa kutimiza lengo lako kwa kila sehemu ndogo uliyoiainisha.

iii. Usiruhusu mawazo hasi kuathiri utekelezaji wa malengo yako.
iv. Jenga mahusiano bora na watu wote ambao watakushika mkono katika nyakati ngumu.

10: Jiunge na kundi lenye shauku ya mafanikio ambalo mtabadilishana uzoefu (Mastermind group).
Kutengeneza kipato kunahitaji nguvu. Bila kuwa na nguvu hautaweza kuweka mipango yako katika utendaji. Kundi lako litaundwa na watu wenye shauku ya kufanikiwa na litakuwa na watu wenye ujuzi wa aina mbalimbali ambao mtabadilishana uzoefu na kupeana hamasa ya kuweza kufikia mafanikio. Tumia ujuzi ambao utakuwa unaupata kwenye kundi lako kutimiza malengo yako.

Kwa ufupi, kitabu cha Think And Grow Rich kinaelezea njia rahisi na zilizothibitishwa ambazo zitakusaidia kuwa tajiri. Kanuni hizi zimeelezwa kwa lugha rahisi na pia ni rahisi kuzifuata.

Kuwa na mtizamo chanya na kuweka mipango inayotekelezeka ni njia zitakazokusaidia kufikia malengo yako na kuwa tajiri. Pia unatakiwa kuambatana na watu sahihi ambao watakupa hamasa ya kufanyia kazi malengo yako.
Kanuni hizi ni za msingi, na hivyo jinsi utakavyozitumia itategemea na malengo yako. Hata hivyo, kitabu hiki kinatoa ushauri bora sana kwa mtu yeyote mwenye ndoto kubwa maishani ya kufanikiwa na kuwa tajiri.

Kama una maoni au swali lolote usisite kuandika hapa. Pia unaweza kuwasiliana nami kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu kwenye makala zijazo.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp