Jinsi Ya Kutengeneza Kipato Kinachokua Kila Siku

Kutengeneza Kipato endelevu Kinachokua Kila Siku

Mfumo wetu wa elimu huwa unatufundisha aina mbili za elimu: Aina ya kwanza ni elimu ya kujua kusoma, kuandika na kuhesabu (scholastic education). Hii ni elimu ambayo inakuwezesha kujua jinsi ya kusoma, kuandika na kuhesabu. Aina ya pili ya elimu ni elimu ya ujuzi (professional education). Aina hii ya elimu ndiyo inayozalisha wataalamu mbalimbali kama vile madaktari, walimu, wahandishi na kadhalika. Kuna aina ya tatu ya elimu ambayo haifundishwi darasani, nayo ni elimu ya msingi kuhusu fedha (financial education). Hii ni elimu inayokuwezesha kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato, jinsi ya kutumia pesa yako na jinsi ya kuwekeza pesa yako. Katika Makala ya leo nitakushirikisha aina hii ya tatu ya elimu na nitazungumzia jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku (Passive income).
Jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku.
Kwanza kabisa, ili uweze kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato ambacho kitakuwa kinakuwa kila siku na endelevu, ni lazima nianze kwanza kuelezea aina ya vipato. Watu wote wanaofanya kazi duniani na kupata kipato, vipato vyao vimegawanyika sehemu kuu tatu: aina hizi za vipato ni active income, portfolio income na passive income. Nitaelezea kila aina ya vipato.
Aina za vipato:
1. Active income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inakutaka wewe uwe mahali pa kazi, ufanye kazi ndio ulipwe. Hii inajumuisha watu walioajiriwa ambao wanalipwa baada ya kuwa wamefanya kazi. Maana yake ni kuwa, kama hakufanya kazi hawawezi kulipwa. Pia inajumuisha watu waliojiajiri ambao ni lazima waende kwenye maeneo yao ya kazi, wafanye kazi ndio waweze kupata kipato. Kwa lugha rahisi ni kuwa, active income ni aina ya kipato ambayo unalipwa tu pale unapokuwa umefanya kazi. Kama hukufanya kazi huwezi kulipwa.
2. Portfolio income
Hii ni aina ya kipato inayopatikana mtu anapoamua kuwekeza pesa yake kwenye maeneo ambayo itaongezeka thamani kama vile kuwekeza kwenye kununua hisa, kuwekeza kwenye mifuko ya pamoja na kuwekeza kwenye hatifungani. Kwa ligha rahisi ni kuwa, unawekeza pesa yako kwenye maeneo ambayo baadaye utapata faida.
3. Passive income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inapatikana bila ya ulazima wa wewe kuwepo mahali pa kazi. Biashara yako inakuwa inajiendesha yenyewe bila ya wewe kufanya kazi. Kwa mfano: unapokuwa umeamua kuandika kitabu na ukamaliza, basi kitabu hicho utakiuza maisha yako yote. Kazi kubwa utaifanya mwanzoni tu wakati wa kuandika. Lakini baada tu ya kumaliza kuandika kazi yako itakuwa ni kuuza tu. Hivyo kitabu chako kinakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato kikubwa na endelevu (passive income). Mfano mwingine ni unapokuwa umeandaa kozi yako na ukaiweka mtandaoni. Kazi yako kubwa itakuwa tu mwanzoni wakati wa kuandaa kozi yako lakini ukishamaliza, basi inakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato endelevu bila ya ulazima wa wewe kufanya kazi nyingine ya ziada. Lakini pia unaweza kuandaa video zako za mafunzo na ukaziweka YouTube. Baada ya kuwa umepata wafuasi wa kutosha na video zako zikawa na watazamaji wengi, basi unaweza kutengeneza kipato endelevu (passive income) kwani YouTube itakuwa inakulipa kupitia matangazo yake ambayo itayaweka kwenye video zako.
Kama njia yako ya kutengeneza kipato ni ile ya kwanza (active income) basi unaweza kuifanya lakini uwe na malengo ya kuandaa njia nyingine ambayo itakusaidia kupata kipato endelevu ambacho hakitakulazimu kufanya kazi (passive income). Hii ni kwa sababu, kadiri unavyoendelea kufanya kazi, nguvu zako zinaendelea kupungua hivyo ni muhimu kuwa na njia ya kutengeneza kipato ambayo hakitakulazimu kufanya kazi.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ya jinsi ya kutengeneza kipato kinachokua kila siku. Kama una maoni au swali, usisite kuweka maoni yako hapo chini. Pia kwa ushauri wowote usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu katika Makala zinazokuja.

Mambo 4 Ya Kufanya Unapoamka Asubuhi

Mambo 4 ya kufanya unapoamka asubuhi

Jinsi unavyoianza siku yako kila unapoamka asubuhi ina mchango mkubwa sana katika mafanikio yako. Watu wengi huwa wanakosea jinsi wanavyoanza siku asubuhi na hivyo kushindwa kupata mafanikio. Kisaikolojia, ukishindwa kuanza siku yako vizuri, utakuwa umeharibu siku nzima kwani utashindwa kupata matokeo makubwa uliyokuwa unayakusudia. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo manne muhimu unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi ili uweze kupata mafanikio makubwa katika maisha yako.
Mambo 4 muhimu ya kufanya kila unapoamka asubuhi.
1. Anza na Mungu.
Mungu ndiye muweza wa kila kitu. Ndiye anayetupa uhai, uwezo na nguvu za kufanya kazi zetu. Hivyo jambo la kwanza kabisa, uanpoamka asubuhi, anza na maombi. Muombe Mungu akusaidie katika kazi zako zote unazoenda kuzifanya. Hii itakusaidia kujenga mahusiano mazuri na Mungu na hivyo kukuwezesha kufanikiwa kwenye kazi zako. Pia unapoanza na Mungu, unapata utulivu wa akili kwa kuwa utakuwa umekabidhi mipango, na kazi zako zote kwake.
2. Angalia malengo yako ya muda mrefu.
Jambo la pili la kufanya kila unapoamka asubuhi ni kupitia malengo yako ya muda mrefu. Hapa utaangalia kama kazi unazoenda kuzifanya ndani ya siku ya leo zinatimiza malengo yako ya muda mrefu au la. Hii itakusaidia kutokuhama kwenye malengo yako uliyojiwekea ya muda mrefu. Kumbuka kuwa, ili uweze kufanikiwa ni lazima uwe na malengo makubwa uliyojiwekea. Kwa mfano , kwa mwaka huu umeweka malengo ya kuandika kitabu. Hivyo, unapoanza siku yako angalia kazi unazoenda kuzifanya zisikuhamishe kwenye lengo lako la muda mrefu.
3. Soma, angalia au sikiliza kitu kinachokutia nguvu na kukupa hamasa.
Kila unapoamka asubuhi, jambo la tatu unalopaswa kulifanya ni kusoma kitabu ambacho kitakupa hamasa (inspirational book). Lakini pia kama huna kitabu unaweza kuangalia video ambayo ina mada zinazohamasisha. Hii itakupa nguvu na hamasa kufanya kazi kwa bidi kutimiza malengo yako. Usianze siku yako kwa kuangalia udaku au kuangalia taarifa. Kumbuka kuwa unapoangalia taarifa, utapata taarifa nyingi ambazo nyingine ni za kusikitisha. Ukifanya hivyo utakuwa umeharibu hamasa ya kufanya kazi kwa siku nzima. Kumbuka kuwa jinsi unavyoianza siku yako asubuhi, ndio itaashiria jinsi siku nzima itakavyokuwa. Kama utaichosha akili yako kwa kusoma udaku asubuhi, utakuwa umeharibu utendaji wako wa siku nzima.
4.Hakikisha unaorodhesha vitu ambavyo utavifanya kwa siku nzima.
Baada ya kuwa umefanya mambo matatu kama nilivyoelezea hapo juu, jambo linalofuata ni kuorodhesha mambo yote ambayo utayafanya kwa siku nzima. Kuna faida kubwa sana kuorodhesha mambo unayoenda kuyafanya. Faida ya kwanza ni kutokupoteza muda kwani utakuwa unafahamu mambo unayopaswa kuyafanya, lipi linaanza na lipi linafuata. Faida ya pili ni kuhakikisha kuwa unafanya mambo yale tu ambayo umeyapanga yafanyike kwa siku hiyo hivyo kukusaidika kutimiza malengo yako ya muda mrefu uliyojiwekea.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi. Jambo la msingi ni kuchukua hatua. Kumbuka kuwa, mafanikio makubwa yanajengwa na vitu vidogo vidogo tunavyovifanya kila siku. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazokuja.

Mambo 3 Wanayofanya Watu Waliofanikiwa.

Mambo 3 muhimu wanayofanya watu Waliofanikiwa Duniani.

Katika kufanya utafiti na kusoma kwangu vitabu nilitamani kujifunza jinsi watu waliofanikiwa na matajiri duniani wanavyoishi. Lengo la kusoma kwangu vitabu lilikuwa ni kujua siri ya maisha yao na kufahamu vitu vya tofauti wanavyofanya na hivyo kuweza kujitofautisha na watu wa kawaida. Miongoni mwa watu ambao niliowahi kusoma vitabu vyao ni aliyekuwa Rais wa Marekani, Donard Trump pamoja na matajiri wengine wengi. Katika kusoma kwangu, niligundua kuna mambo matatu muhimu ambayo watu waliofanikiwa huwa wanafanya. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo matatu muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa Duniani ambayo hata wewe unaweza kuyafanya ili uweze kufanikiwa.
Mambo 3 muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa duniani.
1. Ni wasomaji wazuri sana wa vitabu.
Jambo la kwanza kabisa ambalo watu waliofanikiwa hufanya ni wasomaji wazuri sana wa vitabu. Ukifuatilia matajiri wote wakubwa wa dunia kama vile Donard Trump, hutumia muda wao mwingi katika kuongeza maarifa kupitia usomaji wa vitabu. Lengo kubwa la usomaji wao wa vitabu ni kuongeza ujuzi na maarifa kuhusiana na biashara pamoja na shughuli zao zingine wanazozifanya. Hivyo, hata wewe kama unataka kufanikiwa kwenye malengo yako, wekeza muda wako katika kujenga ujuzi wako kwenye shughuli unayofanya ili uweze kupata matokeo makubwa. Akili ya mwanadamu ni kama panga la kukatia ambalo linatakiwa kunolewa ili liweze kukata kwa urahisi. Tunanoa akili zetu kwa kujifunza maarifa mapya kila siku kupitia usomaji wa vitabu. Hivyo, kama unataka kufanikiwa, panga ratiba ya kusoma vitabu kila siku.
2. Hawaishi maisha ya kujionyesha ili kuridhisha watu.
Changamoto kubwa iliyopo kwa watu wengi ni kuishi maisha yasiyokuwa na uhalisia. Unakuta mtu anatamani kuishi maisha ya juu kuliko kipato chake. Anatamani awe na gari, awe na nguo za gharama kubwa, apange kwenye nyumba ya bei ya juu wakati kipato chake hakiwezi kuhimili gharama hizo. Wanaishi maisha yao ili kuwaridhisha watu. Matokeo yake ni kuingia kwenye madeni na kupata stress za maisha. Watu waliofankiwa hawafanyi hivyo. Wanaishi maisha yao kulingana na kipato chao. Hawaishi kuwaridhisha watu. Hivyo, ili uweze kufanikiwa, unapaswa kuwa na bajeti na matumizi yako yasizidi kipato chako. Ishi maisha yako na siyo kuishi ukishindana na watu.
3. Matumizi yao makubwa ya pesa yanaenda kwenye uwekezaji.
Watu waliofanikiwa wanapopata kipato chao hawaelekezi kipato chao chote kwenye matumizi ya kawaida. Asilimia kubwa ya kipato chao huwa wanakielekeza kwenye uwekezaji. Kila wanapopata kipato, asilimia Fulani wanawekeza kwenye biashara, kwenye kununua hisa, kwenye kununua hatifungani na kadhalika. Kabla ya kuanza kufanya matumizi ya kawaida, jambo la kwanza kabisa huwa wanatenga pesa kwa ajili ya uwekezaji. Hebu jiulize swali hili, kila unapopata pesa, ni asilimia ngapi unawekeza? Kama hauwekezi, na pesa yote unatumia kwa matumizi ya kawaida, basi hautaweza kufanikiwa. Haijalishi unapata kiasi gani cha pesa. Hata kama ni kidogo kiasi gani, kumbuka kutenga kwanza kiasi cha pesa ambacho utawekeza.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo wanayofanya watu waliofanikiwa ambayo hata wewe pia ukifanya utapata mafanikio makubwa. Kama una maoni au swali lolote usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana name kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazofuata.

Vikwazo 3 Vya Kushinda Ili Utimize Malengo Yako

Jinsi ya kutimiza MALENGO yako

Katika maisha kila mtu ana malengo au ndoto Fulani anayotamanai kuikamilisha ili aweze kufikia mafanikio. Hata wewe inawezekana una ndoto katika maisha yako unayotamani kuifikia. Inawezekana unatamani kufanya mambo makubwa kabla hujaondoka duniani. Lakini si wote wanaokuwa na malengo na ndoto katika maisha yao ambao wameweza kutimiza ndoto zao. Kuna sababu ambazo zinawafanya watu wengi washindwe kutimiza ndoto walizo nazo. Katika Makala ya leo nitakushirikisha vikwazo vitatu (3) ambavyo ni lazima uvishinde ili uweze kutimiza malengo yako.
Vikwazo 3 ambavyo ni lazima uvishinde kutimiza malengo yako.
1. Kutokuamini katika uwezo ulio nao.
Watu wengi sana wameshindwa kufikia kilele cha ndoto zao kwa sababu ya kutokuaminni katika uwezo walio nao. Hii inatokana na jinsi walivyoaminishwa toka wakiwa watoto, maneno ya walimu wao, maneno ya marafiki zao, mazingira waliyokulia na kadhalika. Wamekuwa wakisikia kwenye masikio yao maneno ya kukatisha tamaa kuwa hawawezi. Inawezekana hata wewe umekatishwa tamaa na wazazi, walimu, marafiki kuwa hauwezi. Ninataka nikuhakikishie kuwa una uwezo ndani yako wa kufanya makubwa na kutimiza malengo yako. Amini katika uwezo ulio nao na uchukue hatua. Amini kuwa una uwezo wa kuwa mtu mkubwa, amini kuwa unaweza kuwa bilionea na kadhalika. Usijidharau, una uwezo mkubwa sana uliojificha ndani yako ambao unachohitajika tu kufanya ni kuchukua hatua.
2. Kuamini kuwa kuna mtu yupo mahali fulani atakusaidia.
Katika maisha, hatma ya maisha yako unaipanga wewe mwenyewe. Hakuna mtu ambaye yupo kwa ajili ya kukusaidia katika maisha yako. Hata kama yupo, tambua kuwa sio wajibu wake kufanya hivyo. Hivyo ni lazima uchukue hatua wewe mwenyewe kwa asilimia mia moja kutimiza malengo yako. Kumbuka kuwa unapokuwa umeanza kuchukua hatua watu watakuja kukushika mkono wakiona tayari umekwisha anza. Kama malengo yako ni kuwa mwandishi, anza kuandika, kama ni kufanya biashara anza kwa kiasi chochote ulicho nacho. Hata kama hauna mtaji kabisa, tumia nguvu zako kuweza kupata mtaji wa kuweza kuanzisha biashara yako. Jambo la kuzingatia hapa ni wewe kuanza, haijalishi una hali gani. Unapokuwa umeanza, fursa zingine za kukufanya usonge mbele zitafunguka.
3. Kukata tamaa.
Kikwazo kingine ambacho kinaweza kukufanya ushindwe kutimiza malengo yako ni kukata tamaa. Watu wengi wameshindwa kutimiza malengo yao kwa sababu baada ya kuanza walipopata changamoto walikata tamaa na wakaamua kuacha malengo yao. Hata wewe inawezekana tayari umeamua kuchukua hatua, jambo la msingi ni kuendelea haijalishi utapitia changamoto kubwa kiasi gani, usikate tamaa. Endelea kupambana kwani mafanikio hayaji kwa urahisi, yanahitaji kujitoa kwa nguvu zako zote na akili yako yote. Hapa unatakiwa kupuuza maneno yote uliyoambiwa na ambayo unaweza kukutana nayo kuwa hauwezi. Maneno yoyote yale ambayo yatakuvunja moyo na kukukatisha tamaa yapuuze na upige hatua na mafanikio utayaona. Kama bado haujachukua hatua ni lazima utambue kuwa unapoanza kuchukua hatua kutimiza malengo yako kuna wakati utapitia nyakati ambazo zitakufanya ukate tamaa. Usikubali endelea kuchukua hatua mpaka pale utakapokuwa umetimiza kusudi la maisha yako.
Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yatakusaidia kuchukua hatua muhimu sana kwa ajili ya kutimiza malengo yako. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni au swali lako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazokuja.

Kila Aliyefanikiwa Alifanya Uamuzi Huu Mkubwa.

Kila Aliyefanikiwa Alifanya uamuzi huu Mkubwa

Katika maisha kila mmoja wetu anahitaji kufanikiwa. Lakini katika mafanikio kuna kanuni ambazo kila ambaye anahitaji kufanikiwa anapaswa kuzifahamu na kuzifanyia kazi. Na ndio maana katika maisha kuna watu waliofanikiwa na ambao hawajafanikiwa japokuwa wote wanawekeza juhudi kubwa kutafuta maisha. Hivyo kuna moja ambalo watu waliofanikiwa huwa wanalifanya na hivyo kuwatofautisha na watu wengine ambao hawafanikiwi. Katika Makala hii, tutaangalia jambo kubwa au uamuzi mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Tunapozungumzia mafanikio ni pana sana. Kwa mujibu wa Makala hii, mafanikio ni ile hali ya kufikia viwango ulivyojiwekea kwenye maisha yako. Viwango hivyo vinaweza kuwa: Kuwa na elimu kubwa, kuwa na biashara kubwa, Kuwa na kazi nzuri, Kukuza kipaji chako na kadharika. Hivyo katika Makala hii nitajikita kuelezea ni uamuzi gani mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Sasa, nianze na tabia ambayo watu wengi ambao hawajafanikiwa wanayo. Tabia mojawapo ambayo watu ambao wameshindwa kufanikiwa wanayo ni tabia ya kurukaruka. Maana yake ni kuwa watu wengi wanafanya vitu ambavyo kwa asilimia 100 hawajaamua kufanya. Au kwa lugha nyingine ni kuwa, wanafanya vitu kwa kujaribu.

Kwenye maisha, kama hautaweka nguvu zako, akili zako na mawazo yako kwenye jambo unalotaka kufanya kwa asilimia mia moja, kamwe hautaweza kufanikiwa. Ndio maana watu wengi walioingia kwenye biashara walifeli, kwa sababu hawakuingia wazima wazima bali waliingia mguu mmoja ndani mwingine nje. Hivyo wakaweka nguvu kidogo hapo na pale kidogo. Hivyo wakashindwa kupata matokeo makubwa. Watu wa namna hiyo unakuta leo anafanya biashara hii, kesho anaona mwingine anafanya biashara nyingine na wao wanafuata. Hawawekezi nguvu zao sehemu moja.

Sasa ngoja nikusimulie habari hii itakupatia jambo la kujifunza.

Miaka mingi iliyopita kulikuwa na Kamanda mmoja wa kikosi cha Hispania cha Kijeshi aliyekuwa anaitwa Hernan Cortes. Mwaka 1519 alipewa kazi ya kwenda kuvamia kisiwa kimoja nchini Mexico kilichoitwa Berecluse na akapewa wanajeshi 500 na meli 11. Walipofika pale Kisiwani akaagiza wanajeshi wote washuke pamoja na wale mabaharia. Waliposhuka akaagiza meli zote zichomwe moto. Walipochoma moto na moshi ulipoanza kupanda juu, akawaita wale wanajeshi na wale mabaharia akawauliza, mnaona nini? Wakasema tunaona meli zetu zinaungua. Akasema, safi sana. Akawaambia, tuna chaguzi mbili tu zilizobaki hapa, tushinde vita au tushindwe vita tuangamie wote hapa. Hakuna njia mbadala tofauti na hizo.

Matokeo yake yalikuwaje?

Walikuwa wanajeshi wachache sana lakini vita walishinda. Kwa nini? Ni kwa sababu waliamua kwa asilimia mia moja kufanya kile kitu walichokuwa wanakifanya.

Jambo la kujifunza ni hili, ili uweze kufanikiwa kwenye jambo lolote, usiseme ninajaribu. Sema ninafanya. Chochote unachoamua kufanya, jitoe kwa nguvu zako zote na utaona matokeo makubwa. Kuanzia leo, usiseme najaribu jaribu, bali sema nafanya. Na ukiamua kufanya, CHOMA MELI ZAKO ZOTE na utashinda.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Mojawapo ya majuto ambayo watu wengi hupitia hasa umri wao unapokuwa umekwenda ni kuwa, hawakuishi maisha waliyokuwa wanayataka na kufanya kile kitu walichokuwa wanakipenda. Na pia hawakufikia malengo yao ya maisha kama walivyokuwa wanatamani kufikia. Katika Makala hii tutaangalia jambo kubwa ambalo limewachelewesha wengi kufanikiwa kufikia malengo yao ambalo pia linaweza kukufanya ushindwe kufanikiwa kwenye malengo yako na jinsi ya kukabiliana nalo.

Tafiti nyingi sana zinaonesha watu wengi sana hasa wanapokaribia kufa hujilaumu maisha waliyoishi. Mwanasaikolojia mmoja anayeitwa Daniel Amend aligundua kanuni nzuri sana inayoitwa 18, 40, 60. Kanuni hii ilikuwa inasema hivi:

Mtu anapokuwa na umri wa miaka 18-39 huwa anajiuliza nikifanya jambo hili, kazi hii au biashara hii watu watanionaje? Watu wa kundi hili maisha yote yanaendeshwa na maoni ya watu na sio utashi wao.

Mtu huyu akifikisha umri wa miaka 40-59 huwa anaanza kusema, kwa sasa umri wangu umekwenda hivyo sitojali. Mimi nitafanya, mwenye kunisema na aniseme lakini mimi nitafanya ili kufanikiwa.

Mtu huyu anapofikisha umri wa miaka 60 na kuendelea anakuja kugundua kuwa, watu aliokuwa anawafikiria kuwa wanamuwazia yeye hawakuwa wanamfikiria kabisa na wala hawakuwa na mpango naye. Wao pia walikuwa wanahangaikia maisha yao.

Baada ya kuona kanuni hiyo utagundua kuwa ndivyo maisha yalivyo. Watu wengi wanaishi wakiogopa kufanya kitu ambacho kingebadilisha maisha yao wakifofia kuwa watu watawaonanje au kuwafikiriaje. Kumbe wale ambao wanawahofia na wao wana mambo yao na wala hawana muda wa kuwafirikia.

Jambo kuwa ambalo unapaswa kulizingatia ili uweze kufanikiwa ni kuwa, usiwe mtu wa kuishi ili kuwaridhisha watu. Ishi maisha yako. Kama una malengo ya maisha uliyojiwekea na unahisi kuwa ukiyafanya yatabadilisha maisha yako, fanya kwa nguvu zako na akili zako zote. Usihofu kuwa watakuonaje. Kumbuka kuwa hakuna aliye na muda wa kujali au kuangalia maisha yako. Ukiwaangalia na kuwahofia watu, unajichelewesha mwenyewe.

Mfano, watu wengi wanaishi kwenye nyumba zenye gharama kubwa kupita uwezo au kipato chao, wamechukua mikopo wakanunua magari ili kuwaridhisha watu, wananunua nguo za gharama kubwa kuliko uwezo wao. Hii ni kwa sababu walitaka kuwaridhisha watu na hivyo wakajikuta wapo kwenye msongo mkubwa wa madeni katika maisha yao.

Kitu cha msingi katika maisha yako ni kuishi maisha yako na kufanya kitu unachokipenda ambacho unaona kitaleta mapinduzi kwenye maisha yako bila kuangalia watu watasemaje. Nimatumaini yangu umepata maarifa ya msingi sana ambayo yatakusaidia kufanikiwa kufikia malengo yako. Kama una maoni yoyote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kama utahitaji ushauri zaidi kwa simu na. 0752 081669. Asante na karibu katika Malala ijayo.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Karibu mpendwa msomaji katika Makala hii ya leo. Katika Makala hii nitaelezea jambo moja kubwa unalopaswa kulizingatia na kulifanyia kazi ili uweze kufanikiwa katika maisha. Inawezekana umekuwa ukitumia juhudi kubwa katika kazi zako ili uweze kujikwamua kimaisha lakini matokeo yanakuwa hayaonekani. Nikuhakikishie kuwa ukifuatilia Makala hii mwanzo hadi mwisho utakuwa umepata kitu cha msingi sana ambacho kitakusaidia uweze kufanikiwa katika maisha yako. Karibu tuendelee.

Je ulishawahi kujiuliza ni kitu gani kinawatofautisha watu waliofanikiwa sana na wale ambao hawajafanikiwa? Katika Makala hii ya leo ningependa nikushirikishe kitu kimojawapo ambacho kinaweza kukusaidia sana kwenye maisha yako. Kitu hicho ni uwezo wa kupanga malengo na kuyafuatilia.

Watu  wengi wanaamka kwenda kazini lakini ukiwauliza baada ya miaka kumi watakuwa akina nani hawawezi kukujibu. Sasa hebu nikushirikishe utafiti uliowahi kufanywa na Chuo Kikuu cha Havard cha nchini Marekani.

Chuo kikuu cha Havard mwaka 1979 kwenye kitengo cha biashara walifanya utafiti. Walikusanya wanafunzi 100 ili waweze kuwafanyia utafiti. Utafiti huo ulikuwa ni wa kuwauliza maswali. Waliwauliza kuwa,  wakimaliza shule baada ya miaka kumi watakuwa ni wapi ki-maisha au watakuwa na mafanikio gani? Wanafunzi hao walitoa majibu kama ifuatavyo:

Asilimia 84 ya wanafunzi walikuwa hawajui watakuwa wapi, hivyo hawakuwa na mpango wowote katika maisha yao. Walikuwa wakisoma lakini walikuwa hawajui maisha yao yatakuwaje.

Asilimia 13 ya wanafunzi  walikuwa wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote wa jinsi ya kupata kile kitu walichokuwa wanahitaji kwenye maisha yao.

Asilimia 3 ya wanafunzi walisema wanajua wanachokitaka na walikuwa wametengeneza mpango kamili wa jinsi ya kufanikiwa kupata kile walichokuwa wamekusudia kukipata.

Utafiti huo uliendelea baada ya miaka kumi .Baada ya miaka 10 Chuo cha Havard kiliwafuatilia wanafunzi hao ili kiweze kupata matokeo ya utafiti wao. Matokeo yaliyopatikana yalikuwa ni ya kushangaza.

Katika matokeo hayo:

Wale wanafunzi asilimia 13 ambao walisema wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote walikuwa wamefanikiwa  mara mbili zaidi ya wale asilimia 84 waliosema hawajui wanataka nini katika maisha yao.

Wale wanafunzi asilimia 3 ambao walisema wanajua wanachokitaka na wametengeneza mpago kamili wa jinsi ya kufanikiwa walikuwa wamefanikiwa mara 10 zaidi ya wale wanafunzi wengine wote.

Utafiti huu ukahitimisha kuwa, unapokuwa na malengo yako na ukayaishi, una uwezo wa kufanikiwa mara 10 zaidi ya wale ambao hawana malengo.

Kuanzia leo usiwe mtu asiyekuwa na malengo. Tumia muda kutafakari na kujiuliza miaka 10 ijayo utakuwa wapi?

Utakuwa na kiwango gani cha elimu.

Utakuwa na cheo gani.

Utakuza biashara yako kwa kiwango gani na kadhalika.

Hivyo, uwezo wa kupanga malengo na kuyaishi ni muhimu sana katika maisha yako. Usiishi kama mtu asiyekuwa na mwelekeo. Weka malengo na upange namna ya kuyafikia. Unapoamka asubuhi hakikisha unapitia malengo yako uliyojiwekea ili usiweze kupoteza muda wako kwa mambo ambayo yako nje ya malengo yako.

Chukua muda kutafakari na kupanga malengo yako unataka kuwa nani na wapi katika maisha. Unaweza kunishirikisha kwa kukomenti hapo chini. Asante sana na karibu katika Makala ijayo.

Kutengeneza Pesa Kupitia Blog: Mambo 6 Ya Kuzingatia.

Kutengeneza Pesa Kupitia Blog: Mambo 6 Ya Kuzingatia.

Hivi unajua kuwa watu wengi wanashindwa kuanzisha na kumiliki blog kwa kudhani kuwa ni kitu kigumu na kisichowezekana? Lakini ukweli ni kuwa kuanzisha na kumiliki blog ni jambo rahisi kuliko unavyoweza kufikiria. Hivyo katika makala hii nitakuelezea mambo sita ya msingi ya kuzingatia ili uweze kuwa na blog yenye mafanikio na Kutengeneza pesa kupitia blog yako.

Katika makala iliyopita iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho “Sababu kumi za msingi za wewe kuwa na blog yako mwenyewe ambayo itakuingizia kipato“, nilielezea kwa kina maana halisi ya blog na pia nilifafanua sababu za msingi ambazo wewe mpendwa msomaji wangu unapaswa kuwa na blog yako mwenyewe na namna ambavyo itakunufaisha na kuwa chanzo cha kukuingizia kipato.Kama hukuisoma makala hiyo nakushauri uanze kwanza kuisoma makala hiyo halafu ndio uendelee na makala hii.

Ili uweze kuanzisha blog na kutengeneza pesa kupitia blog yako, unapaswa kuzingatia na kufanyia kazi mambo yafuatayo :

Kutengeneza pesa kupitia blog: Mambo 6 ya kuzingatia.

1.Andika makala nyingi iwezekanavyo.

Ili uweze kufanikiwa kutengeneza pesa kupitia blog yako, unapaswa kuandika makala nyingi iwezekanavyo. Jiwekee ratiba na uifuate ya kuandika makala kila siku au kila baada ya siku mbili. Jambo la msingi ni kuwa, blog yako isikae muda mrefu bila kuweka makala mpya.

2. Penda Kusoma Sana

Ili uweze kuwa na vitu vingi vya kuandika kwenye blog yako, unapaswa kusoma sana kuhusiana na mada unazoandikia blog yako.

3. Wapende na kuwathamini wasomaji wako.

Jambo jingine la kuzingatia ili uweze kutengeneza pesa kupitia blog, jitahidi kusoma na kujibu maoni na maswali ya wasomaji wako mara tu yanapotokea. Kwa kufanya hivyo wasomaji wako watakupenda na kukuheshimu.

4. Usiogope kuandika.

Ili uweze kufanikiwa kutengeneza pesa kupitia blog, unapaswa kutokuogopa kuandika maarifa uliyonayo kuhusiana Mada unazoandikia blog yako. Usiwaze watu watakufikiriaje. Kumbuka kuwa maarifa au ujuzi ulionao ni wa thamani sana kwa mtu fulani na kwamba akiupata utamsaidia na atakushukuru.

5. Penda kujifunza vitu vipya kila siku kuhusiana na ujuzi wako.

Jambo jingine la kuzingatia ili uweze kutengeneza pesa kupitia blog ni kutambua kuwa wewe huwezi kuwa unajua vitu vyote, hivyo unapaswa kujifunza vitu vipya kila siku ili uweze kuandika makala bora na zenye kugusa jamii.

6. Kuwa na subira.

Mafanikio katika blog hayapatikani kwa siku moja. Hivyo endelea kuandika makala nyingi iwezekanavyo zinazoelimisha jamii,watu watakupenda,watakuheshimu na kukuthamini na matokeo yake utayaona baadaye.

Kwa leo niishie hapo. Kama una maoni au swali lolote kuhusiana na makala hii ya jinsi ya kutengeneza pesa kupitia blog, usisite kuandika hapo chini. Au unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja kupitia namba yangu ya whatsap 0752081669.

Asante na karibu katika makala ijayo.

Hatua 6 Za Kuanzisha Blog.

Hatua 6 Za Kuanzisha Blog.

Karibu mpendwa katika makala hii. Katika makala hii nitazungumzia hatua 6 za kufuata ili uweze kuanzisha na kumiliki blog itakayokuletea pesa mtandaoni.Hivi unajua kuwa kwa kuanzisha blog unaweza kutumia elimu au ujuzi ulionao kujiingizia kipato mtandaoni bila kuathiri shughuli zako zingine?

Katika makala zilizopita nilielezea maana ya blog na sababu za msingi za wewe kuwa na blog yako mwenyewe. Kama hujapitia makala hiyo unaweza kuipitia halafu ndio uendelee na makala hii. Katika makala hii nitakuelezea hatua sita muhimu za kufuata ili uweze kuanzisha na kumiliki blog itakayokuletea kipato mtandaoni.

1. Chagua Mada (niche) utakayokuwa ukiandikia makala zako.

Hatua ya kwanza kabisa unapotaka kuanzisha blog ni kuchagua mada (niche). Blog nyingi huwa zinaelezea Mada moja. Kwa mfano, kuna blog zinazoandika michezo, habari, afya, elimu na mada zingine nyingi. Hivyo kama wewe una ujuzi wowote, chagua mada ya kuandika kwenye blog yako. Usichanganye mada nyingi kwenye blog yako.

2. Chagua Sauti yako ya kiuandishi (choosing your own voice)

Kitu kizuri sana ninachokipenda kwenye blog ni kuwa, kila mwandishi ana mfumo wake. Hivyo unaweza kuchagua mfumo wowote wa kiuandishi katika blog yako. Kwa mfano : unaweza kuwa unaandika makala katika mfumo wa kitaalamu au unaweza ukawa unaandika makala za kawaida.

3. Chagua vitu vya kuandika kwenye blog yako.

Baada ya kuchagua Mada ya kuandika kwenye blog yako, hatua inayofuata ya kuanzisha blog ni kuchagua mambo ambayo utaandika na yale ambayo hutaandika.

4. Andika makala nzuri na zenye mvuto.

Ili uweze kuwa na wasomaji endelevu kwenye blog yako, unapaswa kuandika makala zenye mvuto na zinazotatua matatizo ya jamii.

5. Tambua aina za makala utakazoandika.

Hatua nyingine ya kuanzisha blog ni kuchagua mtindo wa makala zako. Kuna aina nyingi za mitindo ya uandishi wa makala baadhi yake ni hii ifuatayo :

Mtindo wa kuorodhesha (List) .

Kwa mfano :Mambo sita ya kufanya ili uweze kufanikiwa katika maisha.

Mtindo wa kuandika dondoo (Tips)

Kwa mfano :Ukitaka kufauru mtihani, zingatia mambo yafuatayo.

Mtindo wa kuelezea (review) huduma au bidhaa .

Mfano :Maelezo kuhusu simu ya IPhone 6.

Mtindo wa kupendekezea (recommendation) bidhaa au huduma.

Mfano :Ukitaka kupiga picha zenye ubora camera ya cannon itakufaa.

Mtindo wa ‘jinsi ya ‘(how to)

Mfano :Jinsi ya kuanzisha blog.

Mtindo wa mahojiano (interview)

Mfano :Kutana na Bilionea Maganga aliyeanza biashara yake kwa kuuza ubuyu.

Mtindo wa kutumia video

Mtindo wa kurekodi sauti (podcast)

Mtindo wa kualika wataalam wa mambo mbalimbali (guest post) kuandika makala kwenye blog yako.

6. Weka ratiba nzuri ya kuweka makala zako.

Weka ratiba nzuri ya kuweka makala zako. Ninakupendekezea uwe unaweka makala kila siku, kila baada ya siku mbili, mara mbili kwa juma n.k. Jambo la msingi la kuzingatia hapa ni kuwa na ratiba maalumu ya kuweka makala zako ili uweze kuwa na wasomaji wengi watakaofuatilia blog yako.

Nimatumaini yangu kuwa umejifunza kitu katika makala hii ya hatua za kuanzisha blog. Kwa maoni au swali au ushauri, usisite kuwasiliana nami kwa whatsap 0752081669. Au unaweza kuweka maoni yako hapa chini.

Karibu katika makala ijayo

Jinsi Ya Kuongeza Wasomaji Kwenye Blog Yako.

Jinsi Ya Kuongeza Wasomaji Kwenye Blog Yako.

Mpendwa, nikukaribishe tena katika makala hii. Katika makala ya leo nitazungumzia jinsi unavyoweza kuongeza wasomaji kwenye blog yako. Njia nitakazoeleza hapa zitakusaidia kuongeza maradufu wasomaji wa blog yako na hivyo kupata mafanikio kwenye blog yako.

Soma:Kuanzisha blog: Sababu 10 za kuanzisha Blog yako.

Jinsi ya kuongeza wasomaji kwenye blog yako.

1. Andika makala mara kwa mara kwenye blog yako.

Weka makala mpya mara kwa mara kwenye blog yako. Unaweza kuandika makala, ukaposti picha au ukaweka makala za sauti (Podcasting).

Weka ratiba maalumu kwa ajili ya kuweka makala mpya kwenye blog yako.Ratiba husaidia kuwafanya wasomaji wako wajue ni wakati gani wategemee makala mpya.

2. Wasikilize wasomaji wako na ujibu maoni au maswali yao.

Miongoni mwa vitu vizuri sana ambavyo unaweza kuvifanya kwa wasomaji wako ni kuhakikisha kuwa kila msomaji wako anafurahia kuwa kwenye blog yako. Weka kwenye blog yako ukurasa wa mawasiliano ili kama kuna swali uweze kulijibu haraka iwezekanavyo. Kama kuna maoni yoyote kwenye makala zako, jitahidi kuyajibu haraka. Kwa kufanya hivyo, utaweza kuongeza wasomaji kwenye blog yako.

3. Tembelea Blog zingine na majukwaa mbalimbali na uchangie mada zinazotolewa.

Ili uweze kuwa na wasomaji wengi kwenye blog yako, unatakiwa kushiriki kwenye blog za watu wengine kwa kuchangia maoni yako. Tafuta blog zinazoandika makala kama zako na uwe unatoa maoni yako. Unapokuwa unatoa maoni usisahau kutaja blog yako. Kwa kufanya hivyo utafanya blog yako kutambulika na hivyo kupata wasomaji wengi.

4. Alika miongoni mwa wasomaji wako kuandika makala.

Pia, ili uweze kuongeza wasomaji, unaweza kualika miongoni mwa wasomaji wako kuandika makala. Hii itasaidia kuifanya blog yako kuwa na makala zenye ladha tofauti.

5. Wasiliana na wasomaji wako kwa njia ya email.

Waalike wasomaji kujisajiri (subscribe) ili waweze kupata taarifa kila unapoweka makala mpya. Kuna namna nyingi ya kufanya wasomaji wajisajiri ili kupata taarifa kila unapoweka makala. Mojawapo ya njia hizo ni kuweka kifaa cha kukusanyia taarifa za wasomaji wako kama vile jina na baruapepe (email). Hivyo msomaji anapokuwa amependezwa na makala zako atajisajiri ili aweze kupata taarifa kila unapoweka makala mpya. Mfano wa kifaa hicho ni MailChimp

6. Unganisha blog yako na mitandao ya kijamii.

Miongoni mwa njia bora kabisa za kuongeza wasomaji wa blog yako ni kuiunganisha na mitandao ya kijamii kama vile facebook, twitter, Pinterest na LinkedIn .Mitandao hii ina watu mamilioni. Hivyo unapokuwa na kurasa kwenye mitandao hii na ukawa unashea makala zako, utapata wasomaji wengi.

7. Shirikisha wasomaji wako kutoa maoni yao kwa kuwauliza maswali.

Shirikisha wasomaji wako kwa kuwauliza maswali mbalimbali kuhusiana na makala unazotoa ili watoe maoni yao. Unaweza kukusanya maoni ya wasomaji kwa kuweka kifaa kinachoitwa Survey Monkey kwenye blog yako.

8. Zingatia blog yako kuonekana vizuri kwenye simujanja (smartphone).

Hakikisha kuwa blog yako inaonekana vizuri kwenye smartphone ili uweze kupata wasomaji wengi kwani kwa sasa watu wengi wanatumia simu za mkononi.

9. Andika mada tofauti tofauti kwenye blog yako.

Ili uweze kuongeza wasomaji wengi, unaweza kuchanganya mada tofauti tofauti kwenye blog yako. Lakini zingatia mada hizo ziwe zinaendana na malengo ya blog yako. Kwa mfano blog yako inahusu biashara, unaweza kuandika makala ya namna ya kuanzisha biashara, lakini pia unaweza kuchanganya makala kama vile namna ya kutangaza biashara kwenye mitandao ya kijamii n.k

Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yatakusaidia kuboresha blog yako. Kwa maoni au ushauri usisite kuweka maoni yako hapa chini. Lakini pia unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja kwa njia ya whatsap 0752081669.

Asante na karibu katika makala ijayo.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp