Kila Aliyefanikiwa Alifanya Uamuzi Huu Mkubwa.

Kila Aliyefanikiwa Alifanya uamuzi huu Mkubwa

Katika maisha kila mmoja wetu anahitaji kufanikiwa. Lakini katika mafanikio kuna kanuni ambazo kila ambaye anahitaji kufanikiwa anapaswa kuzifahamu na kuzifanyia kazi. Na ndio maana katika maisha kuna watu waliofanikiwa na ambao hawajafanikiwa japokuwa wote wanawekeza juhudi kubwa kutafuta maisha. Hivyo kuna moja ambalo watu waliofanikiwa huwa wanalifanya na hivyo kuwatofautisha na watu wengine ambao hawafanikiwi. Katika Makala hii, tutaangalia jambo kubwa au uamuzi mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Tunapozungumzia mafanikio ni pana sana. Kwa mujibu wa Makala hii, mafanikio ni ile hali ya kufikia viwango ulivyojiwekea kwenye maisha yako. Viwango hivyo vinaweza kuwa: Kuwa na elimu kubwa, kuwa na biashara kubwa, Kuwa na kazi nzuri, Kukuza kipaji chako na kadharika. Hivyo katika Makala hii nitajikita kuelezea ni uamuzi gani mkubwa ambao kila aliyefanikiwa alifanya.

Sasa, nianze na tabia ambayo watu wengi ambao hawajafanikiwa wanayo. Tabia mojawapo ambayo watu ambao wameshindwa kufanikiwa wanayo ni tabia ya kurukaruka. Maana yake ni kuwa watu wengi wanafanya vitu ambavyo kwa asilimia 100 hawajaamua kufanya. Au kwa lugha nyingine ni kuwa, wanafanya vitu kwa kujaribu.

Kwenye maisha, kama hautaweka nguvu zako, akili zako na mawazo yako kwenye jambo unalotaka kufanya kwa asilimia mia moja, kamwe hautaweza kufanikiwa. Ndio maana watu wengi walioingia kwenye biashara walifeli, kwa sababu hawakuingia wazima wazima bali waliingia mguu mmoja ndani mwingine nje. Hivyo wakaweka nguvu kidogo hapo na pale kidogo. Hivyo wakashindwa kupata matokeo makubwa. Watu wa namna hiyo unakuta leo anafanya biashara hii, kesho anaona mwingine anafanya biashara nyingine na wao wanafuata. Hawawekezi nguvu zao sehemu moja.

Sasa ngoja nikusimulie habari hii itakupatia jambo la kujifunza.

Miaka mingi iliyopita kulikuwa na Kamanda mmoja wa kikosi cha Hispania cha Kijeshi aliyekuwa anaitwa Hernan Cortes. Mwaka 1519 alipewa kazi ya kwenda kuvamia kisiwa kimoja nchini Mexico kilichoitwa Berecluse na akapewa wanajeshi 500 na meli 11. Walipofika pale Kisiwani akaagiza wanajeshi wote washuke pamoja na wale mabaharia. Waliposhuka akaagiza meli zote zichomwe moto. Walipochoma moto na moshi ulipoanza kupanda juu, akawaita wale wanajeshi na wale mabaharia akawauliza, mnaona nini? Wakasema tunaona meli zetu zinaungua. Akasema, safi sana. Akawaambia, tuna chaguzi mbili tu zilizobaki hapa, tushinde vita au tushindwe vita tuangamie wote hapa. Hakuna njia mbadala tofauti na hizo.

Matokeo yake yalikuwaje?

Walikuwa wanajeshi wachache sana lakini vita walishinda. Kwa nini? Ni kwa sababu waliamua kwa asilimia mia moja kufanya kile kitu walichokuwa wanakifanya.

Jambo la kujifunza ni hili, ili uweze kufanikiwa kwenye jambo lolote, usiseme ninajaribu. Sema ninafanya. Chochote unachoamua kufanya, jitoe kwa nguvu zako zote na utaona matokeo makubwa. Kuanzia leo, usiseme najaribu jaribu, bali sema nafanya. Na ukiamua kufanya, CHOMA MELI ZAKO ZOTE na utashinda.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Jambo Linalokuchelewesha Kufanikiwa.

Mojawapo ya majuto ambayo watu wengi hupitia hasa umri wao unapokuwa umekwenda ni kuwa, hawakuishi maisha waliyokuwa wanayataka na kufanya kile kitu walichokuwa wanakipenda. Na pia hawakufikia malengo yao ya maisha kama walivyokuwa wanatamani kufikia. Katika Makala hii tutaangalia jambo kubwa ambalo limewachelewesha wengi kufanikiwa kufikia malengo yao ambalo pia linaweza kukufanya ushindwe kufanikiwa kwenye malengo yako na jinsi ya kukabiliana nalo.

Tafiti nyingi sana zinaonesha watu wengi sana hasa wanapokaribia kufa hujilaumu maisha waliyoishi. Mwanasaikolojia mmoja anayeitwa Daniel Amend aligundua kanuni nzuri sana inayoitwa 18, 40, 60. Kanuni hii ilikuwa inasema hivi:

Mtu anapokuwa na umri wa miaka 18-39 huwa anajiuliza nikifanya jambo hili, kazi hii au biashara hii watu watanionaje? Watu wa kundi hili maisha yote yanaendeshwa na maoni ya watu na sio utashi wao.

Mtu huyu akifikisha umri wa miaka 40-59 huwa anaanza kusema, kwa sasa umri wangu umekwenda hivyo sitojali. Mimi nitafanya, mwenye kunisema na aniseme lakini mimi nitafanya ili kufanikiwa.

Mtu huyu anapofikisha umri wa miaka 60 na kuendelea anakuja kugundua kuwa, watu aliokuwa anawafikiria kuwa wanamuwazia yeye hawakuwa wanamfikiria kabisa na wala hawakuwa na mpango naye. Wao pia walikuwa wanahangaikia maisha yao.

Baada ya kuona kanuni hiyo utagundua kuwa ndivyo maisha yalivyo. Watu wengi wanaishi wakiogopa kufanya kitu ambacho kingebadilisha maisha yao wakifofia kuwa watu watawaonanje au kuwafikiriaje. Kumbe wale ambao wanawahofia na wao wana mambo yao na wala hawana muda wa kuwafirikia.

Jambo kuwa ambalo unapaswa kulizingatia ili uweze kufanikiwa ni kuwa, usiwe mtu wa kuishi ili kuwaridhisha watu. Ishi maisha yako. Kama una malengo ya maisha uliyojiwekea na unahisi kuwa ukiyafanya yatabadilisha maisha yako, fanya kwa nguvu zako na akili zako zote. Usihofu kuwa watakuonaje. Kumbuka kuwa hakuna aliye na muda wa kujali au kuangalia maisha yako. Ukiwaangalia na kuwahofia watu, unajichelewesha mwenyewe.

Mfano, watu wengi wanaishi kwenye nyumba zenye gharama kubwa kupita uwezo au kipato chao, wamechukua mikopo wakanunua magari ili kuwaridhisha watu, wananunua nguo za gharama kubwa kuliko uwezo wao. Hii ni kwa sababu walitaka kuwaridhisha watu na hivyo wakajikuta wapo kwenye msongo mkubwa wa madeni katika maisha yao.

Kitu cha msingi katika maisha yako ni kuishi maisha yako na kufanya kitu unachokipenda ambacho unaona kitaleta mapinduzi kwenye maisha yako bila kuangalia watu watasemaje. Nimatumaini yangu umepata maarifa ya msingi sana ambayo yatakusaidia kufanikiwa kufikia malengo yako. Kama una maoni yoyote, usisite kuweka maoni yako hapa chini. Pia unaweza kuwasiliana name moja kwa moja kama utahitaji ushauri zaidi kwa simu na. 0752 081669. Asante na karibu katika Malala ijayo.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Jambo Moja La Kuzingatia Ili Uweze Kufanikiwa Katika Maisha.

Karibu mpendwa msomaji katika Makala hii ya leo. Katika Makala hii nitaelezea jambo moja kubwa unalopaswa kulizingatia na kulifanyia kazi ili uweze kufanikiwa katika maisha. Inawezekana umekuwa ukitumia juhudi kubwa katika kazi zako ili uweze kujikwamua kimaisha lakini matokeo yanakuwa hayaonekani. Nikuhakikishie kuwa ukifuatilia Makala hii mwanzo hadi mwisho utakuwa umepata kitu cha msingi sana ambacho kitakusaidia uweze kufanikiwa katika maisha yako. Karibu tuendelee.

Je ulishawahi kujiuliza ni kitu gani kinawatofautisha watu waliofanikiwa sana na wale ambao hawajafanikiwa? Katika Makala hii ya leo ningependa nikushirikishe kitu kimojawapo ambacho kinaweza kukusaidia sana kwenye maisha yako. Kitu hicho ni uwezo wa kupanga malengo na kuyafuatilia.

Watu  wengi wanaamka kwenda kazini lakini ukiwauliza baada ya miaka kumi watakuwa akina nani hawawezi kukujibu. Sasa hebu nikushirikishe utafiti uliowahi kufanywa na Chuo Kikuu cha Havard cha nchini Marekani.

Chuo kikuu cha Havard mwaka 1979 kwenye kitengo cha biashara walifanya utafiti. Walikusanya wanafunzi 100 ili waweze kuwafanyia utafiti. Utafiti huo ulikuwa ni wa kuwauliza maswali. Waliwauliza kuwa,  wakimaliza shule baada ya miaka kumi watakuwa ni wapi ki-maisha au watakuwa na mafanikio gani? Wanafunzi hao walitoa majibu kama ifuatavyo:

Asilimia 84 ya wanafunzi walikuwa hawajui watakuwa wapi, hivyo hawakuwa na mpango wowote katika maisha yao. Walikuwa wakisoma lakini walikuwa hawajui maisha yao yatakuwaje.

Asilimia 13 ya wanafunzi  walikuwa wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote wa jinsi ya kupata kile kitu walichokuwa wanahitaji kwenye maisha yao.

Asilimia 3 ya wanafunzi walisema wanajua wanachokitaka na walikuwa wametengeneza mpango kamili wa jinsi ya kufanikiwa kupata kile walichokuwa wamekusudia kukipata.

Utafiti huo uliendelea baada ya miaka kumi .Baada ya miaka 10 Chuo cha Havard kiliwafuatilia wanafunzi hao ili kiweze kupata matokeo ya utafiti wao. Matokeo yaliyopatikana yalikuwa ni ya kushangaza.

Katika matokeo hayo:

Wale wanafunzi asilimia 13 ambao walisema wanajua wanachokitaka lakini hawakuwa na mpango wowote walikuwa wamefanikiwa  mara mbili zaidi ya wale asilimia 84 waliosema hawajui wanataka nini katika maisha yao.

Wale wanafunzi asilimia 3 ambao walisema wanajua wanachokitaka na wametengeneza mpago kamili wa jinsi ya kufanikiwa walikuwa wamefanikiwa mara 10 zaidi ya wale wanafunzi wengine wote.

Utafiti huu ukahitimisha kuwa, unapokuwa na malengo yako na ukayaishi, una uwezo wa kufanikiwa mara 10 zaidi ya wale ambao hawana malengo.

Kuanzia leo usiwe mtu asiyekuwa na malengo. Tumia muda kutafakari na kujiuliza miaka 10 ijayo utakuwa wapi?

Utakuwa na kiwango gani cha elimu.

Utakuwa na cheo gani.

Utakuza biashara yako kwa kiwango gani na kadhalika.

Hivyo, uwezo wa kupanga malengo na kuyaishi ni muhimu sana katika maisha yako. Usiishi kama mtu asiyekuwa na mwelekeo. Weka malengo na upange namna ya kuyafikia. Unapoamka asubuhi hakikisha unapitia malengo yako uliyojiwekea ili usiweze kupoteza muda wako kwa mambo ambayo yako nje ya malengo yako.

Chukua muda kutafakari na kupanga malengo yako unataka kuwa nani na wapi katika maisha. Unaweza kunishirikisha kwa kukomenti hapo chini. Asante sana na karibu katika Makala ijayo.

error

Enjoy this blog? Please spread the word :)

Follow by Email
WhatsApp