Sababu 6 Usizozijua Zinazozuia Mafanikio Yako.

Sababu 6 Usizozijua Zinazozuia Mafanikio Yako.

Kila mmoja anahitaji kufanikiwa katika malengo aliyojipangia. Hata wewe ninaamini una malengo ambayo umeyaweka kwa mwaka huu Ili uweze kuyakamilisha. Malengo ambayo yatakutoa kutoka hatua moja kwenda nyingine. Watu wengi wamekuwa wakiweka malengo makubwa katika maisha yao lakini wameshindwa kupata matokeo waliyokusudia. Kuna sababu nyingi zinazochangia kushindwa kufikia malengo uliyojipangia. Katika makala ya leo nitakushirikisha sababu 6 usizozijua zinazozuia mafanikio kwenye malengo yako.

Sababu 6 usizozijua zinazozuia mafanikio kwenye malengo yako.

1. Kuwa na malengo mengi bila Kuweka vipaumbele.

Miongoni mwa sababu zinazozuia mafanikio kwenye malengo yako, sababu ya kwanza kabisa ni kuwa na malengo mengi bila kuweka vipaumbele. Unapokuwa na malengo mengi, siyo rahisi kupata matokeo makubwa. Hii ni kwa sababu, kila lengo unaloliweka litahitaji rasilimali ya muda, nguvu, pesa na kadhalika. Kwa hivyo, unapokuwa na malengo mengi utajikuta kuwa unatawanya rasilimali zako kidogo kidogo kwenye kila lengo na hivyo utapata matokeo madogo kwenye kila lengo. Hivyo, ili uweze kupata matokeo makubwa ni sharti uwe na malengo machache na uwekeze rasilimali za kutosha kwenye malengo hayo. Kama una malengo mengi ni sharti uwe na vipaumbele uanze na malengo yapi kisha utakapofanikiwa uhamie malengo mengine. Unaweza kugawanya malengo yako katika sehemu tatu: malengo ya muda mfupi, malengo ya muda wa kati na malengo ya muda mrefu.

2. Kutofanya jambo linalochangia malengo Yako Kila siku.

Unapokuwa umeweka malengo yako, kwa mfano malengo ya mwaka, gawa malengo hayo sehemu ndogo ndogo ili upate malengo madogo ya kufanya kwa mwezi, juma na siku. Hii itakusaidia kuwa na kitu cha kufanya kila siku kinachochangia malengo yako. Kwa kufanya hivyo utajikuta unatimiza malengo yako hata kama yalikuwa ni makubwa kiasi gani.

3. Kutokujenga tabia ambazo zitakuwezesha kufanikisha malengo yako.

Unapokuwa umeweka lengo, ni lazima ujenge tabia ambazo zitakusaidia kuweza kutimiza lengo hilo. Kwa mfano: umeweka lengo la kuandika kitabu mwaka huu. Hapa ni lazima ujenge tabia mpya ambazo inawezekana haukuwa nazo. Mfano wa tabia hizi ni kama vile kujisomea vitabu, kuandika na kadhalika. Hivyo, kila lengo utakaloliweka litahitaji tabia fulani ambazo lazima uzijenge ili uweze kufanikiwa.

4. Kushindwa kuwekeza kwenye maarifa na ujuzi unaohitajika.

Katika kila lengo utakaloliweka, utahitajika kupata ujuzi na maarifa ambayo yatakusaidia kufanikisha lengo lako. Maarifa hayo unaweza kuyapata kwa watu,kupitia kusoma vitabu,kuhudhuria semina au kusoma chuoni. Hivyo ili uweze kufanikiwa, ni lazima uwekeze ujuzi utakaohitajika kutimiza lengo lako.

5. Kushindwa kuwa na nidhamu binafsi (self discipline)

Kuwa na nidhamu binafsi ni kuwa na uwezo wa kujitawala na kuwajibika. Hapa ni lazima uhakikishe mambo uliyoyapanga unayatimiza kwa muda muafaka. Ni lazima uwe na ratiba ya kutimiza malengo yako na uisimamie. Watu wengi huwa wanaweka malengo mazuri lakini huwa wanakosa nidhamu binafsi ya kuhakikisha malengo waliyoyaweka yanatimia kwa muda muafaka.

6. Kuwa na tabia ya kughairisha mambo

Hii ni sababu nyingine inayowafanya watu wasiweze kuchukua hatua kutimiza malengo yako. Huwa wanasubiri mpaka wawe na kitu fulani ndio waanze. Tabia hii inachelewesha sana mafanikio. Unapokuwa umeweka malengo, usisubiri mpaka uwe umekamilika. Anza na ulichonacho na milango itafunguka mara tu utakapokuwa umeamua kuanza.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yamekusaidia kufahamu sababu 6 usizozijua zinazozuia mafanikio yako. Kama una swali au maoni yoyote, usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu katika makala zijazo.

Jinsi Ya Kutumia Pesa Zako Vizuri Ili Ufanikiwe.

Jinsi Ya Kutumia Pesa Zako Vizuri Ili Ufanikiwe.

Katika maisha kila mtu huwa anapata kipato. Kipato hiki inawezekana kikawa kinatokana na ajira, kujiajiri au kufanya biashara. Hata wewe ninaamini huwa unapata kipato. Lakini, mafanikio katika maisha, hayatokani na kiwango cha pesa unachopata bali yanatokana na kiwango unachobakiza kwenye kila pesa inayopita mkononi mwako. Hii ndio sababu unaweza kuona mtu fulani alikuwa anapata kipato kikubwa lakini baada ya muda unashangaa kuona kuwa amezidiwa maendeleo na mtu ambaye alikuwa na kipato kidogo. Hivyo, ili uweze kufanikiwa na kuwa na uhuru wa kifedha, ni lazima ufahamu Kanuni za fedha za kuzingatia. Katika makala ya leo nitakushirikisha jinsi ya kutumia pesa zako vizuri ili uweze kufanikiwa na kuwa na uhuru wa kifedha.
Jinsi ya kutumia pesa zako vizuri ili uweze kufanikiwa.
Katika makala hii nitakushirikisha kanuni moja ya fedha iliyotungwa na Northcoste Parkinson’s. Kanuni hii inaitwa “Parkinson’s law”.
Kanuni hii inasema: Siku zote matumizi ya mtu huwa yanaongezeka kila mara kipato chake kinapoongezeka.
Hivyo, ili uweze kuwa na uhuru wa kifedha ni sharti ufanye maamuzi ya kupingana na kanuni hii ya Parkinson. Yafuatayo ni mambo ambayo unapaswa kuyafanya.

1. Hakikisha kuwa kipato chako kinaongezeka kwa kasi kuliko matumizi yako.
Hili ni jambo la kwanza kabisa na la muhimu kama unataka kuwa na uhuru wa kifedha. Maana yake ni kuwa, kama kipato chako kitaongezeka asilimia 20, basi ni sharti matumizi yako yawe chini ya asilimia 20.

2. Kuamua kujilazimisha kuendelea kuishi maisha uliyokuwa unaishi hata baada ya kipato chako kuongezeka.
Hapa inamaanisha kuwa, unaamua kuwa hautaongeza matumizi kwa kipindi fulani mpaka pale kipato chako kitakapofikia asilimia fulani. Lakini pia, hata kama utafikia asilimia ya ongezeko uliyokusudia, basi kama utaamua kuongeza matumizi basi yanatakiwa yawe chini ya asilimia ya ongezeko la kipato chako.
Lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha unabakiza pesa ya ziada ambayo utaitumia kwenye uwekezaji au kufanya jambo ambalo ni la kimaendeleo. Watu wengi wameshindwa kufanikiwa kwa sababu kila mara vipato vyao vilipoongezeka, waliongeza matumizi na hivyo kujikuta wanaendelea kuishi kwenye mzunguko wa kanuni ya Parkinson. Hivyo, kuanzia leo kama unahitaji kufanikiwa, hakikisha unavunja kanuni hii ili uweze kufanikiwa kwenye maisha yako.
Nimatumaini yangu umepata maarifa ambayo yatakusaidia namna ya kutumia pesa vizuri ili uweze kufanikiwa katika maisha kwa kuwa na uhuru wa kifedha. Kama una swali au maoni, basi usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena katika makala ijayo.

Jinsi Ya Kutumia Ujuzi Wako Kujiajiri Mtandaoni

Jinsi ya kutumia ujuzi wako wako kujiajiri Mtandaoni

Katika maisha, kila mtu ana ujuzi wake. Ujuzi huu unatokana na kusomea chuoni, kufundishwa nyumbani au mtaani. Hata wewe inawezekana una ujuzi ambao umesomea chuoni au umejifunza mahali fulani. Changamoto kubwa ambayo inajitokeza hapa ni kwa jinsi gani unaweza kutumia ujuzi wako kujiajiri na kutengeneza kipato. Katika makala hii nitakushirikisha jinsi ya kujiajiri mtandaoni na kutengeneza kipato kwa kutumia ujuzi wako.
Katika makala yangu ya njia 10 za kutengeneza pesa mtandaoni nilielezea kwa ufupi njia ambazo unaweza kuzitumia kuweza kujiajiri mtandaoni na kutengeneza kipato. Katika makala hii nitaelezea kwa kina njia moja ya kujiajiri mtandaoni ambayo ni kuanzisha blog. Hapa nitazungumzia jinsi unavyoweza kujiajiri kwa kuanzisha blog ya kitaalamu (niche blog).
Maana ya blog ya kitaalamu (niche blog).
Niche blog au kwa Kiswahili blog ya kitaalamu ni aina ya blog ambayo imejikita katika kufundisha ujuzi wa aina moja. Hapa ina maanisha kuwa, kama wewe una maarifa au ujuzi wa kilimo, basi blog yako itajikita katika kufundisha kilimo tu bila kuchanganya mambo mengine yasiyohusu kilimo. Vivyo hivyo, kwa ujuzi wa aina nyingine kama vile Sheria, Biashara, Elimu, Afya, Mapambo, Mitindo, Ujasiriamali na kadhalika.
Hivyo, kwa kutumia ujuzi au maarifa yoyote uliyonayo, unaweza kuanzisha blog inayotatua changamoto zinazoihusu jamii yako kupitia ujuzi ulionao. Jambo la kuzingatia ni kuwa, unapokuwa umeanzisha niche blog, lenga kundi la watu wanaohitaji ujuzi wako na ujitahidi kuandika makala zinazoelimisha na kutatua matatizo ya kundi hilo. Usichanganye mada. Kama umeamua kuanzisha blog ya kufundisha mapishi au ujasiriamali, usichanganye na mada za siasa. Hii ni kwa sababu, watu watakaokuwa wasomaji wa blog yako ni wale wanaohitaji ujuzi wako na si vinginevyo.
Kwa nini unapaswa kuwa na blog ya ujuzi au utaalamu wako?
Sasa hebu tuangalie ni faida gani utazipata unapokuwa umeanzisha blog ya ujuzi au utaalamu wako.
1. Utapata wasomaji wanaopenda kufuatilia maarifa au ujuzi wako (Loyal readers)
Ukiwa na blog ya kufundisha utaalamu wako, utapata watu wenye changamoto katika jamii wanaohitaji ujuzi wako ili waweze kutatua changamoto zao. Hivyo, watu watakupenda na kukuheshimu kwa sababu unawasaidia kutatua changamoto zao.
2. Utajenga mtandao mkubwa (community) wa watu wenye ujuzi kama wa kwako na wanaopenda kujifunza ujuzi wako.
Kwa kuwa na mtandao mkubwa wa watu wenye ujuzi kama wa kwako, mtaweza kubadilishana maarifa na hivyo kukuza ujuzi wako.
3. Utatambulika katika jamii kuwa wewe ni mtaalamu.
Unapokuwa umeanzisha blog ya utaalamu wako, na ukawa unaandika makala zinazotatua matatizo katika jamii, jamii itakutambua kuwa wewe ni mtu wa kutegemewa.
4. Utakuza jina lako (Brand, Credibility and Profile)
Ukiwa unaandika makala zinazoelezea mada moja kwa muda mrefu, utaifanya blog yako iwe ni sehemu inayoaminika na kuheshimika (trusted source) kwa maarifa unayofundisha. Ukifanya hivyo kwa usahihi, utatambulika kuwa ni mtaalamu uliyebobea kwenye kada unayofundisha.
Faida za kuwa mtaalamu uliyebobea ni nyingi. Mojawapo kubwa ni pale utakapokuwa na bidhaa au huduma unayotaka kuuza. Badala ya kuanza kusaka wateja, utashangaa kuwa watu ndio watakutafuta wewe wakihitaji huduma yako kwa kuwa wanakutambua kuwa wewe ni mtaalamu uliyebobea.
5. Utaweza kuuza bidhaa zako.
Unapokuwa na blog inayoelezea mada au ujuzi wa aina moja, ni rahisi kuuza bidhaa zinazoendana na ujuzi unaofundisha na watu wakanunua. Hii ni kwa sababu, wasomaji wa blog yako watakuwa ni wale wanaopenda na kuhitaji ujuzi wako. Mfano: Ukiwa na Blog ya Ujasiriamali, ni rahisi kuuza vitabu, kozi au bidhaa zinazohusu ujasiriamali. Kadhalika kwa blog zenye ujuzi wa aina nyingine.
6. Ni rahisi kupata watu au makampuni ya kuweka matangazo kwenye blog yako.
Ukiwa na blog yenye mada au ujuzi wa aina moja, ni rahisi kupata watu au makampuni yanayotoa huduma inayofanana na ujuzi wako na wakahitaji kuweka matangazo yao ya biashara. Kwa mfano: Kama blog yako imejikita katika kuelezea mitindo mbalimbali ya nguo, ni rahisi kupata watu wanaohitaji kutangaza bidhaa zao za nguo kwenye blog yako, nao wakakulipa kwa kuweka matangazo yao.
7. Blog yako itaonekana kwa urahisi watu wanapoitafuta Google (Search engine optimization).
Google huwa inatoa kipaumbele kwa blog zinazoelezea mada ya aina moja. Hivyo blog yako itaonekana kwenye ukurasa wa kwanza. Kwa mfano: kama blog yako inahusu ufugaji wa kuku, na mtu akaandika neno ufugaji wa kuku Google, blog yako itaonekana juu kwa sababu, ina makala nyingi za ufugaji wa kuku.
8. Utaweza kuandika makala nyingi.
Unapokuwa unafundisha ujuzi unaoupenda, utakuwa na vitu vingi vya kuandika. Hivyo kila siku utakuwa unapata mawazo na maarifa mapya ya kuandika kwenye blog yako.
9. Blog yako haitapata ushindani mkubwa (Less competition)
Blog za kitaalamu huwa ni chache na huwa zinalenga kundi fulani la watu. Hivyo, unapokuwa unaandika makala zenye mada ya aina moja, utapata faida ya kutokupata ushindani mkubwa mtandaoni.
Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ya jinsi ya kujiajiri mtandaoni kwa kutumia ujuzi wako. Kama utahitaji kuanzisha blog wewe mwenyewe, nimeelezea kwa kina na hatua kwa hatua jinsi ya kuanzisha blog kwenye makala yangu ya Jinsi ya kuanzisha blog na kutengeneza kipato. Pia kama utahitaji huduma ya kutengenezewa blog, unaweza kuwasiliana nami kwa simu namba. 0752 081669. Kama una maoni au swali lolote kuhusiana na mada hii, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Asante na karibu kwenye makala zijazo.

Faida 10 Usizozijua Za Kuanzisha Blog Yako.

Faida 10 za Kuanzisha blog


Kwa nini unapaswa kuanzisha blog? Kama limekuwa ni swali ambalo umekuwa ukijiuliza kwa muda mrefu, basi nikuhakikishie kuwa, makala hii ni kwa ajili yako. Katika makala hii, nitakushirikisha faida 10 usizozifahamu za kuanzisha blog yako.
Kabla ya kuendelea kwenye faida za kuanzisha blog, hebu kwanza nizungumzie maana ya blog pamoja na aina zake.
Maana ya blog.
Kwa tafsiri rahisi, blog ni aina ya tovuti. Aina hii ya tovuti inakuwa na vitu vifuatavyo:
i. Makala: Blog inakuwa na makala ambazo zinaandikwa mara kwa mara. Kila makala moja inapoandikwa inakuwa juu ya makala ya zamani. Kwa mfano, kama uliandika makala juzi na jana, makala ya juzi itakuwa chini ya makala ya jana. Mfano mzuri wa blog ni hii uliyopo kwa sasa.
ii. Sehemu ya kuweka maoni: Kila makala inapowekwa kwenye blog, kwa chini yake huwa kunakuwa na sehemu ya kuweka maoni. Hivyo, kama msomaji atakuwa amepata swali au maoni yoyote kuhusiana na makala husika, ataweza kuweka maoni yake kwenye sehemu ya kuwekea maoni.
iii. Maktaba: Hii ni sehemu ambayo makala zote za blog zilizowahi kuandikwa huhifadhiwa.
Aina za Blog.
Kuna aina nyingi sana za blog na nitakutajia aina chache tu kama ifuatavyo:
i. Blog binafsi (Personal blog)
Hizi ni blog ambazo huanzishwa na watu binafsi ili kuelezea mambo yao binafsi ya ki-maisha.
ii. Blog za biashara.
Hizi ni blog ambazo huanzishwa na watu au wafanyabiashara ili kutangaza bidhaa au huduma zao na kuweza kuwasiliana na wateja wao.
iii. Blog za kitaalamu.
Hizi ni blog ambazo huanzishwa na watu ambao ni wataalamu wa fani fulani ili kuweza kutoa elimu kutokana na utaalamu wao. Kwa mfano, kuna blog za kilimo, afya, elimu, mapambo, mapishi, mitindo na kadhalika.
iv. Blog za habari.
Hizi ni blog zinazotoa habari na matukio yanayotokea kila siku. Mfano blog ya Milladayo.
v. Blog za Burudani.
Hizi ni blog zinazoandika habari za michezo na burudani. Mfano blog ya Salehe Jembe.
Faida 10 Za kuanzisha Blog.
Kuna faida nyingi sana za wewe kuanzisha blog. Miongoni mwa faida hizo ni hizi zifuatazo:
1. Blog itakujengea ujasiri na kufahamika.
Ukiwa na blog utaweza kufahamina na watu wengi na hivyo kukuza jina lako. Kutokana na kukuza jina lako, utakuwa na followers wengi. Hivyo, ukihitaji kuuza bidhaa au huduma, tayari utakuwa na mtaji wa watu wengi wanaokufahamu.
2. Kupata watembeleaji wengi (Traffic) kwenye bidhaa au huduma unayotoa.
Kama utakuwa unauza bidhaa au unatoa huduma mtandaoni, unapokuwa na blog na ukawa unaandika makala mbalimbali za kuelimisha, utapata watembeleaji wengi kwenye blog yako na hivyo utaweza kuwauzia bidhaa au huduma unayotoa.
3. Kuongeza wigo wa marafiki (Network)
Unapokuwa na blog, utaweza kufahamiana na watu wengi kutokana na makala unazoandika na hivyo kuweza kukuza mtandao wa marafiki.
4. Kuongeza Mauzo (Sales)
Pamoja na kufahamiana na kuongeza mtandao wa marafiki, makala unazoandika zitakufanya uaminike (Trust) na kukujengea heshima (credibility) mambo ambayo ni ya msingi katika kuongeza mauzo ya bidhaa au huduma unayotoa.
5. Kujifunza zaidi.
Ili uweze kuandika makala mara kwa mara, utatakiwa kujifunza zaidi. Hivyo, kwa kuwa na blog, itakufanya uweze kujifunza kila siku mambo mapya kutokana na mada unayoandikia kwenye blog yako.
6. Kuibadilisha jamii kwa kufanya vitu vya tofauti.
Kama una maarifa ambayo ufikiria ukiyatoa kwa jamii yako yataleta mabadiliko, basi, kwa kutumia blog utaweza kuielimisha jamii yako na jamii itakupenda na kukuheshimu.
7. Utaweza kuwasaidia watu.
Kama una ujuzi wowote ambao inawezekana ni wa kujifunza au umesoma chuoni, kwa nini usiwashirikishe watu ujuzi ulionao? Kwa kutumia blog, utaweza kuwashirikisha watu ujuzi wako nao watakupenda na kukuheshimu.
8. Utaweza kutangaza biashara yako.
Kama una bidhaa au huduma yoyote, blog ni sehemu nzuri sana ya kuweza kutangaza biashara yako.
9. Jamii itakutambua kuwa wewe ni mtaalamu (Expart)
Unapokuwa na blog, utaweza kuelimisha jamii ujuzi ulionao. Hivyo, jamii itakueshimu na kukutambua kuwa wewe ni mtaalamu wa fani au ujuzi huo.
10. Utatengeneza pesa.
Unapokuwa na blog na blog yako ikawa na watembeleaji wengi, utaweza kutengeneza pesa. Katika kutengeneza pesa, kuna njia nyingi ambazo unaweza kuzitumia. Njia hizo zimegawanyika katika makundi mawili ambayo ni:
i. Njia za moja kwa moja (Direct methods)
ii. Njia zisizo za moja kwa moja (Indirect method)
i. Njia za moja kwa moja ni (Direct methods)
Njia za moja kwa moja ni njia ambazo utapata kipato moja kwa moja kutoka kwenye blog yako. Ingawa njia hizi sikupendekezei uzitumie kwenye blog yako kwani ili uweze kupata kipato kupitia njia hizi, ni lazima blog yako iwe na watembeleaji wengi. Mojawapo ya njia hizo ni:
-Kuweka matangazo ya biashara kwenye blog yako (Advertisements)
-Kupata makampuni yatakayodhamini blog yako.
Undani wa njia hizi nimeuelezea kwenye makala yangu ya njia za kutengeneza kipato kupitia blog.
ii. Njia zisizokuwa za moja kwa moja (Indirect methods)
Hizi ndio njia ambazo ninakushauri uzitumie, kwani zitakupatia kipato kikubwa hata kama blog yako itakuwa na watembeleaji wachache. Njia hizo ni pamoja na:
Kuandika na kuuza vitabu pepe (ebooks) kutokana na makala unazoandika.
Kuandaa kozi za mtandaoni kutokana na mada unazoandika na kuziuza kwa wasomaji wako.
-Kutoa huduma za kitaalamu za kulipia kwa wasomaji wako.
-Kuuza bidhaa zako zingine kwa wasomaji wa blog yako.
Njia hizi zote, nimezielezea kwa kina kwenye makala yangu ya njia za kutengeneza kipato kupitia blog.
Pia kama unahitaji kujifunza kutengeneza blog yako wewe mwenyewe, unaweza kupitia makala yangu ya jinsi ya kuanzisha blog, ambapo nimeelezea kwa kina na kwa lugha rahisi, jinsi ambavyo utaweza kuanzisha blog yako wewe mwenyewe. Lakini pia kama utahitaji huduma ya kutengenezewa blog, basi unaweza ukawasiliana nami kwa simu no. 0752 081669.
Ni matumaini yangu, kuwa umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na faida za kuanzisha blog yako. Kama una swali au maoni, usisite kuandika hapo chini. Pia unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja kwa kutumia na. 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye makala zijazo.

Mambo 3 Ya Kufanya Kila Siku Ili Kufanikiwa.

Mambo 3 Ya Kufanya Kila Siku Ili Kufanikiwa.

Mafanikio Katika maisha yanategemea na jinsi unavyoitumia siku moja uliyopewa ya kuishi. Pia mafanikio ya siku yanategemea ni kwa namna gani umetumia vizuri masaa na dakika kwa siku hiyo. Kumbuka kuwa, muda ni rasilimali ya muhimu sana ambayo kila mtu amepewa kwa usawa. Hivyo, mafanikio yoyote Katika maisha yanategemea kwa kiwango kikubwa na jinsi unavyotumia muda wako. Kumbuka kuwa, haitoshi kuweka malengo ya mwaka, malengo hayo hayataweza kufanikiwa kama hautajua namna ya kuitumia vyema kila siku inayokuja na kupita.
Maana ya mafanikio.
Mafanikio ni neno pana sana na tafsiri yake inatofautiana kati ya mtu mmoja na mwingine. Kwa ujumla, mafanikio ni kuweza kufikia malengo uliyokusudia katika maisha yako kama vile: kuhitimu masomo, Kuanzisha biashara, kujenga nyumba, kuongeza kipato chako, kuwa na maisha mazuri na kadhalika. Hivyo, Kila mmoja anaweza kutafsiri neno mafanikio kwa kuhusianisha na malengo aliyojiwekea. Katika makala ya leo, nitakushirikisha mambo 3 muhimu ya kufanya Kila siku Ili uweze kufanikiwa.
Mambo 3 ya kufanya Kila siku ili uweze kufanikiwa.

1.Weka orodha ya mambo unayopaswa kuyakamilisha.
Ili uweze kufanikiwa Katika maisha, ni lazima uwe na orodha ya mambo unayopaswa kuyakamilisha ndani ya siku husika. Orodha hii unatakiwa kuiandika siku moja kabla ili unapoamka asubuhi uwe na ufahamu wa mambo unayopaswa kuyafanya. Hii itakusaidia kutokupoteza muda wako kwenye mambo ambayo si ya msingi. Pia itakusaidia kutokufanya mambo ambayo haukuwa umeyapanga.

2.Tumia Kanuni ya 80/20
Kanuni ya 80/20 ni Kanuni maarufu sana ya mafanikio ambayo Kwa jina jingine inaitwa ‘Pareto Principle‘. Hii ni Kanuni ya muhimu sana ambayo itakusaidia kufanikiwa katika maisha. Kanuni hii inasema kuwa:
“20 percent of your activities will account for 80 percent of your results”.
Maana ya kanuni hii Kwa lugha ya kiswahili ni kuwa: asilimia 20 ya mambo unayoyafanya ndiyo yanayochangia asilimia 80 ya mafanikio yako. Halafu, asilimia 80 ya mambo unayoyafanya yanachangia asilimia 20 tu kwenye mafanikio. Maana yake ni kuwa, ili uweze kufanikiwa ni lazima ufahamu kuwa, kuna mambo machache ya muhimu ambayo ukiyafanya, ndiyo yanayochangia kwa kiwango kikubwa kwenye mafanikio yako. Halafu, mambo mengine yaliyobaki yanachangia sehemu ndogo ya mafanikio yako.
Kwa mujibu wa kanuni hii,unapokuwa umeweka orodha ya mambo ambayo utayafanya Kwa siku, hakikisha unaanza na mambo muhimu yanayochangia kwa kiwango kikubwa kwenye mafanikio yako. Weka nguvu na akili zako zote kwenye kutimiza mambo hayo ya muhimu sana halafu ndio umalizie na mambo ambayo yanachangia Kwa kiwango kidogo kwenye mafanikio yako.

3. Anza na mambo magumu.
Katika orodha ya mambo ya kufanya uliyoweka, unapoamka na kuanza kutekeleza, anza na mambo ambayo ni magumu. Hii ina faida kubwa sana kwani itakusaidia kuweza kuyafanya ukiwa na nguvu na hivyo kufanya Kwa ufanisi. Baada ya kuwa umemaliza kufanya mambo magumu ambayo yanahitaji umakini wa hali ya juu, basi hapo ndio utaweza kuhamia kwenye mambo rahisi.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa kuhusiana na mambo matatu muhimu unayopaswa kuyafanya kila siku ili uweze kufanikiwa. Kama una swali au maoni yoyote kuhusiana na mada hii, usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami moja Kwa moja Kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena katika makala ijayo.

Kanuni Ya Kupata Mafanikio: “The Equal Odds Rule”

Kanuni ya kupata mafanikio

Keith Simonton, mwanasaikolojia aliyehitimu masomo yake Chuo Kikuu cha Havard, mwaka 1977 alikuja na kanuni ya mafanikio inayojulikana kwa jina la The Equal Odds Rule. Kanuni hii aliiandika kwenye chapisho la “Creative productivity, age and stress: a biographical time-series analysis of 10 classical composers la mwaka 1977.
Kanuni ya The Equal Odds Rule inasema hivi:
“The average publication of any particular scientist does not have any statistically different chance of having more of an impact than any other scientist’s average publication.”
Kwa tafsiri rahisi ni kuwa, chapisho lolote la mwanasayansi yoyote haliwezi kuleta matokeo makubwa na ya tofauti kuliko chapisho la mwanasayansi mwingine.
Maana yake ni kuwa, ili mwanasayansi aweze kuleta matokeo makubwa na ya tofauti itategemea ni mara ngapi mwanasayansi huyo amerudia kufanya utafiti wa kile kitu kuliko wanasayansi wengine.
Hivyo ndivyo kanuni hii ya The Equal Odds Rule inavyoelezea jinsi ya kupata mafanikio kwenye jambo lolote. Ili uweze kupata mafanikio, nitakushirikisha mambo matatu ambayo unapaswa uyazingatie na kuyafanyia kazi kwa mujibu wa kanuni hii.
1. Amua unataka kuwa nani.
Hili ni jambo la muhimu sana na la kwanza kabisa unapotaka kupata mafanikio kwenye jambo lolote. Amua unataka kuwa nani au unataka kubobea kwenye kazi gani kwenye maisha yako. Je unataka kuwa mkulima, mfanyabiashara, mwanamichezo, mwajiriwa au uliyejiajiri? Hii itakusaidia kutambua ni kwenye eneo gani utawekeza nguvu zako na akili zako zote ili uweze kupata mafanikio. Kumbuka kuwa unapokuwa umechagua eneo ambalo utabobea kwenye maisha, utaifanya akili yako iongeze ubunifu Zaidi.
2. Amua huduma au bidhaa utakazokuwa unazalisha
Baada ya kuwa umeamua unataka kuwa nani, hatua ya pili ni kuchagua huduma utakazokuwa unatoa au bidhaa ambazo utakuwa unazalisha kwenye eneo ulilochagua. Kwa mfano umeamua kuwa mkulima. Kumbuka kuwa, kilimo ni eneo pana sana, hivyo unaweza kuchagua huduma au bidhaa ambazo utakuwa unazalisha. Kwa mfano, unaweza kuchagua kuzalisha mazao, kusindika, kusafirisha na kadhalika. Kama umejiajiri, chagua bidhaa au huduma ambayo watu watakutambua kuwa unatoa kwa viwango vya juu. Chagua huduma au bidhaa ambazo utakuwa unazalisha, usitake kufanya kila kitu kwani hautafanya kwa ufanisi hivyo utashindwa. Chagua eneo moja au maeneo machache ya kutoa huduma ambayo utajikita zaidi na hivyo kubobea.
3. Toa huduma au zalisha bidhaa mara nyingi na kwa muda mrefu bila kuacha.
Hapa ndio kwenye kiini cha kanuni hii ya The Equal Odds Rule. Katika kanuni hii inasema, mafanikio yatapatikana kama utaamua kufanya jambo moja na kulifuatilia kwa muda mrefu bila kuacha. Unapokuwa umechagua kufanya kazi fulani kwenye maisha yako, fanya kwa muda mrefu bila kuacha, haijalishi utapata vikwazo na kushindwa mara nyingi kiasi gani. Kumbuka kuwa, unapokuwa unarudia kufanya kile kitu mara nyingi na bila kuacha, hata kama utakuwa unapitia changamoto za kushindwa, kushindwa huko kutakupatia uzoefu mkubwa wa kufanikiwa baadaye kama hautakata tamaa.Mara nyingi watu wanashindwa kupata matokeo makubwa kwenye kazi wanazofanya kwa sababu wanafanya kidogo tu halafu wanakata tamaa na kuacha. Kama unataka kufanikiwa, fanya shughuli uliyoichagua kwa muda mrefu bila kukata tamaa.
Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya jinsi ya kupata mafanikio kwa kutumia kanuni hii ya The equal odds rule. Kama una maoni yoyote kuhusiana na mada hii, ninatamani sana uweke maoni yako hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu kwenye Makala ijayo.

Kanuni Ya Mafanikio ‘Choma Meli Zako Zote’

Kanuni ya Mafanikio

Hernan Cortes, kamanda wa Hispania alikuja na Kanuni ya Mafanikio moja inayojulikana kama “Choma Meli Zako Zote'”. Kanuni hii inatokana na kazi aliyopewa ya kwenda kuvamia kisiwa kilichokuwa kinajulikana Kwa jina la Veracruz nchini Mexico mwaka 1519.

Kitu alichokifanya ni kuwa, alichukua makamanda 500 pamoja na Meli 11 za kivita na akawapandisha kwenda kuvamia kwenye kile kisiwa. Alipofika kwenye kile kisiwa, akaamuru makamanda pamoja na mabaharia wote washuke. Baada ya wote kuwa wameshuka, akaagiza Meli Zote zichomwe moto. Wakati Meli zilipokuwa zinaungua, akawauliza makamanda pamoja na mabaharia ” mnaona nini?” wakamjibu “Tunaona moto pamoja na moshi, meli zetu zinaungua”. Akawaambia ” Hivyo basi, hatuna uchaguzi zaidi kwenye vita hii. Ni lazima tuchague moja kati ya mambo haya mawili: Moja, tuamue kufa tushindwe vita, au pili, tupigane tushinde vita ambayo tumeianza.”

Unajua nini kilitokea? Ingawa walikuwa ni wachache ukilinganisha na jeshi ambalo walilikuta pale kisiwani, walishinda ile vita. Hapa ndipo tunapata Kanuni ya kuchoma meli zako zote. Kanuni ya kuchoma meli zako zote inamaanisha, ili uweze kufanikiwa kwenye malengo yako uliyojiwekea, jitahidi kufanya jambo na kulifuatilia kwa kutoa kila kitu ulichonacho. Hata Biblia inasema:
“Lolote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako, kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe” Mhubiri 9:10.
Maana yake ni kuwa, Katika maisha, ili uweze kufanikiwa kwenye jambo lolote ni lazima uwekeze nguvu zako zote na kila kitu ulichonacho. Kutokana na kanuni hii ya ‘choma meli zako zote’, kuna mambo matatu ambayo lazima uyazingatie:

  1. Lazima uamue kuhusu hatma ya maisha yako (Your future)

Lazima uamue kuhusu hatma ya maisha yako (your future). Usiruhusu maisha yako yaendeshwe na hali zinazokuzunguka au na matokeo ambayo yanaambatana na maisha yako. Hivyo, lazima uamue kuhusiana na kazi uliyonayo, kama ni mahusiano yako hauyafurahii, amua leo kuboresha mahusiano yako. Hivyo, haupaswi kuona kuwa, hali yako uliyonayo hauna mamlaka nayo na kwamba hauwezi kufanya kitu chochote kuboresha hali yako. Hivyo, jambo la kwanza kwenye Kanuni hii ya kuchoma meli zako zote ni , amua kuhusiana na kesho yako.

2. Achilia na usahau mambo yaliyopita.

Moja ya vitu ambavyo vinawafanya watu wengi washindwe kufanikiwa Katika maisha yao ni Kwa sababu wameruhusu mambo yao yaliyopita yaendeshwe maisha yao. Pengine kuna mambo ya kukatisha tamaa uliyopitia huko nyuma, pengine kuna maumivu uliyoyapata kutokana na mahusiano yako au uzoefu fulani unaoumiza ulioupitia. Mambo haya yote yamekusababisha mpaka sasa ukijiangalia unajiona kuwa ni mtu ambaye hauwezi kusonga mbele au kuchukua hatua na kufikia kule unakotaka kwenda. Hivyo, jambo la pili, usiruhusu mambo yaliyopita yaendelee kutembea na wewe. Hesabu mambo yaliyopita kuwa yalikuwa ni mambo ya kukufundisha, kukukomaza na kufanya uwe bora zaidi leo.

3. Tumia Kila kitu ulichonacho kufuatilia ndoto ambayo umechagua.

Kama alivyofanya Hernan Cortes ni kwamba, angeachia zile meli, angekuwa ameachia upenyo wa yeye kurudi atakapokuwa amezidiwa na maadui. Lakini Kwa sababu alichoma meli zote, kilichotokea ni kwamba, alihakikisha kwamba hakuna upenyo wa kukimbia. Hivyo, Ili ufanikiwe, toa kila kitu ulichonacho kupigania ndoto zako. Kama uko kwenye biashara, fanya kazi Kwa bidii, tumia nguvu zako, tumia akili zako zote. Kama uko kazini umeajiriwa na ndicho ulichokichagua, hakikisha unatumia kila kitu ulichonacho kufanya ambacho umekichagua. Tatizo la watu wengi ni kwamba, hawaweki kila kitu walichonacho Ili kufanikiwa.
Nimatumaini yangu kuwa umejifunza hizi hatua tatu kwenye kanuni ya mafanikio ya kuchoma meli zako zote kuweza kufikia ndoto zako. Kumbuka kuwa, siku zote hauwezi kufanikiwa kama ulichoamua kufanya haukifanyi Kwa nguvu zako zote. Je, wewe una ndoto gani? Nitafurahi sana kama utaniandikia hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana nami Kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu kwenye makala ijayo.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp