Tabia 8 Zinazozuia Fursa Za Mafanikio Maishani.

Tabia 10 Zinazozuia Fursa Za Mafanikio Maishani

Katika Maisha, ili uweze kufanikiwa ni lazima uwe na uwezo wa kuchangamkia fursa zinazokuja mbele yako. Watu waliofanikiwa ni wale waliotumia kwa usahihi fursa ambazo walizipata. Ninapozungumzia fursa, ninamaanisha jambo lolote ambalo ukilipata litakufanya ufanikiwe Katika maisha. Mfano wa fursa ni kama vile kupata ajira, kupata mtaji wa biashara, kupata wateja kwenye biashara yako na kadhalika. Kimsingi, fursa hazitafutwi bali zinavutiwa. Kuna tabia ambazo mtu akiwa nazo zinamfanya aweze kuvutia fursa nyingi kwake. Lakini pia kuna tabia ambazo ukiwa nazo zinafukuza fursa. Unabaki unalalamika tu kuwa huna bahati ya mafanikio, kumbe mafanikio umeyazuia kutokana na tabia ulizonazo. Katika makala ya leo nitakushirikisha tabia nane zinazozuia fursa za Mafanikio kwenye maisha yako.
Tabia 8 zinazozuia fursa za Mafanikio kwenye maisha yako.

  1. Mawazo hasi (negative thought)
    Mawazo hasi ni tabia inayoweza kuzuia fursa za Mafanikio. Mtu mwenye mawazo hasi ni mtu ambaye haamini kuwa anaweza kufanikiwa. Haamini kuwa vitu vinawezekana. Hawezi kuthubutu kufanya jambo ambalo linaweza kumletea Mafanikio. Hivyo, ukiwa na mawazo hasi watu watashindwa kukushirikisha fursa ambazo zingeweza kukufaa Katika maisha yako wakijua kuwa utazitilia mashaka na hivyo hautathubutu kuzifanyia kazi.
  2. Malalamiko au kutoa lawama.
    Malalamiko ni tabia nyingine ambayo inaweza kuzuia fursa za Mafanikio kwenye maisha yako. Mtu mwenye malalamiko ni mtu ambaye haridhiki na chochote atakachopata. Ni mtu ambaye analalamikia watu changamoto alizonazo badala ya kutafuta njia ya kuzitatua. Kimsingi, watu hawapendi mtu mwenye kulalamika muda wote kwani huwa wanahisi kuwa analalamika Ili awatwike matatizo yake. Mtu mwenye malalamiko hata kama akipata fursa, hataridhika bali ataitafutia kasoro na kulalamika. Hivyo ukiwa mtu mlalamishi, watu hawatakushirikisha fursa, kwani wanafahamu kuwa hautaridhika nayo.
  3. Kutokujali muda na kutokuwa na ratiba
    Kutokujali muda ni tabia nyingine ambayo inaweza kuzuia fursa za mafanikio kwenye maisha yako. Watu wanajali sana muda, hivyo wakiona kuwa wewe haujali muda, watakukwepa na hawatakushirikisha fursa. Jitahidi kujali sana muda Kwa kuwa na ratiba Katika maisha yako. Usikubali muda Wako kupotea bila sababu ya msingi kwani muda ni rasilimali ambayo ikipotea hauwezi kuirudisha.
  4. Kutokuwa mwaminifu
    Kuna msemo wa kiswahili unaosema ‘uaminifu ni mtaji’. Ukiwa mwaminifu Katika mambo Yako yote, watu watakuamini na watatamani kufanya na wewe kazi. Kama umeajiriwa fanya kazi zako Kwa uaminifu, watu watakupenda na utapata fursa nyingine nyingi kupitia uaminifu Wako. Kama umejiajiri, kuwa mwaminifu kwenye kazi unazoletewa. Zifanye Kwa ubora wa hali ya juu, watu watakupenda na utapata fursa nyingi zaidi. Hivyo, kutokuwa mwaminifu ni tabia inayoweza kuzuia fursa za Mafanikio kwenye maisha yako.
  5. Kudharau mwanzo mdogo
    Watu wengi wameshindwa kuanzisha biashara au kazi zao Kwa kuhofia kuanzia na mwanzo mdogo. Ili uweze kufanikiwa. Kubali kuanzia chini Ili upate msingi wa kukupeleka kwenye mafanikio unayoyahitaji. Ukianzia chini na ukafanya Kwa uaminifu, unajiwekea nafasi ya kupata fursa kubwa zaidi.
  6. Kushindwa kujifunza kwa haraka
    Katika Dunia ya leo mambo yanabadilika Kwa haraka sana. Hii ni kuanzia mfumo wa maisha, jinsi tunavyofanya kazi, jinsi tunavyofanya biashara na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Hivyo Ili uweze kuendana na mabadiliko haya, unapaswa kuwa mwepesi kujifunza. Ukishindwa kujifunza kwa haraka utaachwa nyuma na utakosa fursa za mafanikio kwenye maisha yako. Kama unafanya biashara, jifunze Kila siku Ili uboreshe biashara yako. Kama unafanya kazi usiache kuboresha ujuzi Wako ili uweze kutoa huduma Bora zaidi. Kumbuka kuwa unapotoa huduma bora, unajiweka kwenye nafasi ya kupata fursa nyingi zaidi za mafanikio.
  7. Kujifanya mjuaji
    Ujuaji ni tabia mbaya sana inayoweza kukukosesha fursa. Mtu mjuaji ni mtu ambaye anahisi kuwa anajua Kila kitu hivyo hahitaji kujifunza zaidi. Ni mtu ambaye hashauriki. Watu hawapendi mtu mjuaji hivyo hawawezi kumshirikisha fursa kwani wanajua kuwa ataharibu.
  8. Kuwa na hasira za haraka Mtu mwenye hasira za haraka ni mtu asiyetabirika. Anaweza kukasirika muda wote akafanya maamuzi ya ajabu ambayo yanaweza kuleta hasira kubwa kazini au kwenye biashara. Hivyo, ukiwa na hasira za haraka, watu watashindwa kukushirikisha fursa ambazo zingeweza kukufaa Katika maisha yako. Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yatakusaidia kwenye safari yako ya mafanikio. Kama una swali au maoni yoyote kuhusiana na mada hii usisite kuandika hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752081669. Asante na karibu kwenye makala ijayo.

Hatua 4 Za Kupitia Kabla Wazo Lako Halijafanikiwa

Hatua 4 Za Kupitia Kabla Wazo Lako Halijafanikiwa

Kwenye maisha, ili uweze kuweka malengo ambayo yatakupa matokeo makubwa katika maisha yako ni lazima utaanzia katika wazo. Mambo yote makubwa unayoyaona hapa duniani yalianzia kwenye wazo. Mtu alikaa akawaza na akaamua kuchukua hatua. Ili wazo liweze kufanikiwa, ni lazima lipitie mchakato wa hatua mbalimbali. Watu wengi huwa wanaishia njiani kwenye mchakato huo na ndio maana mawazo yao huishia njiani na hivyo kushindwa kufikia malengo waliyokusudia. Katika Makala ya leo nitakushirikisha na kukupitisha kwenye hatua hizi nne muhimu ambazo ni lazima upitie kabla wazo lako halijafanikiwa.
Hatua 4 ambazo utapitia kabla wazo lako halijafanikiwa.
1. Conception stage

Katika hatua hii, unakuwa umepata wazo ambalo unafikiria linaweza kukutoa kimaisha. Ni hatua ambayo unakuwa na hamasa kubwa ya kufanya. Katika hatua hii hauoni vikwazo vyovyote ambavyo vinaweza kusababisha wazo lako lisiweze kufanikiwa. Unakuwa na hamu ya kumshirikisha kila mtu wazo lako. Hii ni hatua ya mwanzo kabisa.
2. Rejection stage
Baada ya conception stage, hatua inayofuata ni rejection stage. Katika hatua hii, wazo lako linaanza kupata upinzani. Unaanza kupata ukosoaji kutoka kwa marafiki, ndugu na jamaa wa karibu yako ambao mwanzoni uliamini kuwa wanaweza kukusaidia. Katika hatua hii watu wako wa karibu wanageuka na kuwa wakosoaji wakubwa. Ni hatua ambayo watu wanakuwa wanakueleza mapungufu tu ya wazo ulilowashirikisha na hawakupi mazuri ambayo yapo kwenye wazo lako. Ili uweze kuvuka kwenye hatua hii ni lazima uwe na uvumilivu wa kukabiliana na wakosoaji wote na usonge mbele ili uweze kupata mafanikio.
3. Implementation stage
Baada ya kuwa umevuka vikwazo vya wakosoaji wote, hatua inayofuata kuelekea mafanikio ya wazo lako ni implementation stage. Hapa unaanza kufanya kile ambacho ulikuwa umekipanga. Katika hatua hii unapaswa kufanya kwa bidii bila kuacha. Watu wengi wanashindwa kufanikiwa kwa sababu walipofikia kwenye hatua hii walifanya kidogo halafu wakaacha na kuhamia kwenye wazo lingine jipya. Kwa lugha nyingine wanaacha kufanyia kazi mawazo yao wanaanzisha wazo jipya na hivyo kurudi kwenye hatua ya mwanzo ambayo ni conception stage. Ili uweze kufanikiwa, fanyia kazi wazo lako bila kuacha na kwa muda mrefu. Komaa na wazo lako na mafanikio utayaona.
4. Celebration stage
Hatua ya nne ni celebration stage. Hii ni hatua ambayo, mafanikio yameanza kuonekana. Hata wale waliokuwa wanakukosoa na kukupinga wanapoona umeanza kufanikiwa wanarudi kuungana na wewe na kujisifia kuwa na wao walikuwa ni sehemu ya mafanikio yako. Ni hatua nzuri ambayo unatakiwa kuendelea kufanyia kazi wazo lako.
Hivyo, mafanikio yoyote huwa hayaji kirahisi. Kila aliyefanikiwa alianza na wazo. Baada ya kuwa amepata wazo na kuanza kulifanyia kazi, alipitia vikwazo vingi vya wakosoaji na hatimaye baada ya kushinda vikwazo hivyo, mafanikio yalipatikana. Hivyo, kama una wazo na unafikiria kuwa linaweza kukutoa kimaisha, usihofu kufanya. Utapitia katika hatua hizi nilizozizungumzia kwenye somo hili, ukiweza kuvuka hatua tatu za mwanzo, mafanikio utayaona.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakusaidia kushinda vikwazo vyote ili uweze kufanikiwa. Kama una swali au maoni yoyote, usisite kuandika hapo chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu kwenye Makala zinazofuata.

Aina 4 Za Elimu Unazohitaji Ili Uweze Kufanikiwa.

Aina 4 za Elimu Unazohitaji Ili uweze Kufanikiwa

Ili uweze kufanikiwa katika maisha unahitajika kuwa na aina nyingi mbalimbali za elimu na maarifa. Maarifa hayo unapokuwa umejifunza kwa pamoja na kuyafanyia kazi yatakusaidia kutimiza malengo uliyojiwekea. Katika mfumo wetu wa elimu tumekuwa tukijifunza aina mbili tu za elimu ambazo kwa uhalisia hazitoshi kutufanya tufanikiwe kwa viwango vya juu. Aina hizo za elimu ni elimu ya kujifunza kusoma, kuandika na kuhesabu (scholastic education) na elimu inayofundisha ujuzi (professional) education. Aina hizi za elimu ni muhimu lakini bila kuongeza na aina nyingine mbili za elimu ambazo nitakushirikisha katika Makala hii hazitoshi kukufanya uweze kufanikiwa. Hivyo, katika Makala ya leo nitakushirikisha aina nne za elimu unazohitaji ili uweze kufanikiwa.
Zifahamu aina 4 za elimu unazohitaji ili uweze kufanikiwa.
Aina hizi za elimu zimegawanyika katika makundi makuu mawili. Kundi la kwanza ni
1. elimu inayofundishwa darasani.
2. Elimu ambayo haifundishwi darasani.
1. Elimu inayofundiswa darasani.
Katika kundi hili la elimu kuna elimu za aina mbili ambazo ni:
a. Elimu ya kujua kusoma kuandika na kuhesabu (scholastic education).
Hii ni elimu inayokusaidia kufahamu kujua kusoma, kuandika na kuhesabu. Katika elimu hii, mtu anasoma elimu kuondoa ujinga. Hivyo mtu anaposema kuwa amesoma, huwa anamaanisha aina hii ya elimu. Aina hii ya elimu pekee haiwezi kukufanya uweze kufanikiwa.
b. Elimu inayofundisha utaalamu (professional education)
Hii ni elimu inayofundishwa kwenye vyuo mbalimbali. Kazi ya hii elimu ni kufundisha utaalamu kwenye fani mbalimbali. Elimu hii ndiyo inayozalisha wataalamu kama vile madaktari, wahandisi, walimu na kadhalika. Hii ni elimu ambayo inazalisha wataalamu ambao wanaingiza kipato kwa kuuza utaalamu wao. Wanaweza kuwa wameajiriwa au kujiajiri. Hivyo ili waweze kutengeneza kipato, ni lazima wauze utaalamu wao. Aina hii ya elimu itakuwezesha kuwa na kipato cha kati (middle income). Haiwezi kukufanya uweze kufanikiwa kwa kiwango cha juu na kuwa na uhuru wa kifedha. Hii ni kwa sababu haiwezi kukufanya uwe na kipato endelevu (passive income).
2. Elimu ambayo haifundishwi darasani.
Katika kundi hili la elimu kuna aina mbili za elimu ambazo ni:
a. Elimu ya msingi kuhusu fedha (financial education)
Hii ni elimu ya muhimu sana kwani inakufundisha jinsi kutengeneza kipato chako, jinsi ya kutumia kipato chako na ni jinsi gani utawekeza pesa zako ili ziweze kuongezeka thamani na hivyo kukufanya utajirike na kuwa na uhuru wa kifedha (financial freedom), jinsi ya kuweka bajeti na kadhalika. Elimu hii ndiyo inawatofautisha watu matajiri na masikini. Elimu hii haifundishwi darasani. Unaipata kupitia kusoma vitabu mbalimbali. Hivyo wekeza sana kwenye aina hii ya elimu ili uweze kufanikiwa.
b. Elimu ya maendeleo binafsi (self development)
Hii ni elimu inayokusaidia kuweza kutumia vipawa, vipaji na uwezo ulionao ili uweze kufanikiwa. Aina hii ya elimu ni muhimu sana kwani unapofahamu jinsi ya kutumia vipawa na vipaji ulivyonavyo utaweza kufanikiwa kwa viwango vya juu sana. Ndiyo maana kuna watu ambao hawakuwahi kuingia darasani lakini wana mafanikio makubwa sana katika maisha yao. Elimu hii pia unaipata kupitia kusoma vitabu. Hivyo wekeza muda wako kusoma vitabu ili uweze kufanikiwa katika maisha.
Swali la msingi ni hili, je elimu mbili za kwanza sio muhimu?
Jibu ni hapana. Elimu zote ni muhimu, hivyo ili uweze kufanikiwa, kama ukiwa na elimu ya darasani halafu ukaongezea kwenye aina hizi mbili za elimu ambazo hazifundishwi darasani basi mafanikio yako yatakuwa makubwa sana. Hivyo basi kama umebahatika kusoma, basi wekeza pia na kwenye aina hizi mbili za elimu ili uweze kufanikiwa. Lakini pia, kama haukubahatika kusoma, wekeza kwenye aina hizi mbili za elimu ambazo hazifundishwi darasani, utafanikiwa kwani kuna watu ambao hawakubahatika kuingia darasani, lakini kwa sasa ni matajiri wakubwa.
Kwa leo niishie hapo, nimatumaini yangu umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakufanya uweze kufanikiwa katika maisha yako. Kama una maoni au swali lolote usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazofuata.

Mbinu 2 Za Kukusaidia Kutunza Muda Wako.

Mbinu 2 Za Kukusaidia Kutunza Muda Wako.

Katika maisha ili uweze kufanikiwa, unahitaji rasilimali. Kati ya rasilimali zote ambazo Mungu ametubariki, Muda ndiyo rasilimali ya muhimu sana kuliko rasilimali zote na inapaswa kutunzwa kwa umakini wa hali ya juu. Hii ni kwa sababu, muda ukipotea hauwezi kuurudishwa (non- renewable resource). Muda ni wa thamani kuliko pesa kwani ukipoteza pesa, unaweza kutafuta nyingine ukapata na maisha yakaendelea. Lakini ukipoteza muda hauwezi kuurudisha. Hivyo, ili uweze kufanikiwa ni lazima uweze kufahamu jinsi ya kutunza muda wako. Katika Makala ya leo, nitakushirikisha mbinu mbili ambazo zitakusaidia kutunza muda wako ili uweze kufanikiwa.
Mbinu 2 za kukusaidia kutunza muda wako uweze kufanikiwa.
1. Panga vitu vyako katika mpangilio maalumu (systematic arrangement).
Jambo la kwanza kabisa ambalo litakusaidia kutunza muda wako ni kupanga vitu vyako katika mpangilio maalumu. Kama ni nyumbani weka mpangilio maalumu unaoonesha vitu vyako vitakaaje. Kwa mfano, nguo za kazini mahali zinapokaa, funguo za nyumba, ufunguo wa gari, vitabu na kadhalika. Mpangilio huu utakusaidia kufahamu kila kitu mahali kinapokuwa na hivyo kukusaidia kuokoa muda ambao ungeweza kuupoteza kwa kutafuta vitu. Kama ni ofisini, fanya mpangilio mzuri wa aina za faili. Mfano weka sections mbalimbali zinazotofautisha aina ya faili zilizopo ofisini kwako. Mfano unaweza kutofautisha aina za faili kama vile: Faili za barua, faili za nyaraka, faili za mikataba, faili za mambo ya fedha na kadhalika. Hii itakusaidia kutumia muda mfupi sana kutafuta faili zako. Pia unaweza kuweka mpangilio wa vitu vingine vilivyopo ofisini kwako kama vile vitabu, daftari, peni, mihuri na kadhalika. Kwa kufanya hivyo, utaonkoa muda mwingi sana ambao utautumia kufanya shughuli zingine.
2. Panga vitu vyako siku moja kabla.
Jambo la pili ambalo unaweza kulitumia kutunza muda wako ni kupanga vitu vyako siku moja kabla. Hapa kama unaenda kazini, unaweza kupanga nguo ambazo utavaa na unazitenga kabisa. Pia unatenga vitu vingine ambavyo utakwenda navyo kazini, kama vile vitabu, notebook, laptop na kadhalika. Hii itakusaidia unapoamka kesho, usipoteze muda muda kuanza kutafuta vitu ambavyo unapaswa kuenda navyo kazini. Kwa kufanya hivyo, utaokoa muda mwingi sana ambao utautumia kwa kuwahi kwenye eneo lako la kazi na hivyo kuongeza ubora wa kazi yako.
Kwa leo niishie hapo, nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakusaidia kutunza muda wako vizuri ili uweze kufanikiwa kwenye maisha yako. Kumbuka kuwa muda ndio rasilimali ambayo ikipotea hauwezi kuirudisha. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuandika hapo chini. Pia kama una swali lolote kuhusiana na mada ya leo, usisite kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante sana na karibu kwenye Makala zinazokuja.

Rasilimali 3 Unazohitaji Kutimiza Malengo Yako

Rasilimali 3 Muhimu Unazohitaji Uweze Kutimiza Malengo Yako

Watu wengi huwa wanaweka malengo makubwa katika maisha yao lakini wanaofanikiwa kutimiza malengo yao ni wachache sana. Hata wewe unaweza kujiuliza, mwaka uliopita ulikuwa umeweka malengo, je umeweza kutimiza malengo yako kwa kiwango gani? Jibu unalo. Lakini pia mwaka huu inawezekana una malengo ambayo tayari umeyaweka. Ili uweze kutimiza malengo yako, kuna rasilimali ambazo lazima uwekeze. Kila lengo unalopanga litahitaji rasilimali hizi. Katika Makala ya leo nitakushirikisha rasilimali tatu muhimu unazohitajika kuwa nazo ili uweze kutimiza malengo yako.
Rasilimali 3 muhimu unazohitaji uweze kutimiza malengo yako
1. Muda

Muda ndio rasilimali ya kwanza na muhimu sana katika maisha ambayo unahitaji kuweza kufikia malengo yako. Ni rasilimali ambayo inapaswa kulindwa na kutumika kwa uangalifu mkubwa sana. Hii ni kwa sababu muda ukipotea hauwezi kurudishwa (non-renewable resource). Hivyo ili uweze kutimiza malengo yako unapaswa kutumia vizuri muda wako kwenye kile tu ulichojiwekea malengo. Usiruhusu muda wako kupote ovyo. Kumbuka kuwa unaweza kupotesa pesa na ukatafuta nyingine ukaipata. Lakini hauwezi kuurudisha muda uliopotea. Mara nyingi huwa ninaona watu wapo kijiweni, na ukiwasalimia wanasema tupo hapa tunapoteza muda! Wanapoteza rasilimali ya thamani ambayo hawawezi kuirudisha. Hivyo, muda ni rasilimali ya thamani sana kwenye mafanikio yako.
2. Watu
Rasilimali nyingine ambayo utahitaji kuweza kufanikisha malengo yako ni watu. Utahitaji watu wa kukushika mkono, utahitaji watu wa kukusaidia kwenye kazi yako na utahitaji watu kwenye kila unachokifanya.
3. Fedha
Fedha pia ni rasilimali nyingine ambayo ni ya muhimu ili uweze kutimiza malengo yako. Fedha inahitajika katika kuendesha mradi au biashara uliyoianzisha.
Swali la msingi ni hili, kwa nini watu wengi huwa wanashindwa kutimiza malengo yao?
Jibu ni kuwa, watu wengi wanashindwa kutimiza malengo yao kwa sababu huwa wanatapanya rasilimali zao kwenye malengo mengi. Unakuta mtu ameanza biashara ya duka, mara akasikia kilimo cha matikiti kinalipa akaamua kulima matikiti, baadaye akasikia kuwa biashara ya mtandao inalipa akaamua pia kufanya biashara hiyo. Kumbuka kuwa kila lengo linahitaji rasilimali hizi muhimu tatu kama nilivyozielezea hapo juu yaani muda, watu na fedha. Hivyo ukiwa na malengo mengi utashindwa kufanikiwa kwa sababu utakuwa unarashia kwenye kila lengo. Hivyo, ili uweze kufanikiwa kutimiza malengo yako, ni lazima uwekeze nguvu kwenye lengo moja. Nguvu zako zote na rasilimali zako zote ni sharti uziwekeze kwenye lengo moja, hapo mafanikio utayaona. Kumbuka kuwa mafanikio hayaji kwa kufanya vitu vingi, bali yanakuja kwa kufanya kitu kimoja kwa weredi wa hali ya juu. Weredi huu unapatikana pale tu ambapo utakuwa umewekeza rasilimali zako zote kwenye lengo lako yaani pesa zako zote, muda wako wote na watu wa kukusaidia kufikia lengo lako.
Kuna neno la kingereza linalosema FOCUS. Maana ya neno focus ni kuzingatia na kufanya kile ulichokipanga na kukataa kila vishawishi ambavyo vitakuhamisha kwenye kile unachokifanya. Hivyo ili uweze kutimiza malengo yako ni lazima uwe na Focus, fanya kitu kimoja na usiruhusu upepo wowote ambao unaweza kuja kutaka kukuhamisha kwenye kile unachokifanya.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ambayo yatakusaidia kuweza kufanikisha malengo yako. Kama una maoni au swali, usisite kuandika hapo chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu kwenye Makala zinazofuata.

Jinsi Ya Kutambua Kusudi La Maisha Yako

Jinsi kugundua Kusudi la Maisha Yako

Katika maisha, Mungu amemuumba kila mwanadamu na kumleta duniani kwa kusudi maalumu. Hivyo Mungu amempatia kila mwanadamu uwezo mkubwa ndani yake, kila mtu kwa aina yake ili aweze kutimiza kusudi lake la kuwa duniani. Hata wewe, Mungu ameruhusu uwepo duniani kwa kusudi maalumu. Ukigundua kusudi la maisha yako, utaweza kufanya mambo makubwa sana. Kwa bahati mbaya sana, watu wengi wanazaliwa mpaka wanakufa bila kutambua kusudi la maisha yao na hivyo kushindwa kutumia uwezo mkubwa ambao Mungu ameuweka ndani yao ambao kama wangeutumia wangeweza kufanya mambo makubwa sana Duniani na wangekuwa mbaraka mkubwa kwa watu wengine. Katika Makala ya leo nitakushirikisha jinsi ya kutambua kusudi la maisha yako ili uweze kufanikiwa kufanya mambo makubwa.
Jinsi ya kutambua kusudi la maisha yako uweze kufanikiwa.
1. Chunguza nguvu (umahili) wako.
Ili uweze kugundua kusudi la maisha yako, njia ya kwanza ni kuchunguza kwenye uwezo wako wa ndani. Hebu jichunguze, ni vitu gani ambavyo ukivifanya, unavifanya kwa ubora wa hali ya juu. Kwa mfano inawezekana ukawa una uwezo wa kuongea vizuri mbele za watu, kuimba, kucheza mpira, kuandika na kadhalika. Kutambua uwezo ulio nao ni hatua kubwa sana ya kutambua kusudi ambalo Mungu amekuleta Duniani. Hii itakusaidia kuwekeza nguvu kubwa kwenye eneo ambalo una umahili wa kutosha na kukufanya uweze kufanya mambo makubwa na ya kushangaza. Kumbuka kuwa kila uwezo au umahili ulionao una uwezo kabisa wa kuubadilisha na ukawa ni chanzo cha kuuingizia kipato.
2. Ongea na watu wa karibu wakuambie uwezo wako upo kwenye maeneo gani.
Njia nyingine ya kutambua kusudi la maisha yako ni kuongea na watu wako wa karibu. Hawa wanaweza kuwa ni wale watu unaowaamini kuwa watakuambia ukweli wa jinsi ulivyo. Mfano: marafiki wako wa karibu, mke au mme wako, wazazi na kadhalika. Waulize maswali wakuambie ni kitu gani unapokuwa unakifanya, unaonekana umekifanya vizuri sana na watu huwa wanakifurahia. Kusanya majibu ambayo watakuwa wamekupatia. Majibu uliyoyapata, yatakusaidia kugundua uwezo wako na hivyo kuweza kufahamu kusudi la maisha yako.
3. Fikiria ni vitu gani ulivyowahi kuvifanya na watu wakavifurahia (Past experience).
Njia nyingine ambayo unaweza kugundua kusudi la maisha yako ni kwa kuangalia uzoefu wako wa nyuma (past experience). Hapa unaangalia mambo yote ambayo uliwahi kuyafanya na ukayafurahia na pia watu wakakupongeza kuwa umefanya vizuri. Mfano, inawezekana kuna siku uliwahi kusimama mbele ya watu na ukaongea vizuri, baada ya kumaliza kuongea watu wakakupongeza sana kuwa umeongea vizuri sana. Hii ni dalili nzuri kuwa una uwezo mkubwa wa kuongea mbele ya watu kwa sababu si kila mtu anaweza kusimama na akaongea mbele za watu vizuri. Huo ulikuwa ni mfano tu, sasa unaweza kufikiria mambo yote uliyowahi kuyafanya na watu wakakupongeza.
Baada ya kutumia njia nilizokuelezea hapo juu, sasa unaweza kujua ni mambo gani una uwezo kubwa wa kuyafanya. Kwa kuangalia mambo hayo, sasa unaweza kufikiria ni kazi au shughuli gani unaweza kuifanya ambayo inahusiana na uwezo ulio nao. Kazi utakayoifanya ndilo litakuwa ni kusudi lako la maisha kwa sababu itakuwa ni kazi ambayo utakuwa unaifurahia na ni kazi ambayo inakuwezesha kutumia uwezo wote ambao Mungu ameuweka ndani yako. Hivyo, utafanya kazi kwa viwango vya juu na Kufanikiwa sana.
Kwa leo niishie hapo. Kama una maoni yoyote kuhusiana na mada ya leo, usisite kuweka maoni au swali lolote, usisite kuweka hapo chini. Pia kama unahitaji ushauri wowote, usisite kuwasiliana name moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazokuja.

Jinsi Ya Kutengeneza Kipato Kinachokua Kila Siku

Kutengeneza Kipato endelevu Kinachokua Kila Siku

Mfumo wetu wa elimu huwa unatufundisha aina mbili za elimu: Aina ya kwanza ni elimu ya kujua kusoma, kuandika na kuhesabu (scholastic education). Hii ni elimu ambayo inakuwezesha kujua jinsi ya kusoma, kuandika na kuhesabu. Aina ya pili ya elimu ni elimu ya ujuzi (professional education). Aina hii ya elimu ndiyo inayozalisha wataalamu mbalimbali kama vile madaktari, walimu, wahandishi na kadhalika. Kuna aina ya tatu ya elimu ambayo haifundishwi darasani, nayo ni elimu ya msingi kuhusu fedha (financial education). Hii ni elimu inayokuwezesha kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato, jinsi ya kutumia pesa yako na jinsi ya kuwekeza pesa yako. Katika Makala ya leo nitakushirikisha aina hii ya tatu ya elimu na nitazungumzia jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku (Passive income).
Jinsi ya kutengeneza kipato endelevu kinachokua kila siku.
Kwanza kabisa, ili uweze kufahamu jinsi ya kutengeneza kipato ambacho kitakuwa kinakuwa kila siku na endelevu, ni lazima nianze kwanza kuelezea aina ya vipato. Watu wote wanaofanya kazi duniani na kupata kipato, vipato vyao vimegawanyika sehemu kuu tatu: aina hizi za vipato ni active income, portfolio income na passive income. Nitaelezea kila aina ya vipato.
Aina za vipato:
1. Active income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inakutaka wewe uwe mahali pa kazi, ufanye kazi ndio ulipwe. Hii inajumuisha watu walioajiriwa ambao wanalipwa baada ya kuwa wamefanya kazi. Maana yake ni kuwa, kama hakufanya kazi hawawezi kulipwa. Pia inajumuisha watu waliojiajiri ambao ni lazima waende kwenye maeneo yao ya kazi, wafanye kazi ndio waweze kupata kipato. Kwa lugha rahisi ni kuwa, active income ni aina ya kipato ambayo unalipwa tu pale unapokuwa umefanya kazi. Kama hukufanya kazi huwezi kulipwa.
2. Portfolio income
Hii ni aina ya kipato inayopatikana mtu anapoamua kuwekeza pesa yake kwenye maeneo ambayo itaongezeka thamani kama vile kuwekeza kwenye kununua hisa, kuwekeza kwenye mifuko ya pamoja na kuwekeza kwenye hatifungani. Kwa ligha rahisi ni kuwa, unawekeza pesa yako kwenye maeneo ambayo baadaye utapata faida.
3. Passive income.
Hii ni aina ya kipato ambayo inapatikana bila ya ulazima wa wewe kuwepo mahali pa kazi. Biashara yako inakuwa inajiendesha yenyewe bila ya wewe kufanya kazi. Kwa mfano: unapokuwa umeamua kuandika kitabu na ukamaliza, basi kitabu hicho utakiuza maisha yako yote. Kazi kubwa utaifanya mwanzoni tu wakati wa kuandika. Lakini baada tu ya kumaliza kuandika kazi yako itakuwa ni kuuza tu. Hivyo kitabu chako kinakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato kikubwa na endelevu (passive income). Mfano mwingine ni unapokuwa umeandaa kozi yako na ukaiweka mtandaoni. Kazi yako kubwa itakuwa tu mwanzoni wakati wa kuandaa kozi yako lakini ukishamaliza, basi inakuwa ni chanzo cha kukupatia kipato endelevu bila ya ulazima wa wewe kufanya kazi nyingine ya ziada. Lakini pia unaweza kuandaa video zako za mafunzo na ukaziweka YouTube. Baada ya kuwa umepata wafuasi wa kutosha na video zako zikawa na watazamaji wengi, basi unaweza kutengeneza kipato endelevu (passive income) kwani YouTube itakuwa inakulipa kupitia matangazo yake ambayo itayaweka kwenye video zako.
Kama njia yako ya kutengeneza kipato ni ile ya kwanza (active income) basi unaweza kuifanya lakini uwe na malengo ya kuandaa njia nyingine ambayo itakusaidia kupata kipato endelevu ambacho hakitakulazimu kufanya kazi (passive income). Hii ni kwa sababu, kadiri unavyoendelea kufanya kazi, nguvu zako zinaendelea kupungua hivyo ni muhimu kuwa na njia ya kutengeneza kipato ambayo hakitakulazimu kufanya kazi.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha ya jinsi ya kutengeneza kipato kinachokua kila siku. Kama una maoni au swali, usisite kuweka maoni yako hapo chini. Pia kwa ushauri wowote usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu katika Makala zinazokuja.

Mambo 4 Ya Kufanya Unapoamka Asubuhi

Mambo 4 ya kufanya unapoamka asubuhi

Jinsi unavyoianza siku yako kila unapoamka asubuhi ina mchango mkubwa sana katika mafanikio yako. Watu wengi huwa wanakosea jinsi wanavyoanza siku asubuhi na hivyo kushindwa kupata mafanikio. Kisaikolojia, ukishindwa kuanza siku yako vizuri, utakuwa umeharibu siku nzima kwani utashindwa kupata matokeo makubwa uliyokuwa unayakusudia. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo manne muhimu unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi ili uweze kupata mafanikio makubwa katika maisha yako.
Mambo 4 muhimu ya kufanya kila unapoamka asubuhi.
1. Anza na Mungu.
Mungu ndiye muweza wa kila kitu. Ndiye anayetupa uhai, uwezo na nguvu za kufanya kazi zetu. Hivyo jambo la kwanza kabisa, uanpoamka asubuhi, anza na maombi. Muombe Mungu akusaidie katika kazi zako zote unazoenda kuzifanya. Hii itakusaidia kujenga mahusiano mazuri na Mungu na hivyo kukuwezesha kufanikiwa kwenye kazi zako. Pia unapoanza na Mungu, unapata utulivu wa akili kwa kuwa utakuwa umekabidhi mipango, na kazi zako zote kwake.
2. Angalia malengo yako ya muda mrefu.
Jambo la pili la kufanya kila unapoamka asubuhi ni kupitia malengo yako ya muda mrefu. Hapa utaangalia kama kazi unazoenda kuzifanya ndani ya siku ya leo zinatimiza malengo yako ya muda mrefu au la. Hii itakusaidia kutokuhama kwenye malengo yako uliyojiwekea ya muda mrefu. Kumbuka kuwa, ili uweze kufanikiwa ni lazima uwe na malengo makubwa uliyojiwekea. Kwa mfano , kwa mwaka huu umeweka malengo ya kuandika kitabu. Hivyo, unapoanza siku yako angalia kazi unazoenda kuzifanya zisikuhamishe kwenye lengo lako la muda mrefu.
3. Soma, angalia au sikiliza kitu kinachokutia nguvu na kukupa hamasa.
Kila unapoamka asubuhi, jambo la tatu unalopaswa kulifanya ni kusoma kitabu ambacho kitakupa hamasa (inspirational book). Lakini pia kama huna kitabu unaweza kuangalia video ambayo ina mada zinazohamasisha. Hii itakupa nguvu na hamasa kufanya kazi kwa bidi kutimiza malengo yako. Usianze siku yako kwa kuangalia udaku au kuangalia taarifa. Kumbuka kuwa unapoangalia taarifa, utapata taarifa nyingi ambazo nyingine ni za kusikitisha. Ukifanya hivyo utakuwa umeharibu hamasa ya kufanya kazi kwa siku nzima. Kumbuka kuwa jinsi unavyoianza siku yako asubuhi, ndio itaashiria jinsi siku nzima itakavyokuwa. Kama utaichosha akili yako kwa kusoma udaku asubuhi, utakuwa umeharibu utendaji wako wa siku nzima.
4.Hakikisha unaorodhesha vitu ambavyo utavifanya kwa siku nzima.
Baada ya kuwa umefanya mambo matatu kama nilivyoelezea hapo juu, jambo linalofuata ni kuorodhesha mambo yote ambayo utayafanya kwa siku nzima. Kuna faida kubwa sana kuorodhesha mambo unayoenda kuyafanya. Faida ya kwanza ni kutokupoteza muda kwani utakuwa unafahamu mambo unayopaswa kuyafanya, lipi linaanza na lipi linafuata. Faida ya pili ni kuhakikisha kuwa unafanya mambo yale tu ambayo umeyapanga yafanyike kwa siku hiyo hivyo kukusaidika kutimiza malengo yako ya muda mrefu uliyojiwekea.
Kwa leo niishie hapo. Ni matumaini yangu umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo unayopaswa kuyafanya kila unapoamka asubuhi. Jambo la msingi ni kuchukua hatua. Kumbuka kuwa, mafanikio makubwa yanajengwa na vitu vidogo vidogo tunavyovifanya kila siku. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena katika Makala zinazokuja.

Mambo 3 Wanayofanya Watu Waliofanikiwa.

Mambo 3 muhimu wanayofanya watu Waliofanikiwa Duniani.

Katika kufanya utafiti na kusoma kwangu vitabu nilitamani kujifunza jinsi watu waliofanikiwa na matajiri duniani wanavyoishi. Lengo la kusoma kwangu vitabu lilikuwa ni kujua siri ya maisha yao na kufahamu vitu vya tofauti wanavyofanya na hivyo kuweza kujitofautisha na watu wa kawaida. Miongoni mwa watu ambao niliowahi kusoma vitabu vyao ni aliyekuwa Rais wa Marekani, Donard Trump pamoja na matajiri wengine wengi. Katika kusoma kwangu, niligundua kuna mambo matatu muhimu ambayo watu waliofanikiwa huwa wanafanya. Katika Makala ya leo nitakushirikisha mambo matatu muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa Duniani ambayo hata wewe unaweza kuyafanya ili uweze kufanikiwa.
Mambo 3 muhimu wanayofanya watu waliofanikiwa duniani.
1. Ni wasomaji wazuri sana wa vitabu.
Jambo la kwanza kabisa ambalo watu waliofanikiwa hufanya ni wasomaji wazuri sana wa vitabu. Ukifuatilia matajiri wote wakubwa wa dunia kama vile Donard Trump, hutumia muda wao mwingi katika kuongeza maarifa kupitia usomaji wa vitabu. Lengo kubwa la usomaji wao wa vitabu ni kuongeza ujuzi na maarifa kuhusiana na biashara pamoja na shughuli zao zingine wanazozifanya. Hivyo, hata wewe kama unataka kufanikiwa kwenye malengo yako, wekeza muda wako katika kujenga ujuzi wako kwenye shughuli unayofanya ili uweze kupata matokeo makubwa. Akili ya mwanadamu ni kama panga la kukatia ambalo linatakiwa kunolewa ili liweze kukata kwa urahisi. Tunanoa akili zetu kwa kujifunza maarifa mapya kila siku kupitia usomaji wa vitabu. Hivyo, kama unataka kufanikiwa, panga ratiba ya kusoma vitabu kila siku.
2. Hawaishi maisha ya kujionyesha ili kuridhisha watu.
Changamoto kubwa iliyopo kwa watu wengi ni kuishi maisha yasiyokuwa na uhalisia. Unakuta mtu anatamani kuishi maisha ya juu kuliko kipato chake. Anatamani awe na gari, awe na nguo za gharama kubwa, apange kwenye nyumba ya bei ya juu wakati kipato chake hakiwezi kuhimili gharama hizo. Wanaishi maisha yao ili kuwaridhisha watu. Matokeo yake ni kuingia kwenye madeni na kupata stress za maisha. Watu waliofankiwa hawafanyi hivyo. Wanaishi maisha yao kulingana na kipato chao. Hawaishi kuwaridhisha watu. Hivyo, ili uweze kufanikiwa, unapaswa kuwa na bajeti na matumizi yako yasizidi kipato chako. Ishi maisha yako na siyo kuishi ukishindana na watu.
3. Matumizi yao makubwa ya pesa yanaenda kwenye uwekezaji.
Watu waliofanikiwa wanapopata kipato chao hawaelekezi kipato chao chote kwenye matumizi ya kawaida. Asilimia kubwa ya kipato chao huwa wanakielekeza kwenye uwekezaji. Kila wanapopata kipato, asilimia Fulani wanawekeza kwenye biashara, kwenye kununua hisa, kwenye kununua hatifungani na kadhalika. Kabla ya kuanza kufanya matumizi ya kawaida, jambo la kwanza kabisa huwa wanatenga pesa kwa ajili ya uwekezaji. Hebu jiulize swali hili, kila unapopata pesa, ni asilimia ngapi unawekeza? Kama hauwekezi, na pesa yote unatumia kwa matumizi ya kawaida, basi hautaweza kufanikiwa. Haijalishi unapata kiasi gani cha pesa. Hata kama ni kidogo kiasi gani, kumbuka kutenga kwanza kiasi cha pesa ambacho utawekeza.
Kwa leo niishie hapo. Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ya kutosha kuhusiana na mambo wanayofanya watu waliofanikiwa ambayo hata wewe pia ukifanya utapata mafanikio makubwa. Kama una maoni au swali lolote usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana name kwa simu namba 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazofuata.

Vikwazo 3 Vya Kushinda Ili Utimize Malengo Yako

Jinsi ya kutimiza MALENGO yako

Katika maisha kila mtu ana malengo au ndoto Fulani anayotamanai kuikamilisha ili aweze kufikia mafanikio. Hata wewe inawezekana una ndoto katika maisha yako unayotamani kuifikia. Inawezekana unatamani kufanya mambo makubwa kabla hujaondoka duniani. Lakini si wote wanaokuwa na malengo na ndoto katika maisha yao ambao wameweza kutimiza ndoto zao. Kuna sababu ambazo zinawafanya watu wengi washindwe kutimiza ndoto walizo nazo. Katika Makala ya leo nitakushirikisha vikwazo vitatu (3) ambavyo ni lazima uvishinde ili uweze kutimiza malengo yako.
Vikwazo 3 ambavyo ni lazima uvishinde kutimiza malengo yako.
1. Kutokuamini katika uwezo ulio nao.
Watu wengi sana wameshindwa kufikia kilele cha ndoto zao kwa sababu ya kutokuaminni katika uwezo walio nao. Hii inatokana na jinsi walivyoaminishwa toka wakiwa watoto, maneno ya walimu wao, maneno ya marafiki zao, mazingira waliyokulia na kadhalika. Wamekuwa wakisikia kwenye masikio yao maneno ya kukatisha tamaa kuwa hawawezi. Inawezekana hata wewe umekatishwa tamaa na wazazi, walimu, marafiki kuwa hauwezi. Ninataka nikuhakikishie kuwa una uwezo ndani yako wa kufanya makubwa na kutimiza malengo yako. Amini katika uwezo ulio nao na uchukue hatua. Amini kuwa una uwezo wa kuwa mtu mkubwa, amini kuwa unaweza kuwa bilionea na kadhalika. Usijidharau, una uwezo mkubwa sana uliojificha ndani yako ambao unachohitajika tu kufanya ni kuchukua hatua.
2. Kuamini kuwa kuna mtu yupo mahali fulani atakusaidia.
Katika maisha, hatma ya maisha yako unaipanga wewe mwenyewe. Hakuna mtu ambaye yupo kwa ajili ya kukusaidia katika maisha yako. Hata kama yupo, tambua kuwa sio wajibu wake kufanya hivyo. Hivyo ni lazima uchukue hatua wewe mwenyewe kwa asilimia mia moja kutimiza malengo yako. Kumbuka kuwa unapokuwa umeanza kuchukua hatua watu watakuja kukushika mkono wakiona tayari umekwisha anza. Kama malengo yako ni kuwa mwandishi, anza kuandika, kama ni kufanya biashara anza kwa kiasi chochote ulicho nacho. Hata kama hauna mtaji kabisa, tumia nguvu zako kuweza kupata mtaji wa kuweza kuanzisha biashara yako. Jambo la kuzingatia hapa ni wewe kuanza, haijalishi una hali gani. Unapokuwa umeanza, fursa zingine za kukufanya usonge mbele zitafunguka.
3. Kukata tamaa.
Kikwazo kingine ambacho kinaweza kukufanya ushindwe kutimiza malengo yako ni kukata tamaa. Watu wengi wameshindwa kutimiza malengo yao kwa sababu baada ya kuanza walipopata changamoto walikata tamaa na wakaamua kuacha malengo yao. Hata wewe inawezekana tayari umeamua kuchukua hatua, jambo la msingi ni kuendelea haijalishi utapitia changamoto kubwa kiasi gani, usikate tamaa. Endelea kupambana kwani mafanikio hayaji kwa urahisi, yanahitaji kujitoa kwa nguvu zako zote na akili yako yote. Hapa unatakiwa kupuuza maneno yote uliyoambiwa na ambayo unaweza kukutana nayo kuwa hauwezi. Maneno yoyote yale ambayo yatakuvunja moyo na kukukatisha tamaa yapuuze na upige hatua na mafanikio utayaona. Kama bado haujachukua hatua ni lazima utambue kuwa unapoanza kuchukua hatua kutimiza malengo yako kuna wakati utapitia nyakati ambazo zitakufanya ukate tamaa. Usikubali endelea kuchukua hatua mpaka pale utakapokuwa umetimiza kusudi la maisha yako.
Nimatumaini yangu kuwa umepata maarifa ambayo yatakusaidia kuchukua hatua muhimu sana kwa ajili ya kutimiza malengo yako. Kama una maoni au swali lolote, usisite kuweka maoni au swali lako hapa chini. Pia kwa ushauri wowote, usisite kuwasiliana nami moja kwa moja kwa simu no. 0752 081669. Asante na karibu tena kwenye Makala zinazokuja.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp